Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
BARUA ZA MWEZI


Barua ya Mwezi Machi 2002

"Kama Kristo hakufufuka….."

Mpendwa katika Yesu Kristo.

        Salamu!

        Tunafurahia mioyoni mwetu ya kuwa Mungu ametupa tuwasiliane tena mwezi huu wa Machi 2002 kwa njia ya barua hii. Tunaamini Roho Mtakatifu amekuongoza uisome barua hii kwa makusudi kamili yenye lengo la kukusogeza hatua zaidi mbele katika maisha uliyonayo ndani ya Kristo.

        Je! unajua ni hali gani tungekuwa nayo kama Kristo asingekuwa amefufuka? Umewahi kutulia angalau kwa muda mfupi ukatafakari juu ya swali hili? Je! unajua umuhimu wa kuwa na uhakika wewe binafsi ya kuwa Yesu amefufuka? Hata ukisoma katika biblia utaona ya kuwa Yesu baada ya kufa na kufufuka lakini kabla ya kupaa aliwadhihirishia wanafunzi wake; "…. kwa dalili nyingi…..ya kwamba yu hai, akiwatokea siku arobaini, na kuyanena mambo yaliyohusu ufalme wa Mungu" (Matendo ya Mitume 1:3). Lazima kulikuwa na sababu muhimu sana zilizomfanya ajidhihirishe namna hiyo kwa wanafunzi wake ya kuwa amefufuka na kwamba yu hai!

Je! unaamini kwa furaha ya kuwa Yesu amefufuka?

        Kuna wakati wanafunzi wa Yesu walipoambiwa ya kuwa amefufuka, hawakuamini (Luka 24:10-12; 36-43). Lakini baadaye walipokwenda kaburini na kukuta mwili haupo – walijua na kuamini ya kuwa amefufuka lakini si kwa furaha. Hata baada ya kuwatokea wakiwa wamejifungia ndani ya nyumba hawakuamini kwa furaha hadi alipokula nao chakula walichokuwa nacho?

        Je! unajua ya kuwa hata sasa hata kama unaamini ya kuwa Yesu amefufuka – huwezi kuwa na furaha kama Yesu huyu aliyefufuka asipojifunua katika maisha yako ya kila siku na "kula chakula ulichonacho mbele yako"? Maana yake ajifunue katika maisha yako ya kila siku – hapo ndipo furaha ya wengi inaongezeka katika kumwamini Kristo.

        Imeandikwa katika kitabu cha Luka 24:40,41 ya kuwa; " Na baada ya kusema hayo aliwaonyesha mikono yake na miguu yake. Basi walipokuwa hawajaamini kwa furaha wakistaajabu, aliwaambia, mna chakula cho chote hapa? Wakampa kipande cha samaki wa kuokwa. Akakitwaa, akala mbele yao."

        Ikiwa umeokoka na huna furaha au ikiwa unaamini ya kuwa Yesu Kristo amefufuka na huna furaha – mara nyingi ni kwa sababu mbili kubwa. Kwanza, ni kwa sababu humwoni Yesu akajifunua na kujidhihirisha katika maisha yako ya kila siku kwa mfano kazini kwako au katika masomo yako au katika biashara yako, au katika ndoa yako. Je!unamwona Yesu aliyefufuka katika maisha yako? Ikiwa humwoni basi ni maombi yetu kwa Mungu ya kuwa Yesu ajifunue katika maisha yako ya kila siku na uone baraka za kufufuka kwake.

        Pili: Huna furaha hata kama umeokoka na unaamini ya kuwa Yesu amefufuka kwa sababu unashindwa kupata ufunuo ndani yako unaoweza kulinganisha neno la Mungu na kujifunua kwa Yesu katika maisha yako ya kila siku. Ndiyo maana baada ya Yesu kula samaki "mbele yao", aliwaambia; " Hayo ndiyo maneno yangu niliyowaambia nilipokuwa pamoja nanyi, ya kwamba ni lazima yatimizwe yote niliyoandikiwa katika torati ya Musa, na katika Manabii, na Zaburi" (Luka 24:44). Na katika mstari unaofuata wa 45 tunasoma ya kuwa;l "Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko".

        Ni dhahiri ya kwamba Yesu aliwahi kusema nao juu ya maandiko yaliyohusu maisha yake katikati yao na hawakuyaelewa. Kwa hiyo akawafunulia akili zao wapate kuyaelewa hayo maandiko – yaani wapate kulinganisha kuwepo kwa Yesu katikati yao na maandiko! Kwa hiyo baada ya kumwona Yesu akipaa na kuchukuliwa juu mbinguni, biblia inasema;

"Wakamwabudu; kisha wakarudi Yerusalemu  wenye furaha kuu" (Luka 24:52)

        Kwa hiyo ni muhimu na wewe uweze kulinganisha neno la Mungu na kuwepo kwa Yesu aliye hai katikati yako. Bila hili furaha yako inapungua. Ni maombi yetu kwa Mungu ya kuwa "atakuwa anakufunulia akili zako kila siku upate kuyaelewa maandiko."

Kama Kristo hakufufuka…..…… hakuna aliyekufa atakayefufuka!

        Ndiyo! Kama Kristo hajafufuka, basi hakuna kiyama ya wafu au hakuna aliyekufa atakayefufuka! Imeandikwa hivi:

"Basi, ikiwa Kristo nahubiriwa ya kwambaamefufuka katika wafu, mbona baadhi yenuhusema kwamba hakuna kiyama ya wafu?Lakini kama hakuna kiyama ya wafu, Kristonaye hakufufuka….. Maana kama wafuhawafufuliwi, Kristo naye hakufufuka….. Na hapowao nao waliolala katika Kristo wamepotea(1Wakorintho 15:12,13,16,18)

        Lakini tunajua ya kuwa Yesu amefufuka – Yuko hai na kwa sababu hiyo iko siku atayowafufua wote waliokufa. Wengine watapata nafasi ya kukaa naye milele mbinguni na wengine watatupwa katika Ziwa la Moto katika mateso ya milele. Soma Ufunuo wa Yohana 20:11-15 na 1Wathesalonike 4:13-17)

Kama Kristo hakufufuka……...…..basi, imani yetu ni bure!

        Imani ya Kikristo imesimama kwenye kitu gani? Imesimama katika Yesu Kristo aliyesulubiwa, akafa, akazikwa, na akafufuka. Kama Kristo asingekuwa amefufuka, kusulubiwa kwake, kufa kwake na kuzikwa kwake kusingekuwa na faida yo yote kwetu wakati huu. Ndiyo maana imeandikwa:

"Na kama Kristo hakufufuka, imani yenu ni bure;mngalimo katika dhambi zenu na kama katika maishahaya tumemtumaini Kristo, sisi tu maskinikuliko watu wote" (1 Wakorintho 15:17,190

        Ikiwa Yesu hakufufuka isingekuwa rahisi kwa sasa kupata msamaha wa dhambi, au kupata ondoleo la dhambi au kupata uzima wa milele! Hii ni kwa sababu haya yote tunayapata kwa njia ya Roho Mtakatifu. Na Roho Mtakatifu asingeweza kuja na kufanya hayo kwa kila anayemwamini Yesu aliyefufuka kama Yesu asingekuwa amefufuka. Hii ni kwa sababu Roho Mtakatifu hakuja kwetu hadi Yesu alipotukuzwa na kuketi mkono wa kuume wa Mungu baada ya kufufuka. Soma Yohana 7:37-39; Yohana 16:7-16.

Kama Kristo hakufufuka…...…..basi, kuhubiri kwetu ni bure!

        Je! unajua kwa nini Yesu Kristo alipofufuka alitaka sana na akahakikisha ya kwamba wanafunzi wake wanapata uhakika ya kuwa amefufuka? Ni kwa sababu alikuwa anataka wawe ‘mashahidi’ wake ya kuwa yote aliyoandikiwa yalitokea kama yalivyoandikwa katika " torati ya Musa, zaburi na Manabii" (Luka 24:36-53). Na ya kwamba wanafunzi wake wazunguke na kutangaza habari njema za msamaha wa dhambi na uzima wa milele unaopatikana katika Yesu Kristo aliyefufuka. Mtume Paulo aliandika hivi;

"Tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubirikwetu ni bure na imani yenu ni bure. Naam,na sisi tumeonekana kuwa mashahidi wa uongowa Mungu; kwa maana tulimshuhudia Munguya kuwa alimfufua Kristo, ambaye hakumfufua,ikiwa wafu hawafufuliwi" (1Wakorintho 15:14,15)

        Kwa maneno mengine Mtume Paulo angeweza kusema hakuna sababu ya kuhubiri habari za Yesu ikiwa hakufufuka. Au Yesu aliyekufa lakini hakufufuka hana faida yo yote ukimhubiri. Lakini Yesu aliyekufa na kufufuka ana faida kwa anayemhubiri na kwa anayehubiriwa pia. Uzuri wa kumhubiri Yesu Kristo aliyefufuka ni kwamba huwa analithibitisha hilo neno linalohubiriwa juu yake kwa ishara na miujiza. Soma Marko 16:20.

Kama Kristo hakufufuka….…..basi, Jina la Yesu haliwezi kuwa na nguvu!

        Hata katika maisha haya ya kawaida kibinadamu, jina la mtu linapoteza nguvu yake pale anapokufa. Kwa sababu mwenye jina hayupo kufanya yale ambayo alikuwa anayafanya alipokuwa hai. Akiisha kufa hawezi tena kuyafanya mambo hayo, na jina lake likiitwa hawezi kujitokeza mwenyewe – maana amekufa. Jina lake likiitwa baada ya yeye kufa, hawezi kujitokeza – rafiki au ndugu au majirani zake wanaweza kujitokeza kwa niaba yake, lakini hawawezi kufanya alivyokuwa anafanya! Wanaweza kuiga vitendo alivyokuwa akifanya lakini haviwezi vikawa halisi.

        Imeandikwa katika Waebrania 13:8 ya kuwa; "Yesu Kristo ni yeye yule , jana na leo na hata milele". Huu mstari hauwezi kuwa kweli kama Yesu Kristo hajafufuka. Na kwa kuwa amefufuka, Jina lake lina nguvu sana, kwa sababu ukimwita anaitika na kufanya yale yale aliyokuwa anayafanya alipokuwa hai. Kwa mfano, kabla ya kufa alikuwa anaponya wagonjwa, kwa hiyo hata baada ya kufufuka akiitwa kwa jina lake Yesu kuponya wagonjwa anakuja anawaponya!

        Tunasoma katika kitabu cha Matendo ya Mitume sura ya tatu habari za mtu aliyekuwa kiwete tangu tumboni na akaponywa kwa Jina la Yesu Kristo baada ya Petro kumwombea. Watu waliokuwepo walistaajabu sana wakifikiri akina Petro wamemponya mtu huyo kwa nguvu zao au kwa utakatifu wao. Ilimbidi Petro aliweke wazi jambo hili ili wajue huyo kiwete kapona kwa namna gani. Petro akawaambia hivi; "Mungu wa Ibrahimu na wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa baba zetu, amemtukuza mtumishi wake Yesu, ambaye ninyi mlimsaliti….mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi wake. Na kwa imani katika Jina lake, jina lake limemtia nguvu mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele yenu ninyi nyote"(Matendo ya Mitume 3:13,15,16)

Mwisho

        Tulitaka katika barua hii tukukumbushe ya kuwa Yesu Kristo amefufuka na ya kwamba Yuko hai kwa ajili yetu wote; na ulimwengu unatakiwa kuhubiriwa habari hii njema! Tuzidi kuombeana.

ni sisi katika utumishi wa Kristo,

Christopher na Diana Mwakasege

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.