Barua ya Mwezi Aprili 2002
JE!
UNAJUA YA KUWA UNAPOTOA SADAKA
MUNGU HATAFUTI MALI YAKO BALI IMANI YAKO?
Mpendwa
katika Kristo,
Tunakusalimu
katika Jina la Yesu Kristo.
Tunamshukuru
Mungu sana kwa kutupa nafasi nyingine ya kuwasiliana na wewe kwa njia ya
waraka huu. Tena mwezi huu tumepewa neno ambalo tunaamini litakusogeza
karibu zaidi na Mungu kama vile lilivyotusogeza sisi. Roho Mtakatifu
ameweka swali hili ndani yetu kwa ajili yako linalosema hivi: “Je!
unajua ya kuwa unapotoa sadaka,-Mungu hatafuti mali yako bali imani yako?
Inawezekana
unajua au hujui au huna uhakika. Kwa vyo vyote vile na katika hali yo
yote ya uelewa uliyonayo, tufuatane pamoja katika kupitia na kutafakari
neno la Mungu kwa nia ya kupata jibu la swali hili.
Kwa
nini Mungu hatafuti mali yako?
Watu
wengi wanapotoa sadaka ndani yao huwa wana mawazo yanayodhani Mungu ni
maskini ambaye anahitaji mali za wanadamu ili zimsaidie katika kazi yake.
Kwa mantiki hii wanajenga mawazo yanayowafanya wao wawe ndio watoaji na
Mungu kuwa mpokeaji! Lakini biblia ina maneno yanayotuma usahihi zaidi
juu ya jambo hili. Imeandikwa hivi:
“Mungu
aliyeufanya ulimwengu na vitu vyote vilivyomo, yeye, kwa kuwa ni Bwana
wa mbingu na nchi, hakai katika hekalu zilizojengwa
kwa mikono; wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana kwamba
anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote
uzima na pumzi na vitu vyote”(Matendo
ya Mitume 17:24,25).
Angalia
tena maneno haya: “….wala hatumikiwi kwa mikono ya wanadamu kana
kwamba anahitaji kitu cho chote; kwa maana ndiye anayewapa wote uzima na
pumzi na vitu vyote”. Kama Mungu ndiye anayewapa wanadamu wote uzima
na pumzi na vitu vyote, hii inaonyesha ya kuwa Yeye ndiye chanzo cha
kila kitu tulichonacho.
Wazo
hili tunaliona tena likijitokeza katika Zaburi 24:1 ilipoandikwa ya kuwa:
“Nchi
na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, dunia na wote wakaao ndani yake”.
Ikiwa
kila kitu kinatoka kwa Mungu ina maana basi Mungu anapowataka wanadamu
wamtolee sadaka ana kitu cha zaidi anachotafuta kutoka kwao! Na si mali
zao! Baada ya kulitakari jambo hili kwa muda mrefu sasa tunaona yakuwa
sadaka imewekwa na Mungu ili kusaidia kuimarisha uhusiano wake na
wanadamu. Kwa msingi huu tunaweza kusema ya kuwa Mungu hatafuti wala
kufuata mali zetu anapotutaka tutoe sadaka bali imani tuliyonayo kwake.
Hebu tuangalia mifano michache:
Mfano
wa 1: Habili na Kaini
Je!
unaelewa ni kwa nini Mungu alikubali sadaka ya Kaini lakini akaikataa
sadaka ya Habili nduguye? Katika habari za hawa ndugu wawili tunasoma ya
kuwa:
“Habili
alikuwa mchunga kondoo, na Kaini alikuwa mkulima ardhi. Ikawa hatimaye
Kaini akaleta mazao ya ardhi sadaka kwa Bwana. Habili naye akaleta wazao
wa kwanza wa wanyama wake na sehemu zilizonona za wanyama. Bwana
akamtakabali Habili na sadaka yake; bali Kaini hakumtakabali, wala
sadaka yake. Kaini akaghadhibika sana, uso wake ukakunjamana” (Mwanzo
4:2-5).
Kama
tunavyoona Kaini alikasirika sana kwa sadaka yake kutokubalika na Mungu.
Mungu akashangaa kwa nini Kaini amekasirika na akamuuliza: “Kama
ukitenda vyema, hutapata kibali….” Kwa tafsiri nyingine
anamwambia ya kwamba “hakutenda vyema”. Kama angekuwa
ametenda vyema sadaka yake ingekubalika, lakini kwa sababu hakutenda
vyema sadaka yake ilikataliwa!
Ni
jambo gani la zaidi ambalo Habili alilifanya hata sadaka yake
ikakubalika na Mungu? Ni jambo gani lililopungua katika utoaji sadaka wa
Kaini hata kusababisha sadaka yake isikubalike? Maana wote walitoa kwa
kadri walivyokuwa navyo. Kwa kuwa imeandikwa hivi: “….kama nia
ipo, hukubaliwa kwa kadri ya alivyonavyo mtu, si kwa kadri ya asivyo
navyo” (2Wakorintho 8:12). Kama nia ya kumtolea Mungu sadaka wote
(Habili na Kaini) walikuwa nayo, na kila mtu alitoa kwa kadri alivyokuwa
navyo, ni kitu gani kilisababisha sadaka ya mmoja wao ikubalike na ya
mwingine ikataliwe?
Katika
kitabu cha Waebrania 11:4 inatupa jibu la swali hili inaposema; “Kwa
imani Habili alimtolea Mungu dhabihu iliyo bora kuliko Kaini; kwa hiyo
alishuhudiwa kuwa ana haki; Mungu akazishuhudia sadaka zake, na kwa hiyo,
ijapokuwa amekufa, angali akinena”. Siri iko hapa! Sadaka ya Kaini
haikuwa mbaya, inawezekana ilikuwa ni nzuri, maana imeandikwa ya kuwa
Habili alitoa “iliyo bora”. ‘Bora’ ni sifa ya ngazi ya juu zaidi
ya ‘nzuri’. Kwa hiyo inawezekana sadaka ya Kaini ilikuwa ‘nzuri’,
lakini ya Habili ilikuwa ‘bora’ na ikakubalika na Mungu kwa kuwa
aliitoa kwa imani!
Kwa
hiyo tunaweza kusema katika utoaji wa hawa ndugu wawili Mungu alikuwa
anatafuta kwanza imani zao kabla ya vitu walivyomtolea!
Jifunze katika hili unapotoa sadaka, Mungu anatafuta kwanza imani
yako kabla ya kupokea sadaka yako. Ukikosea kwenye eneo la imani, sadaka
yako haikubaliki mbele za Mungu hata kama ni nzuri au kubwa kwa kiasi
gani. Fikiria mwenyewe ikiwa umewahi kutoa sadaka yoyote ‘kubwa’ na
‘nzuri’ katika maisha yako, - ikiwa hukuitoa kwa imani hakupokelewa
na Mungu, na hii inaweza ikawa ni sababu mojawapo ilioyofanya
‘kutokuvuna’ toka kwenye sadaka hiyo.
Mfano
wa 2: Mjane na Matajiri
Tunasoma
katika kitabu cha Marko 12:41,42 ya kuwa: “Naye (Yesu) akaketi
kulielekea sanduku la Hazina, akatazama jinsi mkutano watiavyo mapesa
katika sanduku. Matajiri wengi wakatia mengi. Akaja mwanamke mmoja,
mjane, maskini, akatia senti mbili, kiasi cha nusu pesa”. Unadhani
Yesu alikuwa anatafuta nini katika kuangalia sadaka zilivyokuwa
zinatolewa? Unadhani ni uwingi na udogo wa sadaka za watoaji? La hasha!
Bali alikuwa anataka kujua imani zao wameziweka wapi wanapotoa
sadaka, kwa kuwa imani ndiyo inayoweka na kuamua thamani ya
sadaka uliyotoa itakavyokuwa mbele za Mungu.
Tunapoendelea
kuisoma habari hii katika Marko 12:43,44 tunaona Yesu akiwaita wanafunzi
wake; “….akawaambia, huyu mjane maskini ametia zaidi kuliko wote
wanaotia katika sanduku la hazina; maana hao wote walitia baadhi ya mali
iliyowazidi; bali huyu katika umaskini wake ametia vyote alivyokuwa
navyo, ndivyo riziki yake yote pia”. Kwa tafsiri nyingine alikuwa
anasema huyu mjane ametoa sadaka yake akiwa ameweka imani yake kwa Mungu
na kwa hiyo thamani ya sadaka yake mbele za Mungu ikahesabika kuwa kubwa
kuliko ya sadaka za wengine.
Yesu
alijuaje hili? Je! na sisi tunaweza kujua? Ndiyo! Kwa sababu Roho
Mtakatifu aliyemfunulia Yesu juu ya hili yuko pamoja nasi kutufunulia
ili tujifunze kumtolea Mungu sadaka zinazompendeza.
Yesu alisema;
“Huyu mjane ametia zaidi kuliko wote wanaotia katika sanduku la hazina…..”
na “….. katika umaskini
wake ametia vyote alivyokuwa navyo, ndiyo riziki yake yote pia.”
Tukianza kutafuta imani ya mjane huyu alipoiweka tutagundua ya kuwa,
hakuiweka katika sadaka aliyotoa. Maana ameitoa, tena yote na haimo
mikononi mwake. Tunaposema imani tunamaana ya uhakika wa kuendelea
‘kula na kunywa’ baada ya kutoa sadaka yako. Tunaona pia ya kuwa
imani hii huyu mama mjane hakuiweka katika fedha iliyobaki baada ya
kutoa sadaka – kwa kuwa hakuwa amebaki na kitu. Kwa hiyo imani ya
kuendelea ‘kula na kunywa’ baada ya kutoa sadaka aliiweka kwa Mungu
– ndiye aliyemtegemea kumtunza baada ya kutoa sadaka. Kwa lugha
nyingine alimweka Mungu ‘kwanza’ katika kumtemgemea badala ya
kutegemea nguzu zake mwenyewe.
Kwa
wale matajiri, Yesu alisema; “….hao wote walitia baadhi ya mali
iliyowazidi…? Tukitafuta imani ya matajiri hawa tunaona ya kuwa
imewekwa katika ‘fedha zilizobaki’ baada ya kutoa sadaka!
Hawa walitoa katika sadaka baadhi ya fedha iliyowazidi. Kumbuka
‘sadaka’ inakuwa ‘sadaka’ inayokubalika inapotokea ya kwamba
mahali ulipoitoa pameacha pengo ambalo unatarajia Mungu mwenyewe alizibe!
Hawa matajiri hawakuwa wametoa sadaka ya namna hii – walitoa baadhi ya
mali iliyowazidi, kwa hiyo hakukuwa na sababu ya kumtegemea Mungu
– maana hawakuwa na pengo lolote! Baada ya kutoa sadaka, imani ya
‘kula na kunywa’ waliiweka kwenye mali iliyobaki na siyo kwa Mungu
wala kwenye baadhi ya mali iliyowazidi waliyoitoa.
Sasa
tukuulize swali, je, unapotoa sadaka imani ya ‘kula na kunywa’ baada
ya kuitoa hiyo sadaka huwa unaiweka wapi? Wengi huwa wanaiweka katika
mali iliyobaki baada ya kutoa sadaka; ndiyo wanayoitegemea katika
kuwalisha! Wengine wameweka katika ‘sadaka’
waliyoitoa, na kutegemea ijizalishe, lakini wamesahau ya kuwa
hakuna mbegu au sadaka inayojikuza kwa sababu “mwenye kukuza ni Mungu”
(1Wakorintho 3: 6,7). Sadaka ya namna hii isipozaa na kumletea matunda
anakata tamaa na kuona utoaji haumsaidii kitu chochote. Lakini kosa lake
ni mahali imani yake alipoiweka! Unapotoa sadaka, imani yako ya
kuendelea kula na kunywa au kutunzwa baada ya kuitoa hiyo sadaka iweke
kwa Mungu na siyo kwenye sadaka uliyoitoa au kwenye mali/fedha
zilizobaki baada ya kutoa sadaka.
Kabla
ya kukueleza namna utakavyoweza kuipata imani ya namna hii tunataka
tukupe mfano mwingine mmoja.
Mfano
wa 3: Mtu Tajiri na Mali yake
Katika
kitabu cha Marko 10:17-30 tunasoma tena mfano mwingine unaotuonyesha ya
kuwa katika kutoa sadaka Mungu anatafuta kwanza imani ya mtu
aliyonayo kwake na si mali yake. Tunapoisoma habari hii tunaona ya kuwa
mtu mmoja tajiri alikwenda kumuuliza Yesu namna atakavyoweza kuurithi
uzima wa milele. Yesu akamwambia ikiwa amezishika amri za Mungu. Yule
tajiri akasema “yote nimeyashika tangu utoto wangu”
Yesu
akamwambia “umepungukiwa na neno moja”. Yesu alikuwa ana maana gani?
Yesu alikuwa anataka yule tajiri ajue ya kuwa katika ‘kushika amri’
Mungu alikuwa anatafuta ‘imani yake’ – lakini neno moja limepungua
linalosababisha imani hiyo isionekane. Yesu akamwaambia; “Enenda,
ukauze ulivyo navyo vyote, uwape maskini, nawe utakuwa na hazina
mbinguni; kisha njoo unifuate”. Yule tajiri hakufurahi na akaondoka
kwa huzuni.
Kwa
nini Yesu alimwambia auze vyote na si vichache au vile vilivyomzidi?
Kwa sababu moyo wake ulikuwa unategemea mali yake na siyo kumtegemea
Mungu. Ndiyo maana alipoondoka Yesu alisema; “…..jinsi ilivyoshida wenye
kutegemea mali (au walioweka imani zao katika mali) kuingia katika
ufalme wa Mungu!” (Marko 10:24) “ Kwa kuwa hazina yako ilipo, ndipo
utakapokuwapo na moyo wako” (Mathayo 6:21)
Yesu
alikuwa hatafuti mali au utajiri wa huyo mtu. Wala hakuwa anataka
kumfilisi! Yesu alitaka kumsaidia ili aweke imani kwa Mungu na si kwenye
mali zake. Lakini kwa sababu moyo wake uliambatana sana na mali zake
kuliko kuambatana na Mungu alishindwa kutii agizo la Yesu.
Hata
wanafunzi wake walishindwa kumwelewa haraka katika hili kiasi kwamba
Petro akauliza wao watapata nini, kwa sababu wameacha vyote na kumfuata.
Yesu akasema; cho chote kile ambacho mtu atatoa kwa ajili yake na kwa
ajili ya injili “atapewa mara mia sasa wakati huu…. na katika
ulimwengu ujao uzima wa milele” (Marko 10:30).
Kwa hiyo
ukitoa sadaka na imani yako
ikawa kwa Mungu juu ya tegemeo lako baada ya kutoa sadaka, kile
ulichotoa Mungu atakurudishia ‘mara mia’ wakati huu.
Imani
hii unaipataje?
Imani
ya namna hii unaipata kwa kutii agizo au ahadi ya Mungu inayoambatana na
utoaji huo ambao Mungu anataka utoe. Kwa sababu; “Imani, chanzo chake
ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo” (Warumi 10:17)
Kwa
hiyo lazima usikie neno la Kristo au ahadi ya Kristo inayohusiana na huo
utoaji. Hii inakusaidia kuweka tegemeo lako kwa Mungu aliyekupa ahadi
juu ya jinsi utakavyoishi baada ya kutoa sadaka hiyo. Imani ikiisha
ingia ndani yako huwa ina tabia ya kutaka au kudai utekeleze agizo
lililomo katika ahadi iliyoleta hiyo imani ndani yako. Hebu
tuangalie mifano hii:
Ibrahim
na Isaka
Hivi ndivyo
ilivyokuwa kwa Ibrahimu alipoambiwa amtoe Isaka kuwa sadaka ya
kuteketezwa. Mungu alikuwa hatafuti kumuua Isaka au haja yake katika
sadaka ya Isaka haikuwa ni Isaka bali alikuwa anatafuta imani ya
Ibrahimu. Katika mazungumzo ya Mungu na Ibrahimu iliwekwa wazi ya kuwa
imani ya Ibrahimu ya kuwa “ baba wa mataifa mengi” ilitakiwa iwe kwa
Mungu na siyo mahali po pote.
Hii imani ya Ibrahimu isingeweza kuwa katika uwezo wao kwa sababu
umri wao ulikuwa mkubwa kwa hiyo wasingeweza kuzaa mtoto ki-kawaida (Warumi
4:17-19). Ilimbidi Ibrahimu aweke imani hiyo kwenye ahadi ya Mungu kwa
sababu ndicho chanzo cha imani aliyotakiwa kuwa nayo. Ndiyo maana
imeandikwa hivi juu ya Ibrahimu; “Lakini akiiona ahadi ya Mungu
hakusita kwa kutoamini, bali alitiwa nguvu kwa imani, akimtukuza Mungu;
huku akijua hakika ya kuwa Mungu aweza kufanya yale aliyoahidi” (Warumi
10:20,21). Mungu anataka imani zetu zisiwe katika uwezo tulionao wa
kuzalisha tunachotaka kizaliwe, bali ziwe katika ahadi za Mungu juu ya
maisha yetu ya kila siku na ya baadaye.
Imani
ya Ibrahimu ya kuwa “baba wa Mataifa mengi” haikutakiwa iwe kwa
Ishmaeli aliyemzaa na msichana wao wa kazi – Hajiri – bali iwe
katika ahadi ya Mungu. Kwa hiyo Mungu alimwambia Ibrahimu akubaliane na
wazo la mke wake la kuwafukuza Hajiri na mtoto Ishmaeli watoke katika
nyumba yao ili wawe mbali nao (Mwanzo 21:8-21). Mungu anataka imani zetu
zisiwe katika uwezo wa wengine kutuzalia au kutuzalishia kile tunachoona
kitatusaidia kupata baraka alizotuahidi, bali imani zetu ziwe katika
ahadi za Mungu alizosema nasi juu ya maisha ya kila siku na ya baadaye.
Imani ya
Ibrahimu ya kuwa “baba wa mataifa mengi” haikutakiwa iwe kwa Isaka
hata kama ni njia ambayo Mungu anataka kuitumia kumbariki –
bali imani iwe katika ahadi ya Mungu. Kwa hiyo Mungu alimwambia Ibrahimu
amtoe Isaka awe sadaka ya kuteketezwa. Na Ibrahimu alipokubali kumtoa
Isaka sadaka alikuwa anaonyesha imani yake kwa Mungu ya kuwa hajaiweka
katika Isaka( ambaye ni njia tu ya kupatia
baraka Mungu akitaka
kuitumia), lakini ameiweka katika Mungu
na ahadi yake.
Ndiyo maana imeandikwa hivi: “Kwa imani Ibrahimu alipojaribiwa ,akamtoa
Isaka awe dhabihu; na yeye aliyezipokea ahadi alikuwa akimtoa
mwanawe, mzaliwa pekee;naam , yeye aliyeambiwa,katika Isaka uzao wako
utaitwa,akihesabu ya kuwa Mungu aweza kumfufua hata kutoka kuzimu ;akampata
tena toka huko kwa mfano”(Waebrania 11:17-19)
Mungu
alitaka aweke imani yake kwake ili Mungu ndiye aamue ni kwa namna
gani atalitimiza neno alilo
muahidi Ibrahimu. Ndiyo maana Ibrahimu
alipokuwa tayari kumchinja
Isaka kama sadaka- alimwambia asimchinje! Kwa nini? Kwa sababu
Mungu alikuwa hamtafuti Isaka ili amuue bali Imani ya
Ibrahimu ili Isaka aendelee kukaa na Ibrahimu bila kuyumbisha imani ya
Ibrahimu!
Ndiyo
maana Mungu akasema ; “sasa ninajua ya kuwa
unamcha Mungu , iwapo hukunizuilia mwanao , mwanao wa pekee”(Mwanzo22:12).
Mungu akamrudishia Ibrahimu
Isaka wake, na badala yake
akampa kondoo mume amtoe
sadaka badala ya Isaka. Kwa
lugha nyingine Mungu alitaka Ibrahimu ajue ya kwamba kuwa baba wa
mataifa mengi haitatimizwa
kwa kupitia kwa Isaka bali
kwa Mungu ambaye ameandaa “kondoo mume” au Yesu Kristo awe chanzo
cha kubariki mataifa mengi yawe uzao wa Ibrahimu(Wagalatia 3:13,14)
Mungu
anataka imani zetu zisiwe katika njia alizotupa kutubariki au alizotupa
ili tumtumikie bali imani zetu ziwe katika ahadi anazotupa kwa ajili ya
maisha ya kila siku na ya baadaye. Mungu anataka njia alizotupa
au mali alizotupa ziwe kama
‘hazipo’ au ‘zimekufa’mbele yetu ili imani zetu zibaki
kwa Mungu ambaye “ndani yake yeye tunaishi;
tunakwenda , na kuwa na uhai wetu”(Matendo ya Mitume 17:28).
Tukiviweka vitu hivyo au njia hizo katika ‘madhabahu’ na kuzitoa
sadaka ili tusizitegemee – Mungu ataturudishia ili tuendelee kukaa
navyo lakini pia atatupa na kondoo mume.
Nabii
Eliya na Mjane wa Serapta
Mungu
alipokuwa akimtuma nabii
Eliya ili akalishwe na kutunzwa na mama wa Serapta
alikuwa anatafuta imani za wote wawili (Eliya na yule mjane)
zikae katika ahadi zake na siyo katika mali walizonazo.
Mungu
alitaka nabii Eliya asiweke imani yake kwenye kile chakula cha yule
mjane bali kwa Mungu na ahadi yake aliyosema;”Ondoka, uende Serepta,
ulio mji wa Sidoni, ukae huko.Tazama, nimemwagiza mwanamke mjane wa huko
akulishe” (1Wafalme17:9). Eliya asingeweza kuweka imani ya ‘kula na
kunywa’ kwa kunguru na kwenye kijito cha Kerethi
kwa sababu kunguru alikuwa ameacha kuleta chakula
na kijito kimekauka.Tena Eliya
asingeweza kuweka kuweka imani yake
ya “kula na kunywa’ kwenye vyakula vya mama mjane wa Serapta
, kwa sababu vilikuwa vichache sana. Kwa hiyo ilibidi aweke imani yake
ya ‘kula na kunywa’ kwenye ahadi ya Mungu (1Wafalme17: 10-16)
Pia
kwa mama mjane wa Serapta, Mungu alitaka aweke imani yake kwa Mungu na
katika ahadi yake,na siyo kwenye vyakula alivyokuwa navyo. Ndiyo maana
mara ya kwanza alisita kumtengenezea chakula kama alivyoamriwa kwa
sababu alikuwa anaogopa kitatokea nini kwake na mtoto wake baada ya
kutoa hiyo sadaka kwa Eliya. Hapa ndipo watu wengi wanakwama.Huwa
wanashindwa kumtolea Mungu hasa wanapokuta ya kuwa
walichonacho au wanachotakiwa kukitoa ndicho kilichobaki na
wakikitoa hawatabakiwa na kitu. Lakini ikiwa utaiondoa imani yako kwenye
mali ulizonazo, au mradi ulionao , au fedha ulizonazo,au huduma
uliyonayo, au njia uliyonayo, au kazi uliyonayo-ndipo utakapoiweka kwa
Mungu na ahadi yake
aliyokupa katika kutoa huko utakakotoa. Na ndipo Mungu atakapokutimizia
ahadi aliyokuahidia.
Mwisho
Tumekuandikia
barua ndefu mwezi huu na
tunaamini Mungu amekupa nguvu na nafasi ya kuisoma na utaendelea
kuyatafakari yaliyomo na kuyafanyia
kazi
Tuzidi
kuombeana. Usiache kusoma masomo tunayoyatoa kila wiki kwa sasa yenye
kichwa cha “JIHADHARI
NA MAFUNUO”.
ni
sisi katika utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege