Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
BARUA ZA MWEZI


Barua ya Mwezi Desemba 2001

 “….NA JINA LAKE UTAMWITA YESU”

Mpendwa katika Kristo Yesu,

Tunakusalimu kwa Jina la Yesu Kristo Jina hili lipitalo kila jina! Tuna uhakika Mungu anazidi kukutunza na ndiyo maana hata umepata nguvu na nafasi ya kuisoma barua hii tunayokuandikia ya mwisho wa mwaka 2001.

Sisi tunamshukuru Mungu sana kwa jinsi ambavyo anazidi kututunza na kutusaidia katika maeneo yote ya maisha yetu. Huu ni mwezi wa Disemba na tangu tuanze Januari – huduma aliyotupa imeendelea vizuri sana. Tunashukuru sana kwa maombi yako kwa wale waliotuombea; na pia, tunashukuru kwa ajili ya michango ya fedha kwa wale waliotutumia ili kugharamia huduma. Mungu azidi kuwabariki kila siku sawa na Neno lake.

… na jina lake utamwita Yesu!

Katika kukumbuka kuzaliwa kwa Yesu Kristo hapa duniani kwa bikira Mariamu, ni jambo gani au ni kitu gani ambacho unakikumbuka zaidi? Kwetu sisi tuna vitu vingi tunavyokumbuka, lakini kimoja ambacho kinajitokeza zaidi ni hili Jina la Yesu!

Malaika Gabrieli alipokwenda kwa Mariamu ili kumjulisha juu ya kuchukua mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu-alimwambia ya kuwa,

“utachukuwa mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu”(Luka 1:31).Yusufu ambaye alikuwa amemposa Mariamu pia alipelekewa habari na malaika Gabrieli juu ya ujauzito wa Mariamu.Akaambiwa, “Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu…” (Mathayo 1:21).

Uamuzi wa ajabu!

Ukisoma Biblia vizuri na kuitafakari utagundua ya kuwa hili jina la Yesu ndilo jina la Mungu Baba ambalo pia amempa mtoto wake!Kwa nini tunasema hivi? Ni kwasababu katika kitabu cha Waebrania 11:4 tunasoma habari za Yesu ya kuwa, “amefanyika bora kupita malaika,kwa kadiri jina alilolirithi lilivyo tukufu kuliko lao”Kama jina la Yesu ni urithi au amerithi basi ina maana Yuko aliyemrithisha! Naye ni Mungu Baba!

Pia, Yesu mwenyewe anasema hivi katika Yohana 5:43 ya kuwa;

“Mimi nimekuja kwa jina la Baba yangu,wala ninyi hamnipokei; mwingine akija kwa jina lake mwenyewe, mtampokea huyo”

Kwa maneno mengine anatuambia ya kuwa hili jina la Yesu si lake “mwenyewe” bali la Baba yake ila amepewa ili aje nalo na kujulikana kwa hili hapa duniani!

Wafilipi 2:9 inatuambia ya kuwa jina hili la Yesu ni “Jina lile lipitalo kila jina”. Kwa hiyo ni rahisi kuwaza ya kuwa ikiwa jina la Yesu ni Jina lipitalo kila jina – basi Mungu Baba hana jina jingine ila hili jina la Yesu! Maana kama angekuwa na jina jingine – basi hilo ndilo lingekuwa kuu kuliko jina la Yesu. Lakini kwa kuwa biblia inatuambia jina la Yesu ni Jina lipitalo kila jina, ina maana Mungu Baba anatumia Jina hili hili!

Huu ni uamuzi wa ajabu sana toka kwa Mungu Baba aliye Mwenyezi! Kwa kulifunua Jina hili la Yesu, heshima ya pekee itokee kutoka kwa vitu vyote “vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi” (Wafilipi 2:10). Kila mara Jina hili linapotajwa katika Roho na kweli – vitu hivi vyote vinatega sikio na kuwa tayari kutii amri au agizo litakalofuata na kulitekeleza “kwa utukufu wa Mungu Baba” (Wafilipi 2:11).

Hakuna maisha ya kikristo bila Jina la Yesu!

Tunatamani sana upate nafasi ya kulitafakari sana Jina hili la Yesu ili uweze kupata siri nzito zilizo ndani yake. Siri mojawapo ni hii ya kwamba hakuna maisha ya kikristo bila Jina la Yesu! Labda tuseme hivi huwezi kutenganisha Jina la Yesu na ukristo na maisha yako ya kila siku! Ukristo bila Jina la Yesu si ukristo! Kwa nini tunasema hivi? Kwa sababu:

1. Ikiwa Umezaliwa mara ya pili au umeokoka basi ni kwa sababu pia unaliamini Jina la Yesu!

Imeandikwa hivi juu ya wote waliompokea Yesu mioyoni na maishani mwao ya kuwa:

“Bali wote waliompokea aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu” (Yohana 1:12,13).

2. Jina la Yesu linapaswa kuhusishwa na kila kitu unachofanya!

Imeandikwa hivi:

“Na kila mfanyalo, kwa neno au kwa tendo, fanyeni yote katika jina la Bwana Yesu, mkimshukuru Mungu Baba kwa yeye”. (Wakolosai 3:17)

Tena imeandikwa hivi:

“….na kumshukuru Mungu Baba sikuzote  kwa mambo yote, katika jina lake Bwana wetu Yesu Kristo” (Waefeso 5:20).

Tena imeandikwa hivi:

“Basi, kwa njia yake yeye, na tumpe Mungu dhabihu ya sifa daima, yaani, tunda la midomo iliungamayo jina lake” (Waebrania 13:14)

3. Kuna ishara zitakazofuata kila utakapotumia Jina la Yesu!

Yesu mwenyewe alisema hivi:

“Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo; watasema kwa lugha mpya; watashika nyoka; hata wakinywa kitu cha kufisha, hakitawadhuru kabisa;  wataweka mikono yao juu ya wagonjwa, nao watapata afya” (Marko 16:17,18)

Tenga muda wa kulitafakari Jina hili!

Kwa yule anayesoma Zaburi mara kwa mara hatakosa kuona ya kuwa Mfalme Daudi alitumia muda mwingi kulitafakari Jina la Bwana hata akaandika mengi juu ya jina la Bwana linavyohusika na maisha yake.

Tunataka tukutie moyo zaidi kwa barua hii ya kuwa mwezi huu wa Disemba unapokumbuka kuzaliwa kwa Yesu Kristo, kumbuka pia na kutafakari pia ujio wa Jina hili la Yesu na sehemu yake katika maisha yako.

Mwisho

Mungu wetu azidi kukutia nguvu na tunaamini utasimama pamoja nasi katika kuifanikisha kazi ya Mungu katika mwaka wa 2002. Watoto wetu na Timu nzima ya Huduma ya Mana inawasalimu.

Ni sisi katika utumishi wa Kristo,

Christopher na Diana Mwakasege

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.