|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
KUISHI NI KRISTO NA KUFA NI FAIDA Salamu,
Kwa Watakatifu, watu wa Mungu aliye Baba yetu, na Baba wa Bwana wetu
Yesu Kristo. Tunamshukuru Mungu wetu katika Yesu Kristo kwa ajili yenu,
kwa kuwa mnazidi kudumu katika tumaini la imani iliyo katika Yesu Kristo.
Kwa maana Mungu tumwabuduye kwa roho zetu katika Injili ya Mwana wake,
ni shahidi wetu jinsi tuwatajavyo katika sala zetu mara kwa mara pasipo
kukoma. Amestahili yeye, Bwana wetu na Mungu wetu, kuupokea utukufu na
heshima na uweza, kwa kuwa yeye ndiye aliyeviumba vitu vyote, na kwa
sababu ya mapenzi yake vilikuwako, navyo viliumbwa.
Tunawasalimu popote mlipo msomapo ujumbe huu ni katika Jina lile
lipitalo majina yote, Jina la Yesu Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai,
Bwana na Mwokozi wetu. Kwa kuwa ujumbe tulionao ni mrefu tumeona tuweke
kwa ajili ya miezi miwili – lakini kwa pamoja. Kusudi la kuwaandikia Usishangae unapoona umeushika ujumbe huu umekufikia hapo ulipo na kuusoma. Si bahati mbaya wala si bahati nzuri, bali ni mpango wa Mungu. Wakati fulani kama miaka kadhaa iliyopita tuliamua kuomba, baada ya kuona kwa macho, na kusikia kwa njia ya redio na kwa vinywa vya watu, na pia kwa kusoma katika magazeti jinsi ambavyo wakristo wengi hasa waliozaliwa mara ya pili wanavyokufa. Wakristo wengi wamekuwa wakifa wakiwa bado vijana kwa njia mbalimbali, lakini wengi ni kwa njia ya magonjwa na ajali za barabani Wakristo wengi wanaokufa karibu kila siku ni wa umri kati ya miaka ishirini na miaka hamsini. Tukawa tunasikia watu wengi wakisema ni mapenzi ya Mungu vifo hivyo vitokee. Lakini ndani ya mioyo yetu hatukupata amani juu ya vifo hivi.
Ndipo tulipoamua kuomba
kumuuliza Mungu ni sababu gani zinazofanya watu wake wafe wakiwa na umri
mdogo namna hii wakati bado wanahitajika katika kazi ya kueneza injili,
wanahitajika na taifa, na wanahitajika na ndugu zao pia. Na Bwana Mungu
alitujibu .
Na tangu wakati huo,
Bwana ametuwezesha kulihubiri jambo hili mahali mbali mbali. Lakini
ndani ya mioyo wetu tunashuhudiwa ya kuwa ujumbe huu unatakiwa uwafikie
watu wa Kristo wengi, wausome, wautafakari na kuufanyia kazi.
Na hilo ndilo kusudi
la kuwaandikia, muusome, muutafakari na kuufanyia kazi. Ni maombi yetu
kwa Bwana ya kuwa kwa uwezo wa Roho wake aliye Mtakatifu utakayoyasoma
humu yatakuwa msaada kwako. Kushibishwa
kwa wingi wa siku
Tunaamini umewahi kusikia watu wengi wakisema ‘kila mtu ameandikiwa
siku yake ya kufa, ikifika siku hiyo hata akiwa wapi atakufa’. Watu
wengi wanausema usemi huu, na walio wengi wanaamini ya kuwa ndivyo Mungu
alivyopanga.
Lakini kwetu sisi kama
watu wa Kristo ni vigumu kuuamini usemi huu kwa kuwa hauendi sambamba na
Neno la Mungu.
Biblia inasema katika
kitabu cha Waebrania 9:27, “Na kama vile watu wanavyowekewa kufa mara
moja, na baada ya kufa hukumu”. Mstari huu hausemi watu wamewekewa
kufa siku moja. Huu mstari unasema watu wamewekewa kufa MARA moja na
SIYO kufa siku moja. Mara moja na siku moja ni maneno yanayomaanisha
mambo mawili tofauti. Imeandikwa; “
Bwana akasema,Roho yangu haitashindana
na mwanadamu milele, kwa
kuwa yeye ni nyama, basi siku zake
zitakuwa miaka mia na ishirini” (Mwanzo 6:3).
Ingawa kuna watu wengi ambao hawafiki hata nusu ya miaka mia na ishirini,
lakini kuna watu ambao wameishi zaidi ya miaka mia na ishirini.
Na katika sehemu
mbalimbali katika Biblia imeandikwa ya kuwa ukifanya mambo fulani siku
zako zitafupishwa; na ukifanya mambo fulani siku zako zitaongezwa. Kwa
hiyo kuishi kwako hapa duniani kutategemea sana jinsi unavyotembea
katika mapenzi ya Mungu.
Si mpango wa Mungu
katika Yesu Kristo ufe ungali kijana au mtu wa makamo. Hebu
soma maneno haya:- “Kwa
hiyo Bwana Mungu asema hivi,Tazama watumishi wangu watakula, bali ninyi
mtaona njaa;tazama, watumishi wangu watakunywa, bali ninyi mtaona kiu;
tazama, watumishi wangu watafurahi, bali ninyi mtatahayarika.
……Hatakuwepo tena mtoto wa siku chache, wala mzee asiyetimia
siku zake; kwa maana mtoto atakufa mwenye umri wa miaka mia; bali mtenda
dhambi mwenye umri wa miaka mia atalaaniwa”. (Isaya 65:13,20).
Unaposoma mistari ya
namna hii, mara moja unaanza kujiuliza kwa nini watu wa Kristo hufa
kabla ya kufikia miaka mia, wakati imeandikwa ya kuwa watoto watatimiza
miaka mia? Pia
imeandikwa; “Aketiye
mahali pa siri pake Aliye juu Atakaa katika uvuli wake Mwenyenzi ……………….Kwa
siku NYINGI nitamshibisha, nami nitamwonyesha wokovu wangu” (Zaburi
91:16)“Ili wafarijiwe mioyo yao, wakiunganishwa katika upendo,
wakapate utajiri wote wa kufahamu kwa hakika, wapate kujua kabisa siri
ya Mungu, yaani, Kristo’ (Wakolosai 2:2).
Aliyeahidiwa kushibishwa kwa wingi wa siku ni yule ambaye anakaa ndani
ya Kristo aliye siri ya Mungu. Kama umezaliwa mara ya pili na Kristo
anakaa ndani yako, na wewe ndani yake ahadi hii ya yako.
Je! unaelewa maana ya
kushibishwa kwa wingi wa siku?
Ngoja tukupe mfano.
Mtu anapoweka chakula
kingi mezani; Ni yule anayekula anaye mwambia NIMESHIBA. Yeye awekae
chakula hapimi kushiba kwa yule anayekula. Anayekula ndiye asemaye
ameshiba, na kama hajashiba anaweza kuongezewa chakula.
Na hivi ndivyo Mungu
anavyofanya. Ametuwekea siku nyingi za kuishi juu ya nchi, ziko mbele
yetu. Tunatakiwa tukae hapa duniani hadi tushibe! SISI ndio tunaotakiwa
kumwambia Mungu ya kuwa tumeshiba!Tutashibishwa kwa wingi wa siku.
‘Kushiba’ hapa
inamaana siku ya kumaliza kazi tuliyopewa na BWANA tuifanye; au siku ya
Yesu Kristo kurudi kutuchukua mara ya pili. Ndiyo maana Yesu Kristo
akasema, “Mimi nimekutukuza duniani, hali NIMEIMALIZA KAZI ILE
ULIYONIPA NIIFANYE” (Yohana 17:4). Kwa
nini tupo duniani sasa
Ukiangalia kwa makini
hali ya watu wa Mungu; wale waliozaliwa mara ya pili kwa Neno la Kristo;
wale walioupokea wokovu kwa njia ya Injili, unashindwa kusoma katika
maisha yao sababu hasa ya Mungu kumwokoa mtu, na bado amwache hapa
duniani.
Tulikuwa hatuoni
sababu kwa nini Mungu amwokoe mtu, amfanye kuwa Mwana kwake na yeye kuwa
Baba, na bado amwache katika dunia iliyojaa majaribu, mahangaiko, dhambi
na magonjwa.
Hebu jiulize hata wewe,
kwa nini Mungu alikuokoa kwa muda na mazingira tofauti na mwingine? Na
baada ya kukuokoa akakuacha uendelee kuishi hapa duniani? Lazima kuwe na
sababu!
Mungu wetu ni Mungu
aliye na mipango na makusudi kamili juu ya kila neno analolisema na kila
jambo analolifanya. Tafakari
maneno haya:
“Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida "(Wafilipi
1:21).
Ikiwa kufa kwa watu wa
Mungu, kufa ni faida kwa nini wanaomba
walindwe wakiwa hapa duniani?
Kufa na kuondoka hapa
ulimwenguni ni faida kwa mtu wa Mungu, kwa kuwa anayaacha matatizo ya
dunia hii na anakwenda kuishi pamoja na Kristo katika raha na utulivu
milele.
Lakini jibu swali hili;
kwa nini unaomba ulinzi wa Mungu usife, usipatwe na ajali yoyote
itakayokatisha maisha hapa duniani?
Na wakati mwingine
kukiwa na hatari mbele yako usiyoifahamu, Roho wa Mungu anakuhimiza
kuomba? Na mara nyingine pia huinua watu wengine waombe kwa ajili yako
usidhurike, kwa nini iwe hivyo?
Hii inatupa picha tu
ya kuwa kuna sababu kubwa sana ambayo Mungu anayo ya kutuacha hapa
duniani, na kutulinda, na kutulisha badala yakutuchukua mara tu baada ya
kuokoka.
Kuna kitu ambacho
Mungu anatarajia tukifanye hapa duniani, ambacho ni muhimu sana kwake,
kiasi kwamba inabidi atulinde ili tukifanye!
Kuna kusudi kamili la
wewe kuwapo hapa duniani wakati huu. Neno la Mungu linatuambia kuwa
kukaa kwako katika mwili huu, kuna faida kubwa kwa watu wengine. “Ila
ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi
ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua
silitambui. Ninasongwa katikati ya mambo
mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na
Kristo; maana ni vizuri zaidi sana; bali kudumu
katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu” (Wafilipi
1:22-24)
Tulipokuwa tunaendelea kutafakari sababu za sisi kuwepo hapa duniani
baada ya kuokoka, Roho wa Mungu alituongoza kusoma mstari huu: “Basi
tu wajumbe kwa ajili ya Kristo” (2Wakorintho 5:20)
Kuwa mjumbe kwa ajili ya Kristo maana yake nini? Tunatakiwa tuwe wajumbe
kwa ajili ya Kristo juu ya nini? Na kwa namna gani? Na kwa nani? Na kwa
wakati gani? Neno la Kiingereza lililotafsiriwa kuwa mjumbe ni
‘Ambassador” Na neno zuri linalotoa picha nzuri ya maana ya
‘Ambassador’ ni neno Balozi. Balozi ni mjumbe na mjumbe ni balozi
Neno balozi na neno mjumbe lina maana sawa lakini kwa jinsi
tunavyoyatumia maneno haya, utafikiria neno balozi lina uzito zaidi
kuliko neno mjumbe.
Kwa hiyo tunaweza
kusema: “ Basi tu mabalozi (wajumbe) kwa ajili ya Kristo” Katika
nchi ya Tanzania tuna mabalozi wa nyumba kumikumi, ambao pia
wanajulikana kuwa ni wajumbe wa nyumba kumikumi. Pia tuna mabalozi
walioko nchi za nje waliotumwa kuiwakilisha nchi hii katika maswala na
majukumu mbalimbali.
Sasa na tuliangalie
katika ngazi ya kitaifa. Balozi ni mjumbe au mwakilishi wa nchi moja
katika nchi nyingine. Kwa mfano: Balozi wa Tanzania nchini Kenya; kwanza
ni raia wa Tanzania anayefahamu vizuri msimamo wa nchi hii katika
maswala mbalimbali. Yuko Kenya kwa ajili ya Serikali ya Tanzania na raia
wa Tanzania.
Yeye ndiye msemaji
mkuu wa Serikali ya Tanzania nchini Kenya. Serikali ya Tanzania
inapopeleka ujumbe kwa serikali ya Kenya, inapitia kwa balozi wake
aliyeko Kenya.
Balozi huyo ni picha
kamili ya Watanzania kwa watu wa Kenya, katika maneno yake na mwenendo
wake. Yeye ni mlinzi wa hadhi ya Tanzania nchini Kenya. Na makazi yake
ni nchini Kenya.
Balozi ni mjumbe
aliyetumwa na mtu mwingine. Balozi wa Tanzania katika umoja wa Mataifa,
ametumwa na nchi yetu, awe msemaji na mtetezi wa mawazo ya Tanzania
katika maswala mbalimbali ya kimataifa. Balozi hasemi mawazo yake
mwenyewe. Balozi anasema tu kile alichotumwa kusema na anafanya kile tu
ambacho ametumwa kufanya.
Tunasisitiza hivi,
BALOZI HASEMI MAWAZO YAKE MWENYEWE: BALOZI ANASEMA TU KILE ALICHOTUMWA
KUSEMA, NA ANAFANYA KILE TU AMBACHO AMETUMWA KUFANYA.Na kitu cha kwanza
anachofanya anapofika katika nchi aliyotumwa ni kutoa vitambulisho
vilivyo na muhuri na sahihi ya kiongozi wa nchi anayotoka.
Biblia inatuambia kuwa
sisi ni mabalozi kwa ajili ya Kristo hapa duniani; sisi ni wajumbe
tuliotumwa kwa ajili ya Kristo hapa duniani. Ndiyo maana Paulo alisema
kuishi kwake ni Kristo. Wewe ni mjumbe wa Kristo na kwa ajili ya Kristo
hapa duniani. Ikiwa wewe ni Mjumbe, basi wewe ni balozi wa Kristo na kwa
ajili ya Kristo.
Kumbuka kuwa balozi
hasemi mawazo yake mwenyewe. Wewe ni balozi wa Kristo hapa duniani kwa
hiyo kutokana na wadhifa huo uliopewa unatakiwa usiseme mawazo yako,
wala kufanya mambo yako hapa duniani; bali USEME MAWAZO YA KRISTO NA
MANENO YAKE; NA UFANYE YAKE TU ALIYOKUTUMA KUFANYA.
Lakini ni wazi kwamba
huwezi kusema mawazo na maneno ya Kristo wakati huyafahamu. Na ikiwa
hapa duniani wewe ni balozi basi, inamaanisha hapa duniani si kwako. Na
ikiwa hapa duniani si kwako, na wala wewe si mwenyeji wa hapa duniani;
basi unatokea wapi na uenyeji (uraia) wako ni wa wapi? Wewe ni mwenyeji
wa wapi? Hili swali ni muhimu sana ambalo ni budi ufahamu jibu lake
katika roho yako. Bila kufahamu ulikotoka utaifanye kazi ya ubalozi au
ya kuwa mjumbe wa Kristo. Balozi (Mjumbe) yeyote anajua alikotoka;
anafahamu uraia wake ni wa wapi. Je wewe unafahamu kuwa wewe ni balozi
wa nchi gani ukiwa hapa duniani?
Tunakazia swali hili
kwa sababu ujumbe utakokuwa unatoa; au mahubiri unayofanya mbele za watu;
na matendo yako yanategemea sasa mahali gani umetoka kiroho na
kimazingira.
Kuna wengine ni
mabalozi wa miili yao wenywe. Wanahubiri kwa sababu ya mwili ili wapate
mishahara yao na kuvaa. Wao wanaona kuwa kuhubiri ni kama kazi nyingine
ya kuajiriwa.
Lakini
la kushangaza ni kwamba wote wanasema ni mabalozi wa Kristo,
wajumbe wa neno la Injili. Na hii si kweli. Muda umefika ambapo Roho wa
Mungu amekududia kuliweka wazi hili. Mabalozi wa Kristo wawe wazi;
mabalozi wa madhehebu wawe wazi, na mabalozi wa miili yao wawe wazi.
Muda umefika wa
kufichuliwa watu wote wanaojiita mabalozi wa Kristo, wameokoka, na ni
wakristo, watumishi wa Kanisa kumbe ni mbwa mwitu wakali wanaowaendea
watu wakiwa wamevaa mavazi ya Kondoo (Mathayo 7:15).
Muda umefika ambao
watu wote wanokaa karibu na wewe, vitu vyote vinavyokuzunguka, mahali
unapopita, watu wote hao wanaokuzunguka wajue, kwamba wanajua KUWA WEWE
NI BALOZI WA KRISTO MJUMBE KWA AJILI YA KRISTO!
UTASEMA MAWAZO NA
MANENO YA KRISTO. NA UTAFANYA MATENDO YA KRISTO KWA AJILI YA KRISTO
MAHALI POPOTE ULIPO NA UTAKAPOKUWA DUNIANI:
Kuishi kwako hapa duniani ni Kristo na kufa kwako ni faida! Mtume Paulo
alipoandika kuwa “Basi tu wajumbe (Mabalozi) kwa ajili ya Kristo,”
alikuwa anamhusisha kila mtu ambaye amefanyika kuwa kiumbe kipya ndani
ya Kristo. Ikiwa wewe ni kiumbe kipya ndani ya Kristo, basi wewe ni
mjumbe(balozi) kwa ajili ya Kristo.
Ikiwa basi wote
waliozaliwa mara ya pili, walio viumbe vipya ndani ya Kristo (waliookoka)
wanatakiwa kuwa mabalozi wa Kristo; mbona basi ubalozi wao hauonekani
ukifanya kazi? Ubalozi hauonekani katika maisha yako, kwa sababu
hujafuatilia katika Biblia kujua neno linasemaje juu ya hili. Laiti basi
Kanisa lingefahamu uzito wa wadhifa huu wa kuwa mjumbe wa Kristo hapa
duniani, hali ya mambo isingekuwa kama ilivyo sasa ya kukata tamaa –
iliyojaa katika mioyo ya watu.
Laiti basi wewe
ungejua uzito wa wadhifa huu wa kuwa mjumbe wa Kristo mahali ulipo ikiwa
in nyumbani, kazini, safarini, kanisani, sokoni, hali ya mambo
isingekuwa kama unavyoiona sasa. Wewe
mkristo ni raia wa mbinguni. “Basi
tangu sasa ninyi si wageni wala Wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja
na watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu” (Waefeso 2:19). Yesu
Kristo alipokuwa akituombea alisema: “Mimi
nimewapa neno lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa WAO SI WA
ULIMWENGU, kama mimi nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi kwamba uwatoe
katika ulimwengu; bali uwalinde na yule muovu. Wao SI WA
ULIMWENGU KAMA MIMI NISIVYO WA
ULIMWENGU. Uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli. Kama
vile ulivyonituma mimi ulimwenguni, nami vivyo hivyo NILIWATUMA HAO
ULIMWENGUNI (Yohana 17:4-18)
Weka jambo ili katika
moyo wako. Watu wa Kristo si wa ulimwengu huu, bali ni wenyeji wa
mbinguni. Watu wa Kristo wako hapa ulimwenguni kwa sababu Kristo
amewatuma kufanya kazi muhimu. Kumbuka upo hapa duniani kwa kuwa kuna
KAZI ambayo KRISTO amekupa uifanye kabla ya kurudi nyumbani kwetu
MBINGINU. Kwa
nini Wakristo wanakufa kabla ya kukamilisha kazi walizopewa:
Tulipokuwa tunaomba kwa ajili ya Watakatifu wa Mungu, popote walipo hapa
nchini, Bwana akatujibu na kutuambia maneno yafuatayo ndani ya mioyo
yetu. “Watu wangu wengi wamefunikwa na roho ya mauti bila ya wao
kufahamu. Na wengi wanaangamia.”
Utajuaje ya kuwa
umefunikwa na roho ya mauti? Watu wengi huwa wakifunikwa na roho ya
mauti kwanza huwa wanaingiwa na hofu ya kufa, na pili huwa wanaona
wanaweza kufa wakati wowote, na tatu huwa wanajiandaa kufa kwa kutubu,
kulipa madeni au kwa kuandika wosia, na wakati mwingine hata kuanza
kugawa mali zao.
Ukiona una hali ya
namna hii ujue umefunikwa na roho ya mauti!
Tunamkumbuka mama
mmoja aliyeokoka aliyetuambia; “Ndugu, kwa muda sasa nimekuwa nikiona
moyoni mwangu ya kuwa nitakufa karibuni. Nimepambana na wazo hili kwa
muda mrefu naona wala haliondoki. Kwa hiyo nimetubu na kutengeneza mambo
yangu kwa sababu naona nitakufa karibuni”
Mimi nikamwambia; “
Kweli kufa kwa mkristo ni faida kwa kuwa atakwenda kukaa na Yesu Kristo
milele. Lakini kumbuka Yesu Kristo alisema ametutuma ulimwenguni kama
yeye alivyotumwa. Je! unaposema uko tayari kufa, umekwisha maliza
kuifanya kazi aliyokuagiza uifanye? Je! utakuwa na matunda gani ya kazi
mikononi mwako utakapokwenda kuonana na Bwana Yesu Kristo baada ya kufa?
Yule mama akatujibu
akasema; “Mmeniambia jambo muhimu ambalo sikulifikiria, kwani ingawa
nafanya kazi ya Mungu lakini sina uhakika kama ndiyo kazi niliyoitiwa
niifanye. Sasa mnanishauri nifanye nini?
Wakristo wengi wako
katika hali ya namna hii. Na tulipokuwa tunaendelea kuomba kwa ajili ya
tatizo la roho ya mauti juu ya watu wa Kristo, Bwana alitupa sababu tano
ambazo zinawafanya wakristo wafe kabla ya kumaliza kazi aliyowapa.
Kumbuka tunaposema juu
ya kifo, hatuna maana kufa kiroho, bali kufa kimwili yaani roho ya mtu
kutoka katika mwili. Kuna sababu nyingi hata zaidi ya tano ambazo
zinawafanya watu wa Kristo wafe kabla ya kushiba wingi wa siku. Lakini
katika barua hii huu tutakushirikisha tano tu ambazo Bwana alitupa ili
watu wake wazitafakari. 1.
Kutokuwaheshimu wazazi “Enyi
watoto, watiini wazazi wenu katika
Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu
baba yako na mama yakoamri hii ndiyo amri ya kwanza yenye
ahadi, upate heri, ukae SIKU NYINGI
KATIKA DUNIA” (Waefeso 6:1-3) “Waheshimu
baba yako na mama yako, kama
Bwana, Mungu wako, alivyokuamuru, SIKU
ZAKO ZIPATE KUZIDI, nawe upate kufanikiwa
katika nchi upewayo na Bwana,
Mungu wako” (Kutoka 5:16).“Na alaaniwe amdharauye baba yake
au mama yake. Na watu wote waseme,
Amina” (Kumb. 27:16).
Tatizo la kutowaheshimu wazazi linazidi kuwa kubwa sana siku hizi
na hasa katika jamii ya Kikristo. Kama vile tunavyomheshimu Mungu kwa
vitu na mali tulizonazo, inatupasa kuwaheshimu wazazi wetu kwa vitu na
mali tulizonazo. Inabidi ukumbuke yakuwa walijinyima vingi kukutunza
ulipokuwa mdogo ili usome na uwe na maisha mazuri baadaye. Lakini hata
kama wazazi wako hawakukusomesha, wewe kama mkristo ni muhimu uonyeshe
upendo kwao kwa kuwagawia ulicho nacho. Iko faida gani wewe kuishi
maisha mazuri na kula na kusaza, wakati wazazi wako wanateseka na maisha
magumu na kukosa chakula na huku wana mtoto waliyemzaa kama wewe?
Vijana wengi
waliookoka wakitaka kuoa au kuolewa huwa wanawapuuza sana wazazi wao.
Utawasikia wakisema, “Wazazi wangu hawajaokoka kwa hiyo hata
nikiwashirikisha jambo hawawezi kuelewa.”
Lakini tunataka
ukumbuke ya kuwa Biblia haisemi uwaheshimu wazazi waliookoka na
uwadharau wazazi wako wasiookoka. Imeandikwa, “Enyi watoto, watiini
Wazazi wenu KATIKA BWANA………. Waheshimu baba yako na mama yako
………….. ukae SIKU NYINGI KATIKA DUNIA”.
Kutokuwatii na kutokuwaheshimu wazazi wako kunafanya SIKU ZAKO ZA
KUISHI ZIWE FUPI – UNAKUFA MAPEMA. Na kuwadharau wazazi kunakuletea
laana. Usije ukasema wazazi wako wamekulaani, bali kumbuka imeandikwa
alaaniwe amdharauye baba yake au mama yake.
Ikiwa wazazi wako wanakuambia ufanye mambo yaliyo kinyume na neno
la Mungu, si hekima kugombana nao na kuwadharau. Kumbuka vita vyetu si
vya mwili, wala si juu ya nyama na damu. Wewe wapende wazazi wako,
waombee na ombea jambo ambalo hamwelewani nao, na Bwana atakujibu; kwa
kuwa ameahidi kujibu. Uwe mvumilivu, usifanye maamuzi ya haraka, kwani
yote yawezekana kwake aaminiye. “Tazama, mimi ni Bwana, Mungu wa wote
wenye mwili. Je! KUNA NENO GUMU LOLOTE NISILOLIWEZA?” (Yeremia 32:27)
Ole, ni kwa wale ambao
hawapatani na WAKWE ZAO! Mkwe wako
ni mzazi wako ukimdharau unapokea laana; na usipomheshimu siku zako za
kuishi duniani zinafupishwa!
Watu wa Kristo wengi
wamenaswa na kutokutii andiko hili. Wengi wao ingawa si wote wamekufa na
wake zao wamekuwa wajane na kubaki na watoto wadogo. Na wengine wamekufa
na kuwaachia waume zao watoto walio wadogo. Ukifuatilia ndoa za marehemu
hao wengine wao (si wote) utakuta walifunga ndoa bila kuelewana na
wazazi wao; au wengine walikuwa hawapatani na wakwe zao. 2.
Kuchukia maonyo
Wakristo wengi huwa wanachukia wanapoonywa juu ya mienendo yao mibaya
isiyompendeza Mungu. Na wengine hata hudiriki kuwanunia wale
waliowaletea maonyo hayo. Lakini kuna hatari kubwa kuchukia maonyo. “Adhabu
kali ina yeye aiachaye njia;
Naye achukiaye kukemewa ATAKUFA”
(Mithali 15:10)
Adhabu kali ina yeye amwachaye Yesu Kristo kwa kuwa yeye ndiye
NJIA. Na unaelewa kwa nini wakristo hawapendi kukemewa wanapoambiwa ya
kuwa wanaenenda kinyume cha ushuhuda wa Yesu Kristo? Wanachukia kukemewa
kwa kuwa wamejaa mzaha. “Mwenye
mzaha hapendi kukaripiwa Wala
yeye hawaendei wenye hekima”
(Mithali 15:12) “Heri
mtu yule asiye kwenda katika shauri
la wasio haki; wala hakusimama
katika njia ya wakosaji; wala hakuketi
barazani pa wenye MIZAHA” (Zaburi 1:1) “Mwanangu,
usidharau kuadhibiwa na
Bwana, Wala usione ni taabu kurudiwa
naye. Kwa kuwa Bwana ampendaye
humrudia, kama vile baba mwanae
ampendezaye. Heri mtu yule aonaye
hekima, na mtu yule apataye ufahamu… ……… ana wingi wa
siku katika mkono wake
wa kiume, utajiri na heshima katika
mkono wake wa kushoto” (Mithali 3:11-13, 1,)
Kumcha Bwana ni kukataa uovu. Roho ya uchaji inakuongoza katika
njia za haki na siyo za uovu. Akukemeae uache maovu anakupenda kwani
hapendi uangamie. “Kumcha Bwana kwaongeza SIKU ZA MTU; bali miaka yao
wasio haki itapunguzwa” (Mithali 10:27). “Usiwe mwovu kupita kiasi;
wala usiwe mpumbavu; kwani ufe kabla ya wakati wako?” (Mhubiri 7:17) 3.
Kutumia ulimi vibaya
Ungefahamu mambo gani ambayo ulimi wako unaweza kufanya ungekuwa
mwangalifu katika yote uyasemayo. Hebu soma kwanza maneno yafuatayo: “Tumbo
la mtu litajazwa matunda ya
kinywa chake; atashiba mazao ya midomo
yake. Mauti na uzima huwa katika
uwezo wa ulimi, na wao waupendao
watakula matunda yake” (Mithali 18:20,21) “Enye
wazao wa nyoka, mwawezaje kunena
mema mkiwa wabaya? Maana, kinywa
cha mtu huyanena yaujazayo moyo
wake. Mtu mwema katika akiba njema
hutoa mema; na mtu mbaya katika
akiba mbaya hutoa mabaya. Basi, nawaambia,
kila neno lisilo maana, watakalo linena
wanadamu, watatoa hesabu ya neno hilo
siku ya hukumu. Kwa kuwa kwa maneno
yako utahesabiwa haki, na kwa maneno
yako utahukumiwa” (Mathayo
12:34-37)
Sheria ya ulimi ni hii, anachokiamini ndicho unachokisema;
unachokisema ndicho kinachotokea. “Basi
ulimi hakuna awezaye kuufunga; ni
uovu usiotulia, umejaa sumu iletayo
mauti. Kwa huo twamhimidi Mungu Baba
yetu, na kwa huo twawalaani
wanadamu waliofanywa
kwa mfano wa Mungu. Katika
kinywa kile kile hutoka baraka na laana. Ndugu zangu HAIFAI MAMBO
HAYA KUWA HIVYO” (Yakobo 3:8-10)
Siku hizi limekuwa jambo la kawaida kwa mkristo kusema maneno ya
baraka akiwa kanisani au ‘fellowship’, lakini kwa kinywa hicho hicho
kusema matusi nyumbani, na masengenyo kwa jirani zake.
Ndugu yetu, haifai
mambo hayo kuwa hivyo! Kumbuka vinywa vyetu ni mitego. Tunayoyasema
yanatufunga. Soma Mithali 6:2. Tunayosema yanaweza kuongeza siku za
kuishi hapa duniani au kuzifupisha. Kwa hiyo chunga unachokisema. 4.
Kuingilia wito wa mwenzako
Katika kanisa, Bwana ameweka huduma na karama mbalimbali. Na kazi ya
huduma na karama hizi ni kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya Kristo
itendeke; na kwa ajili ya kuujenga mwili wa Kristo.
Bwana ameita na kuwaweka wengine wawe mitume, wengine manabii,
wengine Wainjilisti, wengine Wachungaji na Waalimu. Wengine wamegawiwa
karama na vipawa mbalimbali. Na kila siku tunatakiwa tuenende kama
uustahilivyo wito wetu tulioitiwa. Mchungaji aenende kama mchungaji.
Nabii aenende kama nabii. Mtume aenende kama mtume. Mwinjilisti aenende
kama Mwinjilisti.
Jambo la kushangaza ni
kuona mtu aliyeitwa kuwa mwinjilisti anang’ang’ania kufanya kazi ya
uchungaji. Na utakuta pia mtu ameitwa kuwa mtume au/na nabii
anang’ang’ania kufanya kazi ya mwinjilisti au mchungaji au mwalimu.
Kuingiliana kwa wito namna hii kumeleta madhara na magomvi mengi kati ya
wakristo. Kwa nini uingilie ofisi na kazi ya mwenzako? Na kazi yako
unayoiacha ni nani atakayeifanya? Na mwenzako huyo unayemwingilia
unataka aende kufanya kazi wapi?
Hebu fikiria hali ya namna hii itokee katika kiwanda kimoja hapa
nchini. Mtu aajiriwe kuwa Meneja Masoko lakini yeye kila siku umkute
ameacha ofisi na kazi yake na kung’ang’ania katika ofisi ya Meneja
Utawala. Matokeo yake ni ugomvi na kukwama kwa kazi zote mbili na mwisho
kuanguka kwa kiwanda, kama huyo anayemwingilia mwenzake
asiposhughulikiwa kisheria.
Au fikiria mahali kama hospitali. Itakuwaje ikiwa daktari wa
macho aliyefundishwa na kuajiriwa kutibu wagonjwa wa macho, ukimkuta
anang’ang’ania katika wadi ya kuzalisha wakina mama waja wazito? Je!
anaweza kuzalisha bila kufundishwa? Na hao walioajiriwa kuzalisha waende
wapi? Na wagonjwa wa macho watibiwe na nani wakati daktari wa macho
ameihama ofisi yake?
Vivyo hivyo hata
katika kazi ya Mungu. Unapoingilia wito wa mwenzako unaleta madhara si
kwa mwenzako yule unayemwingilia tu, bali kwa mwili mzima wa Kristo.
Wakristo wote wanadhurika na kazi ya Bwana inasimama kwa sababu ya
machafuko hayo.
Katika agano la kale tunasoma ya kuwa mtu ambaye alikuwa
anaingilia Ofisi na na kazi ya kuhani Mkuu alikuwa anakufa hapo hapo.
Ofisi ya kuhani Mkuu ilikwa Patakatifu pa Patakatifu. Mtu mwingine
ambaye Mungu hakumteua na kumtakasa kuwa Kuhani Mkuu akiingia humo
alikuwa anakufa. Na Bwana alituambia tuwaambie tuseme hivi; hata hivi leo mkristo anayeacha wito wake na kuingilia wito wa mwenzake anakufa! Siku zake hapa duniani zinafupishwa! 5.
Kutokutii Maagizo ya Mungu
Kila kiungo katika mwili wa mwanadamu kina umuhimu wake. Na kila mkristo
aliyezaliwa mara ya pili ni kiungo katika mwili wa Kristo; kwa hiyo kila
mkristo ana kazi muhimu aliyopewa na Bwana aifanye. Kutokutii maagizo ya
Mungu juu ya kazi hiyo aliyopewa kunapunguza ziku zake za kuishi hapa
duniani.
Ndivyo ilivyokuwa katika maisha ya Musa na Haruni. Mpango wa
Mungu ulikuwa ni Musa na Haruni wawaongoze wana wa Israeli kutoka Misri
hadi Kaanani. Halikuwa kusudi la Mungu ya kuwa Musa na Haruni wafie
jangwani kabla ya kufika Kanani. Soma kitabu cha Kutoka sura ya 3 na ya
4.
Kwanini Musa na Haruni walikufa njiani kabla ya safari
kumalizika? “Bwana
akasema na Musa siku hiyo hiyo, akamwambia,
kwea katika mlima huu wa
Abarimu, mpaka kilima cha Nebo,
kilicho katika nchi ya Kanaani niwapayo
wana wa Israeli kuimiliki; UKAFE katika
kilima, huko ukweako, ukusanywe uwe
pamoja na jamaa zako; kama alivyo kufa nduguyo
Haruni katika mlima wa Hori, akakusanywa
awe pamoja na watu wake; kwa
sababu MLINIKOSA NINYI JUU YANGU
KATIKATI YA WANA WA ISRAELI KATIKA
MAJI YA MERIBA HUKO KADESHI,
katika bara ya Sini; kwa kuwa
HAMKUNITAKASA katikati ya wana wa Israeli”
(Kumbukumbu la Torati 32:48-52).
Ni wazi hapa ya kwamba Musa na Haruni hawakumalizia huduma waliyopewa,
wakafa njiani wote wawili kwa kuwa HAWAKUMTAKASA BWANA mble ya Wana wa
Israeli. Kwa maneno mengine HAWAKUTII MAAGIZO YA MUNGU BADALA YAKE
WALIASI MBELE YA WANA WA ISRAELI. Soma kitabu cha Hesabu 20:1-12.
Hawakumpa Mungu utukufu katikati ya Wana wa Israeli.
Watumishi wengi wa Mungu wamekufa kabla ya kumaliza huduma walizopewa
kwa sababu ya kutokutii maagizo ya Mungu waliyopewa. Mungu anapowagiza
jambo; wanashindwa kulitekeleza wala hawampi Utukufu wakiwa mbele za
watu. Na wengi wanadhani ya kwamba kwa kuwa miujiza inafanyika katika
huduma zao basi Bwana anawakubali. Lakini Yesu Kristo ana mawazo tofauti
juu ya jambo hili. Hebu na tumsikie anasemaje; “Ndipo
kwa matunda yao mtawatambua. Si
kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana,
atakayeingia katika ufalme wa mbinguni;
bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba
yangu aliye mbinguni. Wengi wataniambia
siku ile, Bwana, Bwana hatukufanya unabii
kwa jina lako na kwa
jina lako kutoa pepo, na
kwa jina lako kufanya miujiza mingi?
Ndipo nitawaambia dhahiri, sikuwajua ninyi
kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao
maovu” (Mathayo
7:20-23).
Kumbuka karama bila tunda la Roho haitoshi. Tawi lisilozaa
matunda hukatwa. Mshitaki
wetu Ibilisi
Biblia inamwita
Ibilisi ya kuwa ni mshitaki wetu. Yeye anatushitaki sisi tulio wa Kristo
usiku na mchana mbele za Mungu aliye Baba yetu. Je! unajua anatushitaki
kitu gani? Analotushitaki ni hili, ya kwamba watu wa Kristo wengi
hawaenendi kama Mungu anavyotaka; na anaona Mungu anapendelea kwa kuwa
hasimamii Neno lake sawasawa.
Ibilisi anauliza; kwa nini wakristo wasio waheshimu wazazi wao
wanaachwa wakae siku nyingi juu ya nchi? Na pia anauliza maswali mengi
yanayofanana na hayo. “Yule
joka akatupwa, yule mkubwa, nyoka
wa Zamani, aitwaye Ibilisi na
Shetani, audanganyaye ulimwengu wote;
akatupwa hata nchi, na malaika zake
wakatupwa pamoja naye. Nikasikia sauti
Kuu mbinguni, ikisema, sasa kumekuwa
wokovu, na nguvu, na ufalme wa Mungu
wetu, na mamlaka ya Kristo wake; kwa
maana ametupwa chini MSHITAKI wa
ndugu zetu, yeye awashitakiye mbele za
Mungu wetu, mchana ya usiku. Nao
wakamshinda kwa DAMU YA MWANA
KONDOO, na kwa NENO LA USHUHUDA
WAO; ambao hawakupenda maisha yao
hata kufa” (Ufunuo 12:9-11).
Je! unadhani Mungu anachukua hatua gani anaposikia mashtaka ya
namna hiyo juu ya watu wake wanaokwenda kinyume na Neno lake, na ambao
wakionywa hatawaki kutubu wala kutengeneza palipo bomoka? OLE
Ole! “Ole
wa nchi na bahari! Kwa maana yule Ibilisi
ameshuka kwenu
mwenye ghadhabu nyingi,
akijua yakuwa ana wakati mchache tu”
(Ufunuo 12:12b). “Ole
wake ashindanaye na Muumba wake!
Kigae kimoja katika vigae vya dunia! Je
udongo umwambie yeye aufinyangae;
Unafanya nini? au kazi yao, hana mikono?
(Isaya 45:9). “Ole
wake amwambiye baba yake, Wazaa nini?
au mwanamke una utungu wa nini? (Isaya
45:10). “Ole
wenu waandishi na Mafarisayo,
wanafiki! Kwa kuwa mnazunguka katika
bahari na nchi kavu ili kumfanya mtu mmoja kuwa mwongofu na
akiisha kufanyika, mnamfanya
kuwa mwana wa jehanam mara
mbili zaidi kuliko ninyi wenyewe”
(Mathayo 23:15). “Ole
wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki!
Kwa kuwa mnasafisha nje ya kikombe na chano,
na ndani yake vimejaa
unyang’anyi na kutokuwa na
kiasi. Ewe Farisayo kipofu, safisha kwanza
ndani ya kikombe, ili
nje yake nayo ipate kuwa safi”
(Mathayo 23:25,2b). “Ole
wenu, waandishi na Mafarisayo, wanafiki!
Kwa kuwa mmefanana na makaburi yaliyopakwa
chokaa, nayo kwa nje yanaonekana kuwa
mazuri, bali ndani yamejaa mifupa ya wafu, na
uchafu wote. Vivyo hivyo ninyi nanyi, kwa nje
mwaonekana na watu wenye haki, bali ndani
mmejaa unafiki na maasi” (Mathayo 23:26,27,28).
Ole wake asiyewaheshimu baba na mama yake kama yanenavyo maandiko, kwa
maana roho ya mauti iko juu yake! Ole kwake achukiaye kukemewa katika
Bwana ili aache njia zake mbaya, kwa maana roho ya mauti iko juu yake!
Ole kwake aingiliaye wito wa mwenzake na kutokutii maagizo ya Mungu; kwa
maana roho ya mauti iko juu yake! Ole kwake autumiaye ulimi wake vibaya;
kwa maana roho ya mauti iko juu yake! Tubu
Leo hii ukiisikia
sauti ya Roho wa Mungu, usiufanye moyo wako kuwa mgumu Ikiwa kuna sehemu
ya ujumbe huu inayokugusa, TUBU NA UTENGENEZE PALIPO BOMOKA kati yako na
Mungu, na kati yako na watu wengine. Hili ni muhimu kwa kuwa ,
“Tukiziungama dhambi zetu, Yeye ni mwaminifu na wa haki hata
atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote” (1Yohana
1:9). “Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo
ya kwanza. Lakini, usipofanya hivyo, naja kwako nami nitakiondoa kinara
chako katika mahali pake, usipotubu ……………… Yeye aliye na
sikio, na alisikie neno hili ambalo Roho ayaambia makanisa. Yeye
ashindaye nitampa kula matunda ya mti wa uzima, ulio katika bustani ya
Mungu” (Ufunuo 2:5,7). Kamilisha
huduma yako
Mtu wa Kristo hajawekwa hapa ulimwenguni ili ale na kushiba na kulala tu!
Mtu wa Kristo amewekwa ili afanye kazi kwa kuwa ametumwa na Kristo
ulimwenguni kama vile Kristo naye alivyotumwa na Baba ulimwenguni.
Hebu na tusome
maneno haya aliyoambiwa Timotheo maana yanatufaa hata sisi leo: “Nakuagiza
mbele za Mungu, na mbele za
Kristo Yesu, atakayewahukumu walio
hai na waliokufa; kwa kufunuliwa kwake
na kwa ufalme wake, lihubiri neno, uwe
tayari, wakati wake ukufaao na wakati
usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa
uvumilivu wote na mafundisho. Maana
utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho
yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia zao
wenyewe watajipatia waalimu makundi
makundi, kwa kuwa wana masikio ya utafiti;
na kuzigeukia hadithi za uongo. Bali wewe
uwe na kiasi katika mambo yote, vumilia
mabaya, fanya kazi ya mhubiri wa Injili
TIMILIZA HUDUMA YAKO” (2Timotheo 4:1 – 5) Tafadhali
soma pia Mathayo 24:42-51. Mwisho
Tunamshukuru Mungu kwa
kukuwezesha kuusoma ujumbe huu; tafadhali usiache kumshirikisha mwenzako.
Tafadhali usisahau kutuombea sisi, watoto wetu na timu nzima ili
tuifanye kazi ya Bwana aliyotupa katika uwezo wake na kama apendavyo
Yeye.
Ukiwa na jambo la kutushirikisha juu ya ujumbe huu tuandikie.
Neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, na upendo wa Mungu Baba, na Ushirika wa
‘Roho Mtakatifu ukae nasi sote, sasa na hata milele na milele. Amina. Ni
sisi watumishi wenzenu katika Shamba la Bwana. Christopher na Diana Mwakasege |
|