|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Je!
Unajua ya kuwa Roho Mtakatifu ni Msaidizi aliyetumwa na Mungu kutusaidia?
Mpendwa katika Kristo,
Salamu katika Jina la Yesu Kristo!
Tunajua inawezekana kabisa ya kuwa unamjua Roho Mtakatifu au kama humjui
basi umewahi kusikia habari zake au pia inawezekana umewahi kusoma
habari zake katika vitabu mbalimbali.
Tunaona ya kuwa katika kitabu cha Yohana Mtakatifu, Yesu Kristo
alimtambulisha Roho Mtakatifu kama ‘Msaidizi’ mara nne! Soma
mistari ifuatayo:
Yohana 14:16,17 inasema hivi: "Nami
nitamwomba Baba, naye atawapa MSAIDIZI mwingine,
ili akae nanyi hata milele; ndiye Roho wa kweli; ambaye ulimwengu
hauwezi kumpokea, kwa kuwa haumwoni wala haumtambui; bali ninyi
mnamtambua, maana anakaa kwenu, naye atakuwa ndani yenu."
Yohana 14:26 inasema hivi: "Lakini
huyo MSAIDIZI, huyo Roho Mtakatifu, ambaye Baba atampeleka kwa
jina langu, atawafundisha yote, na kuwakumbusha yote niliyowaambia"
Yohana 15:26 inasema hivi: "Lakini
ajapo huyo MSAIDIZI, nitakayewapelekea kutoka kwa Baba, huyo Roho wa
kweli atokaye kwa Baba, yeye atanishuhudia."
Yohana 16:7 inasema hivi: "Lakini
mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke; kwa maana mimi
nisipoondoka, huyo MSAIDIZI hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu,
nitampeleka kwenu." Kwa
nini MSAIDIZI alitumwa?
Msaidizi siku zote anatumwa kwa sababu msaada wake ni muhimu kwa yule
anayehitaji msaada. Ukisoma maandiko mbalimbali katika biblia utoana ya
kuwa Yesu Kristo alipopaa na kuketi mkono wa kuume wa Mungu alimwambia
Baba yake ya kuwa sisi tuliomo ulimwenguni tunahitaji msaada ili tuweze kuona,
kuingia, kufanya na kudumu katika mapenzi ya Mungu.
Kwa hiyo Roho Mtakatifu ambaye ni Msaidizi alitumwa kwetu ili kutusaidia.
Msaidizi anapotumwa huwa anabeba msaada ambao anajua utamsaidia yule
anayehitaji msaada. Si watu wengi wanaojua ya kuwa msaada wanaohitaji
ili kutatua matatizo waliyonayo umo ndani ya Roho Mtakatifu. Na si wengi
pia wanaojua ya kuwa Roho Mtakatifu anatumia UPAKO kama njia
mojawapo ya kutusaidia au ya kutupa msaada tunaouhitaji.
Neno "Upako" kama linavyotumika sasa katikati ya watu wa Mungu
linatokana na maneno katika biblia yanayosema "kutiwa mafuta"
(Luka 4:18). Lakini pia neno hili "Upako" limetafsiriwa katika
sehemu zingine katika biblia kama ‘nguvu ya Mungu’ (Matendo 1:8), au
‘uweza wa Bwana’ (Luka 5:17), au ‘mkono wa Mungu’ (1Petro 5:6)
au ‘kidole cha Mungu’ (Luka 11:20), nakadhalika. Je!
unajua ya kuwa:
Imani
huja kwa kusikia….
Warumi 10:17 inasema; "Basi, imani chanzo chake ni kusikia; na
kusikia huja kwa neno la Kristo".Mtu anayetaka kusaidiwa mara
nyingi kitu kinachomfanya atafute msaada ni KUJUA kitakachotokea baada
ya kuupata huo msaada katika eneo analotaka kusaidiwa. Ndiyo
maana mtu mgonjwa anayetaka kupona ugonjwa unaomsumbua atatafuta
uponyaji kila mahali anaposikia unaweza kupatikana.
Upako ni msaada uliotumwa kwetu na Mungu katika jina la Yesu Kristo kwa
njia ya Roho Mtakatifu. Watu wengi hawautafuti upako wala Roho Mtakatifu
ambaye ndani yake kuna upako kwa sababu hawajasikia habari zake wala
faida zake! Ikiwa wewe umesikia habari zake na unajua faida zake mbona
basi huonyeshi kiu ya kutosha ya kuonyesha ya kuwa unahitaji? Au kuna
njia nyingine unayotumia kupata masaada unaouhitaji katika maisha yako?
Maana kama unahitaji msaada toka kwa Mungu, ni muhimu ujue ya kuwa Roho
Mtakatifu ni Msaidizi aliyetumwa na Mungu ulimwengu akiwa amebeba msaada
wa kutusaidia tunaouhitaji. Tafakari
mifano hii!
Kwa nini nabii Elisha aliomba roho (upako) maradufu iliyokuwa juu ya
nabii Eliya imshukie? Soma habari hii vizuri katika kitabu cha 2 Wafalme
2:1-15.
Ni kwa sababu alijua ya kuwa Eliya anaondolewa kwake na ya kuwa hatakuwa
pamoja naye wakati anavuka mto Yordani mara ya pili. Na kwa kuwa alijua
siri iliyomsaidia Eliya kuvuka mto Yordani kwamba haikuwa nguo yake bali
roho iliyokuwa juu yake; na kwa kuwa alijua atakuwa peke yake bila
Eliya atakapovuka mto Yordani tena, akaomba apate roho hiyo maradufu au
upako huo maradufu.
Sikiliza! Kama kuna mtu aliyekusaidia kuvuka mara ya kwanza katika
tatizo ulilonalo, tafuta kuijua siri iliyomfanya kukusaidia ukavuka, ili
hata kama hayupo uweze kuvuka mwenyewe kwa kuitumia wewe siri hiyo
aliyoitumia yeye kwanza.
Wayahudi wangapi waliovuka bahari ya Shamu wakiongozwa na Musa waliijua
siri ya upako (au mkono wa Mungu) uliokuwa juu ya fimbo ya Musa? Soma
kitabu cha Kutoka 4:1-5; Kutoka 14:15-18). Hata kama wangetaka kurudi
Misri peke yao bila Musa baada ya kuvuka bahari ya Shamu mara ya
kwanza wangekwama kwa sababu hawakujua siri iliyomfanya Musa
akawavusha mahali pakavu mara ya kwanza.
Wale waliokuwa karibu na Musa walipokuwa wanavuka bahari ya Shamu,
ilikuwa rahisi kuona ya kuwa ni ‘fimbo’ iliyofanya wakavuka. Kwa
hiyo kila mtu angeanza kuiga kutembea na fimbo kama Musa na kuishika na
kuitumia kama Musa alivyofanya! Tofauti yake ingekuwa fimbo ya Musa siku
zote ingekuwa na matokeo tofauti, yaliyo bora, na yenye mafanikio zaidi
kuliko ya fimbo zao!
Kwa hiyo tunakuambia na kukushauri hivi; Don’t just follow METHODS
but follow the ANNOINTING behind the success of various methods!
Mafanikio hayamo kwenye mbinu au njia unayotumia bali yamo katika
upako unaowezesha mbinu au njia fulani ifanikiwe!
Kumbuka siyo "kupiga maji kwa fimbo" bali upako wa Roho
Mtakatifu uliofanya njia hii ya kupiga maji kwa fimbo ifanikiwe kupasua
bahari ya Shamu. Tena, siyo "kupiga maji kwa nguo ya Eliya"
bali upako wa Roho Mtakatifu uliofanya njia hii ya kupiga maji kwa nguo
ya Eliya ikafanikiwa! Mwisho!
Ni maombi yetu ya kuwa katika barua hii Mungu ameamsha nia na kiu zaidi
ndani yako ya kumjua zaidi Roho Mtakatifu na upako wake. Mungu na
akuhekimishe na kukufunulia zaidi juu ya Msaidizi huyu wa ajabu!
Tuzidi kuombeana! ni
sisi katika utumishi wa Kristo, Christopher
na Diana Mwakasege |
|