Barua ya Mwezi Januari 2002
JE!
UMEPATA NENO LA KUKUONGOZA MWAKA 2002
Mpendwa
katika Kristo Yesu;
Salamu za upendo tunakuletea katika Jina la Yesu Kristo, Mwana wa Mungu
na Mwokozi wetu.
Tunaamini umemaliza mwaka
2001 vizuri na kwa neema ya Mungu umeingia na kuanza mwaka huu wa 2002.
Sisi tunamshukuru Mungu kwa kutupa nafasi nyingine tena ya kutumika
pamoja naye katika shamba lake. Na Mungu, kwa njia ya Roho wake
Mtakatifu, ametupa Neno la kutusaidia na kutuongoza mwaka huu. Neno
lenyewe ni hili:
“
Basi, ‘Bwana’ ndiye Roho; walakini alipo Roho wa Bwana, hapo ndipo
penye uhuru” (2
Wakorintho 3:17)
Hili ndilo Neno tulilopewa
sisi kwa ajili ya mwaka 2002. Kila mwaka Mungu huwa
anatupa Neno la kusimama nalo kwa mwaka unaohusika. Nasi tumeona
katika barua hii tukuulize ikiwa Mungu amekupa Neno la kukuongoza mwaka
2002. Na kama bado hujapata, basi umwombe Mungu ili akupe Neno kwa ajili
yako. Ni muhimu sana!
Ikiwa unaamini ya kuwa ni
Mungu aliyekupa neema na nafasi ya kuufikia na kuishi katika mwaka 2002
– basi liko Neno aliloliandaa kwa ajili yako! Inawezekana jambo hili
ni jipya kabisa machoni pako. Pia, inawezekana unalijua, lakini siyo
jambo unaloliwekea umuhimu unaostahili.
Kumwomba Mungu akupe Neno
lake kwa ajili ya mwaka huu ni muhimu kwa sababu zifuatazo:
1. Neno
hilo linakusaidia kujua mawazo ambayo Mungu anakuwazia kwa mwaka huu:
Mungu
anasema katika Yeremia 29:11 ya kuwa; “Maana nayajua mawazo
ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani, wala si ya mabaya,
kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.” Pia katika kitabu cha
Isaya 55:8-9 anasema hivi; “ Maana mawazo yangu si mawazo yenu,
wala njia zenu si njia zangu; asema Bwana. Kwa maana kama vile mbingu
zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko
njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu”.
Halafu katika Isaya 55:10,11
anaendelea kutuambia ya kuwa,
“
Maana kama vile mvua ishukavyo, na theluji, kutoka mbinguni, wala
hairudi huko; bali huinywesha ardhi, na kuizalisha na kuichipuza, ikampa
mtu ampandaye mbegu, na mtu alaye chakula; ndivyo litakavyokuwa neno
langu, litokalo katika kinywa changu; halitanirudia bure bali litatimiza
mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma”.
Hapa tunajifunza ya kwamba
katika neno analotupa toka katika kinywa chake tunapata kujua mawazo
yake anayotuwazia; njia zake anazotuongoza ili tupite humo.
Lakini pia kwa wale
wapandaji (yaani wapelekaji) wa
neno lake kama sisi neno hilo tunapopewa linatupa mbegu ya kupanda, pia,
linatusaidia kunyweshea maji kama mvua mioyo (ardhi) ya watu ili zile
mbegu tulizopanda mwaka jana zichupue! Wakati huo huo ambapo neno hilo
linapokuwa mbegu ya kupanda mkononi mwa mpanzi; pia na wakati huo huo,
neno hilo hilo linakuwa chakula kwa alaye!
Kwa mfano kwetu sisi
tumepewa neno hili la 2 Wakorintho 3:17 ina maana katika neno hili
tunapata yafuatayo:
-
Mawazo anayotuwazia sisi na wale aliotupangia tuwahudumie mwaka
2002. Kwamba tukusudie kumpa Roho Mtakatifu nafasi anayostahili ili
kutuweka huru katika maeneo yote maishani mwetu ambayo hayako huru
kama ipasavyo katika Kristo Yesu!
-
Njia au mipango yake kwa mwaka 2002. Kwa sababu imeandikiwa; “Neno
lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu” (Zaburi
119:105)
-
Tutaona Bwana akilithibitisha neno hili kwa ishara na miujiza (Marko
16:20); kwa kuwa Mungu ana tabia ya kuliangalia na kulifuatilia neno
lake na kulitimiza (Yeremia 1:12). Kwa hiyo imani inaongezeka ndani
yetu (Warumi 10:17) ya kutegemea na kutarajia kumwona Mungu kwa upya
na kwa nguvu zaidi kuliko miaka iliyopita!
2.
Neno
hilo unalopewa ndilo linalokupa tarajio la kupokea mema toka kwa Mungu.
Maana imeandikwa hivi; “Umemtendea mema mtumishi wako, Ee, Bwana,
sawasawa na neno lako” (Zaburi 119:65). Mema aliyokuandalia Mungu
kwa mwaka huu, yatakujia sawa sawa na Neno analolituma kwako.
3.
Neno hilo unalopewa
linakupa msingi mzuri wa maombi yako kwa mwaka 2002. Maana
imeandikwa hivi; “ Na huu ndio ujasiri tulio nao kwake, ya kuwa,
tukiomba kitu sawasawa na mapenzi yake atusikia. Na kama tukijua kwamba
atusikia, tuombacho chote, twajua kwamba tunazo zile haja tulizomwomba”
(1Yohana 5:14,15). ‘ Sawasawa na mapenzi yake’, maana yake ‘
sawasawa na neno lake’.
Ziko
sababu nyingine ambazo tungeweza kukupa ili kukuhumiza upende kumwomba
Mungu akupe neno la kusimama nalo katika maisha yako kwa mwaka huu.
Lakini hizi chache tulizokuandikia katika barua hii tunaamini zinatosha
kukupa changamoto ya kulifuatilia jambo hili zaidi
Kumbuka mwaka mmoja hauna
siku nyingi, na siku moja haina masaa mengi hata ukadhani unaweza
kufanya kila kitu unavyotaka na wakati utakapo. Kwa hiyo ili uwe
‘focused’ au uwe na lengo au matazamo kwa mwaka huu kusudia kufahamu
na kufanya kile Mungu anachotaka ufanye mwaka huu!
Kumbuka pia Mungu ametupa
mwaka huu ili tumzalie matunda. Na huwezi kumzalia Mungu matunda peke
yako bila neno lake.
Kumbuka pia ya kuwa kwa
kukupa neno la mwaka huu usifikiri Mungu hatakupa maneno mengine baadaye
mwaka huu. Tega sikio lako, Mungu anaweza kukupa maneno mengine ya
kukusaidia wakati wowote kufuatana na hitaji unalokuwa nalo, na pia
kufuatana na kile anachotaka ukijue wakati huo.
Mwisho
Tuzidi
kuombeana. Tunaamini utasimama pamoja nasi tena mwaka huu ili Kanisa la
Bwana lilishwe, Ufalme wa Mungu ujengwe na Jina la Yesu litukuzwe.
Semina tulizonazo mbele yetu mwaka huu ni Moshi tarehe 27 Januari hadi
tarehe 3 Februari , Tanga tarehe 12 –17 Februari, Arusha tarehe 25
Februari hadi tarehe 3 Machi. Unaweza ukaona ratiba yetu nzima katika
sehemu ya ratiba katika mtandao wetu (www.mwakasege.org)
au wasiliana nasi kwa simu hii 2504289
Mungu
akubariki kila siku,
Ni
sisi katika utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege.