Barua ya Mwezi Mei 2002
MFIKIRIE
MUNGU KWANZA KATIKA MAISHA YAKO
Mpendwa katika Kristo,
Tunakusalimu
katika Jina la Yesu Kristo.
Mwezi huu tunakuja kwako na swali hili: “Ni njia zipi unazozitumia
kumwonyesha Mungu ya kuwa Yeye ndiye wa kwanza katika maisha yako?”
Kama unavyofahamu sisi huwa tunasafiri sana sehemu mbalimbali nchini na
nje ya nchi kwa ajili ya kufanya semina za neno la Mungu. Siku moja
tulipofika katika mji fulani, mtu mmoja alikuja na akatupatia fedha
akisema zitusaidie kulipia gharama za safari za kupeleka neno la Mungu.
Tukamshukuru
Mungu kwa ajili yake na kwa ajili ya fedha hizo, kwa kuwa ni kweli
tulikuwa tunazihitaji wakati huo. Kwa kuwa tulikuwa safarini na tulikuwa
tunazihitaji tukaanza kuzitumia mara moja kulipia gharama za mizigo ya
vyombo vya huduma tulivyokuwa tumesafiri navyo.
Lakini
tulipochukua kiasi cha fedha na kulipia mizigo ya vyombo tulikosa amani
mioyoni mwetu. Tulijua mara moja ya kuwa jambo hilo halikumfurahisha
Roho Mtakatifu – kwa hiyo tukataka kujua tumekosea wapi! Roho
Mtakatifu akatuwekea swali hili ndani ya mioyo yetu; “Je! Mungu ni
wa kwanza katika maisha yenu na kila siku?” Wakati tunashangaa juu
ya swali hilo, akaongeza lingine; “ Ikiwa Mungu ni wa kwanza katika
maisha yenu, mbona mlipopokea hizo fedha hamkutoa kwanza zaka ya Mungu
kabla ya kuanza kuzitumia hizo fedha?”
Ghafla tukatambua kosa letu na tukatubu wakati huo huo. Na tunaamini
Mungu ametusamehe!
Wewe
ungekuwa umeulizwa swali kama tuliloulizwa sisi ungelijibu namna gani?
Au hata sasa utajibu namna gani tukikuuliza ya kuwa je, Mungu ana nafasi
ya kwanza katika maisha yako kabla au kuliko mtu au kitu chochote. Ni
rahisi sana kujibu ‘ndiyo’ bila kutafakari kwa undani ikiwa
kama ndivyo Mungu anavyokuona.
Je!
unaelewa maana ya maneno haya aliyoyasema Yesu juu ya Mafarisayo
aliposema; “Watu hawa huniheshimu kwa midomo, ila mioyo yao iko
mbali nami. Nao waniabudu bure ……” (Mathayo 15:8,9). Kwa lugha
rahisi alitaka wajue ya kuwa wanachosema, wanachowaza na wanachofanya
havifanani! Hawawezi wakasema wanampenda Mungu huku mioyo yao inawaza
mawazo yanayoonyesha kutokumpenda Mungu, na kwa sababu hiyo hata matendo
yao yatakuwa ‘bure’ mbele za Mungu maana yake hayatawaletea ‘faida’
au ‘baraka’ yoyote.
Kama
Mungu ni wa kwanza katika maisha yako na unamwabudu yeye basi jizoeze
umfikirie Mungu kwanza katika matumizi yako ya fedha, ya mali ulizonazo,
ya muda ulionao, nakadhalika.
Tuzidi
kuombeana.
ni
sisi katika utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege