Barua ya Mwezi Oktoba 2001
OMBA
MUNGU AFUNDISHE KINYWA CHAKO KUTUMIA MANENO VIZURI.
Mpendwa
katika Kristo,
Tunakusalimu ni katika lile
Jina lipitalo kila jina – Jina la Yesu Kristo, Mwana wa Mungu aliye
hai, ambaye pia ni Bwana na Mwokozi wetu.
Ni furaha yetu kukuandikia
tena barua hii tukiamini ya kuwa ulikuwa unaingojea kwa hamu, hasa kwako
wewe ambaye umekuwa ukisoma barua hizi kila mwezi. Pia, kwako wewe
ambaye ni mara yako ya kwanza kusoma barua yetu hii tunayoiandika kila
mwezi, tunasema Mungu wetu tunayemtumikia, na aliyetuongoza kuandika
tunachoandika akupe neema ya kuelewa maneno yaliyomo katika barua hii.
Je!
umewahi kuombea jambo hili?
Je! umewahi katika maombi
yako kwa Mungu kuomba kinywa chako kifundishwe kutumia maneno vizuri?
– au kutumia maneno ipasavyo? Si rahisi kuona umuhimu wa kuomba maombi
ya namna hii isipokuwa:
Kwanza:
Unajua umuhimu wa maneno katika maisha yako;
Pili:
Unajua ya kuwa bila msaada wa Mungu kinywa chako hakiwezi kusema
jinsi ikupasavyo kusema
Wengine wanajikuta wanaomba
maombi ya namna hii hasa wanapoona wanahitaji maneno yao
yakubalike na wale wanaosema nao! Hili ni sawa lakini tunalotaka uone
katika barua hii ni ule umuhimu wa kuongozwa na Mungu katika Roho
Mtakatifu kusema maneno ikupasavyo kusema, kila wakati na kila mahali.
Tunasoma katika kitabu cha
Kutoka 4:12 ya kuwa Mungu alimwambia Musa wakati akimtuma kwa Farao ya
kwamba “nami nitakuwa pamoja na kinywa chako, na kukufundisha utakalosema”.
Ndivyo ilivyokuwa pia wakati Yeremia alipokuwa anaitwa kumtumikia Mungu
na akajitetea ya kuwa yeye hawezi kusema kwa kuwa alikuwa mtoto bado.
Mungu akamwambia, “Usiseme, mimi ni mtoto; maana utakwenda kwa kila
mtu nitakayekutuma kwake,
nawe utasema neno nitakalo kuamuru”. Halafu Mungu akagusa kinywa cha
Yeremia na kumwambia; “ Tazama, nimetia maneno yangu kinywani mwako”
(Yeremia 1:6-9)
Ukifuatilia maisha ya Yesu alipokuwa hapa duniani alisema mara kwa mara
ya kuwa Baba yake ndiye aliyekuwa anampa maneno ya kusema na jinsi ya
kuyasema. Kwa mfano aliwahi kusema hivi:
“Kwa
sababu mimi sikunena kwa nafsi yangu tu; bali Baba aliyenipeleka, Yeye
mwenyewe ameniagiza nitakayonena na nitakayosema. Nami najua ya kuwa
agizo lake ni uzima wa milele; basi hayo ninenayo mimi, kama Baba
alivyoniambia, ndivyo ninenavyo” (Yohana
12:49,50)
Utaona
ya kuwa maneno kama haya Yesu pia aliyasema katika Yohana 8:26,38 na
Yohana 14:24. Kama ilikuwa muhimu kwa Yesu kuongozwa maneno ya kusema na
jinsi ya kuyasema na Mungu Baba yake na aliye Baba yetu pia, si zaidi
sana sisi ambao ni wafuasi na wanafunzi wake? Ndiyo maana Mtume Paulo
katika kitabu cha Waefeso 6:20 anawaomba watakatifu waliokuwa Efeso
wakati ule wamuombee kwa Mungu ili apate ujasiri wa kunena jinsi
impasavyo kunena!
Lazima
kuna umuhimu wake!
Yes!
Lazima kuna umuhimu wa kuongozwa na Mungu kusema maneno na jinsi
unavyoyasema. La sivyo asingewasaidia wakina Musa, Haruni, Yeremia, Yesu,
Paulo na wengine wengi ambao hatujawataja lakini biblia inasema
walisaidiwa na Mungu kusema maneno waliyosema na walivyoyasema.
Zipo
sababu nyingi zinazoonyesha umuhimu wa jambo hili, lakini katika barua
hii tutakuwekea sababu hizi chache zifuatazo:
Sababu
ya Kwanza: Maneno
yana uwezo wa kubeba na
kuwapa wanaokusikiliza kitu ulichonacho ndani yako. Kwa mfano: Neema
uliyonayo katika Kristo inawafikia wengine kwa njia ya maneno unayosema
(Waefeso 4:29-31). Kumbuka neema inaokoa na pia inafundisha na
kukuwezesha mahali ambapo hukustahili (Tito 2:11-13). Kama vile maneno
yanavyoweza kumchafua mtu machoni pa watu wengine, vile vile kuna maneno
yanayoweza kumsafisha au kumtakasa (Yohana 17:17). Kama vile ambavyo
kuna maneno ambayo yakisemwa yanamfanya ayasikiye ahuzunike, vile vile
kuna maneno yanayoweza kusemwa na kumpa mtu ayasikiaye furaha (Yohana
15:11). Pia kuna maneno ukisema yanabeba hekima ambayo hakuna asikiaye
atakayeweza kushindana nayo (Luka 21:14,15)
Sababu
ya Pili: Maneno
yasiyokuwa na maana yana uwezo wa kudanganya wanaoyasikia, kuharibu
tabia yao, na pia kuvuta hasira ya Mungu kwa wanaoyasema (Waefeso 5:6;
Wakolosai 2:8; 1Wakorintho 15:33). Ndiyo maana tunashauriwa na Zaburi
1:1 kutokuketi barazani pa wenye mizaha. Maneno yasiyokuwa na maana ni
maneno ambayo hayakutakiwa kusemwa na hayana faida katika Mungu kwa yule
anayeyasikia (Mithali 15:23)
Sababu
ya Tatu: Ulivyo na
ulivyonavyo sasa ni matokeo ya maneno ambayo umekuwa ukiyasema na
kuamini ya kuwa maneno hayo ni kweli au kuamini ya kuwa ndivyo yalivyo
(Marko 11:23; Mithali 18:20)
Sababu
ya Nne:
Utakavyokuwa na utakavyokuwa navyo kesho ni matokeo ya maneno
unayoyasema leo na kuamini ya kuwa maneno hayo ni kweli (Hesabu 14:1-38;
Hesabu 13:30-33; Mithali 12:14)
Sababu
ya Tano: Maneno
yako yanauwezo wa kukutega na kukukamata (Mithali 6:2)
Sababu
ya Sita: Unaposema
unapanda unachosema (Mithali 13:2; Mithali 6:14,19). Unakula au unavuna
matunda ya kile ulichopanda kwa midomo yako. Kumbuka maneno ni mbegu (Luka
8:11). Na apandacho mtu ndicho atakachovuna (Wagalatia 6:7). Ikifika
wakati wa kuvuna unavuna kingi kuliko ulichopanda! (Luka 6:38)
Sababu
ya Saba: Maneno
yanayotoka katika kinywa chako yanawapa wale wanaokusikiliza kujua hali
ya moyo wako na kujua kile kilichojaa ndani yake. Hii ni kwa sababu “mtu
mwema katika hazina ya moyo wake hutoa yaliyo mema, na mtu mwovu katika
hazina mbovu ya moyo wake hutoa yaliyo maovu; kwa kuwa mtu kinywa chake
hunena yale yaujazayo moyo wake” (Luka 6:45)
Sababu
ya Nane: Unachosema
kinaweza kuvuta nguvu ya Mungu kutekeleza ulichosema. Kwa mfano Wana wa
Israeli waliotoka Misri walishindwa kufika Kaanani isipokuwa Yoshua na
Kalabu kwa sababu ya maneno waliyoyasema. Maana walisema; “hatuwezi
kupanda tupigane na watu hawa; kwa maana wana nguvu kuliko sisi” (Hesabu
13:31). Na Mungu akawajibu ya kuwa; “hakika yangu kama ninyi
mlivyonena masikioni mwangu, ndivyo nitakavyowafanyia ninyi” (Hesabu
14:28). Yule mama mwenye ugonjwa wa kutokwa damu aliposema – nguvu za
Mungu zilivutwa kuja mwilini mwake kutekeleza alichosema (Marko
5:25-34). Na yule mjakazi wa Akida ndivyo alivyopona (Mathayo 8:5-13).
Akida alimwambia Yesu, “sema neno tu, na mtumishi wangu atapona”.
Yesu ‘alistaajabu’ kusikia imani kubwa ya namna hiyo, kwa hiyo
akamwambia, “nenda zako na iwe kwako kama ulivyoamini”. Na
mtumishi wa Akida akapona saa ile ile – kwa nini – kwa sababu nguvu
za Mungu zilivutwa na maneno ya Akida kutekeleza alichosema!
Sababu
ya Tisa: Unaposema
unaandika unayoyasema moyoni au nafsini mwako au mwake yule akusikie. Na
matokeo yake ni kusema na kutenda kile kilichoandikwa ndani yako. Au
yule aliyekusikiliza atajikuta anasema na
anatenda kile kilichoandikwa ndani yake kwa kutumia vinywa vya
watu (2 Wakorintho 3:2,3; Zaburi 45:1; Hesabu 30:1,2)
Sikiliza! Tunaweza kuendelea kukuorodheshea sababu moja baada ya
nyingine, lakini tunaamini kwa hizi chache tulizokuandikia katika
burua hii ni changamoto ya kutosha kukusukuma kuomba Mungu akupe maneno
ya kusema na kukuongoza jinsi ya kuyasema,kila wakati na kila mahali.
Tumeweka mistari mingi ya biblia katika barua hii tukiwa na lengo la
kukupa hazina ya kujisomea mwenyewe zaidi juu ya ujumbe tuliokuandikia.
Habari
za Huduma
Mwezi
uliopita wa Septemba tulikuwa na semina ya Neno la Mungu Shinyanga Mjini
ambayo ilihusisha madhehebu mbalimbali na watu kutoka Wilaya mbalimbali
za Shinyanga. Tuliona Mungu akiokoa, akiponya na kujaza Roho Mtakatifu
watu wake. Pia, tulipata nafasi ya kutangaza na kurusha mafundisho ya
semina hiyo kupitia Radio Faraja inayomilikiwa na Kanisa Katoliki. Na
hata baada ya kumaliza semina hiyo tumeingia mkataba na redio hiyo
kuendelea kurusha masomo tuliyofundisha sehemu mbalimbali. Kwa hiyo sasa
tuko hewani Mkoa wa Shinyanga kila Jumamosi na Jumapili kwa saa moja
kuanzia saa tatu hadi saa nne kila wiki. Asomaye na afahamu! Na
ukifahamu mshukuru Mungu pamoja nasi.
Mwezi
huu wa Oktoba tutakuwa na semina mbili – Kilombero tarehe 17 – 21
Oktoba na Mbeya Mjini tarehe 23 – 29 Oktoba. Tunahitaji maombi yako.
Na tarehe 9 – 11 Novemba tutakuwa Mererani.
Mungu azidi kukubariki kwa kukubali kusimama pamoja nasi katika huduma
hii ya kufundisha Neno la Mungu.
Ni
sisi katika Utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege