Barua ya mwezi wa Julai, 2001
JE!
UMEANGALIA KAMA IMANI YAKO IKO MAHALI INAPOTAKIWA?
Mpendwa katika Kristo,
Tunakusalimu katika Jina la
Yesu Kristo. Tunashukuru kwamba umepata nafasi ya kuisoma barua hii na
kuutafakari ujumbe tulioongozwa na Roho Mtakatifu kukuandikia.
Tunajua ya kuwa kiu
uliyonayo ya kutaka kujua zaidi juu ya Yesu Kristo ndiyo imekusukuma
kusoma barua hii. Na tunaamini ya kuwa Roho Mtakatifu aliye pamoja nasi
tunapoandika ujumbe huu, yuko pamoja nawe unapousoma? Je! umeangalia
kama imani yako iko mahali inapotakiwa?
Tabia
ya imani
Kwa mtu yeyote
aliyefuatilia kwa karibu juu ya somo la imani, atakuwa amegundua ya kuwa
imani ina tabia yake. Kama unalijua hili basi ni vizuri sana na
upo mahali pazuri. Lakini ikiwa ulikuwa hujui basi ngoja tukupe mifano
michache.
- Imani inaweza kuongezeka.
Wanafunzi walimwambia Yesu awaongezee imani (Luka 17:5). Kama imani
inaweza kuongezeka, basi inaweza kupungua pia!
- Imani ina ngazi (levels)
mbali mbali. Biblia inasema juu ya “…toka imani hata imani” (Warumi
1:17)
- Imani inaweza kuwa kubwa.
Yesu alisema “sijaona imani kubwa….” (Luka 7:9). Kama
imani inaweza kuwa kubwa, basi inaweza kuwa ndogo pia!
- Imani inaweza kuonekana. Yesu
alisema, “Sijaona imani kubwa ….”. Pia
imeandikwa katika Marko 2:5 ya kuwa “…. Akiiona imani yao
…..” Ikiwa imani inaweza kuonekana, basi inaweza isionekane
pia!
- Imani inaweza kufa.
Imeandikwa, “….imani pasipo matendo imekufa”. (Yakobo 2:26).
Kama imani inaweza kufa basi inaweza kuishi pia!
- Imani inaweza kujaribiwa.
Imeandikwa, “….kujaribiwa kwa imani ……” (Yakobo 1:3).
Ikiwa imani inaweza kujaribiwa au kupewa mtihani, basi, inaweza kushinda
hilo jaribu au huo mtihani pia (1Yohana 5:4)!
- Imani haifanyi kazi peke yake!Utaona
ya kuwa imani inafanya kazi na matendo (Yakobo 2:20, 26), na
kwa upendo ( Galatia 5:6; 1Wakorintho 13:2), na kwa uvumilivu
(Waebrania 6:12) na kwa kinywa chako ( 1Timotheo 4:6; Marko
11:23)
Imani
inaweza kuwekwa pasipostahili!
Jambo hili tunaliona
tunaposoma habari za Yesu na wanafunzi wake katika Luka 8:22 –25.
Katika mstari wa 25 tunaona akiwauliza “Imani yenu iko wapi?” Ni
dhahiri kutoka katika swali hili ya kuwa imani walikuwa nayo lakini
waliiweka mahali pasipostahili!
Kutokana na tatizo la bahari
kuchafuka na upepo kuvuma kwa nguvu, wanafunzi walijikuta wanamwacha
Yesu akilala na wakaweka imani zao katika uzoefu wao wa kuvua
samaki baharini! Ndiyo maana hawakuona sababu ya kumpa Yesu usukani wa
boti ili awe kiongozi wao. Uzoefu wao uliwasukuma kuhamisha imani zao
toka kwa Yesu na kuweka katika nguvu na maarifa yao!
Kwa nini hawakumpa Yesu
uongozi wa boti lao? Na kwa nini tatizo la bahari lililopoanza
hawakumwamsha hadi juhudi za uzoefu wao ziliposhindwa? Jibu tunalipata
katika mstari wa 25! Hawakujua ya kuwa Yesu ana uwezo wa kutuliza upepo
na bahari! Imeandikwa hivi:
“Akawaambia,
Imani yenu iko wapi? Wakaogopa,
wakamaka, wakisema wao kwa
wao, ni nani huyu basi hata anaamuru upepo na maji, navyo vyamtii?”
Walikuwa wanajua Yesu anajua kuhubiri, kusamehe, kufundisha, kukemea
pepo na kuponya magonjwa. Pia, walimjua Yesu kama Kristo na kama Mwana
wa Mungu. Lakini hawakujua ya kuwa ana uwezo pia juu ya bahari na upepo
hata kuweza kuvituliza vinapoleta shida kwa wanafunzi wake!
Je!
Uko kama wanafunzi hawa?
Unamfahamu Yesu na uweza
wake kwa kiwango gani? Imani yako umeiweka wapi? Mazingira tunayoishi
yamekuwa chanzo kikubwa cha imani za wengi kuwekwa mahali pasipostahili.
Unapokabiliana na maisha ya
kila siku au unapokabiliana na matatizo yanayokutokea mara kwa mara, au
kama umo katikati ya majaribu au matatizo wakati huu, - imani yako
umeiweka wapi? Je, ni kwenye kisomo chako? Je, ni kwenye ujuzi na uzoefu
wako? Je, ni katika miaka mingi ndani ya wokovu? Je, ni kwa wanadamu
wenye uzoefu katika eneo unalohitaji msaada? Je, ni kwenye fedha zako?
Je, ni kwa watumishi wa Mungu unaowajua?
Je, ni kwa kanisa lako –
mahali unaposali? Je, ni kwenye maombi? Imani yako umeiweka wapi? Na
hapo ulipoiweka, imekufa au inaishi? – inaongezeka au unapungua?
Je! mahali ulipoiweka hiyo
imani yako imekuzalia kitu gani? Au imekuzalia matunda ya namna gani? Au
ulikuwa hujui ya kuwa imani inaweza kuzaa? Soma Yakobo 2:20. Na kama
imani yako imezaa, imezaa baraka au laana, ushindi au kushindwa, furaha
au huzuni, uvumilivu au kukata tamaa?
Ni
kipindi gani hiki?
Hiki ni kipindi ambacho Yesu
anatakiwa kuchukua nafasi anayostahili katika kila eneo la maisha yetu.
Kila eneo awe kiongozi! Usingoje hadi ukwame ndipo umtafute na kuumpa
uongozi wa eneo lililokwama!
Ni vizuri ujue ya kuwa Roho
Mtakatifu anapoamsha kanisa au anapovuma kwa upya kama wakati huu katika
nchi yetu – anatingisha imani yako akiikuta mahali pasipostahili! Nia
yake ni kwamba uhamishe imani yako mahali ilipo na kuiweka inapostahili
– yaani kwa Yesu Kristo! Ni kweli Yesu anaweza kutumia watu, au kisomo,
au watu, au fedha, au kitu chochote anachotaka kukusaidia au
kukufanikisha – lakini hataki uweke imani yako katika vitu hivyo! Weka
imani kwake, na utukufu umrudishie Yeye peke yake! Yesu hashirikiani
utukufu wake na kitu chochote au mtu yeyote!
Jambo
la kufanya!
- Ikiwa,
Imani yako haiko kwa Yesu katika eneo lo lote lile. Basi tubu na
mwombe akusaidie kutokuamini kwako!
- Amini
Neno la Mungu linavyosema juu ya Yesu Kristo na Roho wake Mtakatifu!
- Umpe
Mungu nafasi ya kufanya katika maisha yako kile ambacho Neno
limesema anaweza kufanya!
Kwa sasa tuishie hapa. Tunaamini umepata jambo la kukusaidia katika
ujumbe huu. Mara kwa mara angalia kama imani yako ipo mahali
inapostahili. Usingoje hadi umekwama ndipo ugundue ya kuwa Yesu unae
lakini umemwacha amelala na hana kazi ya kufanya kwa kuwa tu imani yako
inatafuta msaada mahali pengine na si kwa Yesu!
Sisi tunakupenda katika Kristo Yesu! Ni maombi yetu kwa Mungu ya kuwa
imani yako idumu katika Kristo wakati wote, mahali popote na katika hali
yo yote. Tuzidi kuombeana!
Ni
sisi katika utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege