|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
SEHEMU
YA ISHARA NA MIUJIZA KATIKA UINJILISTI
Mpendwa katika Kristo. Salamu
katika Jina la Yesu Kristo tunakupa tukijua ya kuwa Mungu anakupenda na
anazidi kukupigania na kukushindia. Tunafurahi ya kuwa Roho Mtakatifu
ametupa nafasi hii tena tuseme na wewe angalau kwa uchache habari za
Bwana Yesu kwa siku hizi za sasa. Yesu alipokuwa Yerusalemu Biblia inatuambia ya kwamba: “Watu
wengi waliamini jina lake, walipoziona ishara zake alizozifanya” (Yohana
2:23). Na alipokuwa akienda zake ng’ambo ya Bahari ya Galilaya, Biblia
inasema; “Na mkutano mkuu wakamfuata, kwa sababu waliziona ishara
alizowafanyia wagonjwa” (Yohana 6:2) Unaweza ukaona kabisa unaposoma maisha ya Yesu na huduma
yake alipokuwa duniani, ishara na miujiza vilikuwa vivutio vikubwa
vilivyowafanya watu wamfuate, wamsikilize na kumwamini. Tunajua ya kuwa
Yesu Kristo yuko hai sasa. Je! unadhani amebadilika? Waebrania 13:8
inasema hajabadilika! Ikiwa ishara na miujiza vilikuwa muhimu katika huduma yake
wakati ule, na kwa kuwa hajabadilika tunaamini vitakuwa muhimu katika
huduma yake hata leo ndani ya wale wote waliompokea katika maisha yao. Imeandikwa katika Yohana 20:30,31 ya kuwa; “ Basi kuna
ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake,
zisizoandikwa ħkatika kitabu hiki. Lakini hizi zimeandikwa; ili
mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa
kuamini mwe na uzima kwa jina lake.” Uinjilisti katika mwanzo wa
kanisa Ukisoma maagizo ya Bwana Yesu utaona wazi ya kuwa alitaka
huduma ya wanafunzi wake ya uinjilisti na kulitangaza neno la ufalme wa
Mungu, isiwe kwa maneno matupu. Bali iandamane na ishara na miujiza!
Soma Mathayo 10: 7, 8; Luka 9:1,2 na Marko 16: 17-20. Hebu tuangalie mifano ifuatayo jinsi inavyounganisha
uinjilisti pamoja na ishara na miujiza. Mfano wa Kwanza: Matendo 2:1-41. Ilipotokea ishara ya kunena kwa lugha,
Mtume Petro alipata nafasi ya kuhubiri kwa lile kundi lililokusanyika
kushangaa hiyo ishara. Matokeo yake ni “ Watu wapata elfu tatu”
kuokoka na kuwa wakristo. Mfano wa Pili: Matendo ya Mitume sura ya 3 na ya 4: Ulipotokea muujiza wa
kiwete kusimama na kutembea, Mtume Petro alipata nafasi tena ya
kuwahubiri watu waliokuwa wanashangaa muujiza huo habari za Yesu.
Matokeo yake ni watu wengine elfu tano kuokoka na kumfuata Yesu. Mfano wa Tatu: Matendo 8:5-8: Filipo alipohubiri katika mji wa samaria,
Biblia inasema hivi: “ Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno
yale yaliyosemwa na Filipo walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa
akizifanya. Kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao,
wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Mtume Paulo anapowaandikia wakristo waliokuwa Korintho
anasema: “Na neno langu na kuhubiri kwangu hakukuwa kwa maneno ya
hekima yenye kushawishi akili za watu, bali kwa dalili za Roho na za
nguvu…..” Kwa nini: “….ili imani yenu isiwe katika hekima ya wanadamu, bali
katika nguvu za Mungu” (1Wakorintho 2:4,5). Lengo kuu la uinjilisti ni kuwapelekea watu habari za Yesu
Kristo ili wapate kumjua na kumwamini kama Bwana na Mwokozi wa maisha
yao ya kila siku. Kibiblia, tunajua ya kuwa Yesu Kristo ndiye ‘njia’
pekee ya kwenda mbinguni. Yesu aliwahi kusema kuwa “….. mtu haji
kwa Baba, ila kwa njia ya mimi” (Yohana 14:6). Kwa lugha iliyo
nyepesi ni kwamba hakuna mtu atakayekwenda mbinguni ikiwa hajapatana na
Bwana Yesu kabla hajafa. Huu ndio ukweli, na ni ukweli ulio na msukumo ndani yake.
Msukumo huu ni ule wa kutaka kila mtu apate nafasi ya kuisikia injili (habari
njema za Yesu Kristo). Mtu yeyote anayemwamini Yesu Kristo kama Bwana na
Mwokozi wake hawezi kukosa msukumo huu ndani yake; kwa sababu anajua ya
kuwa mtu akifa bila Yesu, anaishia jehanamu. Je! unajua hili? Je! unajua ya kuwa nusu ya watanzania siyo wakristo?
Makisio ya karibuni ya takwimu mbalimbali yanaonyesha ya kuwa asilimia
47 tu ya watanzania wote ndiyo wakristo. Nasi tunajua ya kuwa si
wakristo wote hawa wameokoka. Wengine ni wakristo wa jina tu, lakini
maisha yao hayana ushuhuda wowote ya kuwa wana- Yesu ndani yao mioyo yao. Fikiria kwa mfano Yesu arudi leo! Itakuwaje kwa wale ambao
hawamjui? Au kwa wale waliomsikia lakini hawakutaka kumwamini? Au kwa
wale wanaodhani wanaweza kumkwepa Yesu, wapite “njia”
nyingine wapate kufika mbinguni? Ikiwa wewe ni msomaji wa Biblia, basi
unajua hali inavyoweza kuwa Yesu akirudi leo. Kwa sababu hii, ni muhimu tutafute njia au mbinu ya
kuwafikishia watanzania injili kwa namna ambayo watampokea Yesu na
kumwamini kwa haraka na kuwa uwingi. Kumbuka Biblia haituruhusu
kumlazimisha mtu kumwamini Yesu na kuokoka au kuwa mkristo. Ni hiari ya
mtu. Ni chaguo lake. Kazi yetu ni kuhakikisha kuwa amemsikia na kumwona
Yesu – halafu aamue mwenyewe! Mbinu mmojawapo muhimu ya kutusaidia kufanya uinjilisti wa
namna hii ni kwa kutumia ishara na miujiza anayofanya Bwana Yesu
mwenyewe – kama tutampa nafasi afanye! Yesu alipokuwa duniani Unaposoma habari za Yesu Kristo katika injili zote nne za
Mathayo, Marko, Luka na Yohana utaona ya kuwa: Watu wengi walimwamini
Yesu kwa kuona ishara alizofanya na miujiza aliyofanya kuliko kwa maneno
aliyosema. Utaona wazi ya kuwa ishara na miujiza vilikuwa vitendea kazi
muhimu katika kuwathibitishia watu; Yeye ni nani na ametoka wapi. Hebu
tafakari maneno haya ambayo Yesu alisema; “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini
nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua
na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba”
(Yohana 10:37,38) Yesu Kristo alipoulizwa na Wayahudi kama yeye ndiye Kristo
akawajibu akasema, “Naliwaambia, lakini ninyi hamsadiki; Kazi hizi
ninazozifanya kwa jina la Baba yangu ndizo zinazonishuhudia” (Yohana
10:24,25. Wanafunzi wa Yohana walipouliza swali kama hilo la Wayahudi
baada ya kutumwa na Yohana alipokuwa gerezani; - Yesu aliwajibu kwa
vitendo kwanza! Biblia inasema, “ Na saa ile ile aliwaponya wengi
magonjwa yao, na misiba na pepo wabaya; na vipofu wengi aliwakirimia
kuona. Ndipo alipojibu, akawaambia, Nendeni mkamweleze Yohana hayo
mliyoyaona na kuyasikia. Vipofu wanapata kuona, viwete wanatembea, wenye
ukoma wanatakasika, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, maskini
wanahubiriwa habari njema.” ( Luka 7:19-22). Nikodemo alipokwenda kumwona Yesu usiku alianza kwa kusema,
“ Rabi, twajua ya kuwa u mwalimu, umetoka kwa Mungu; kwa maana
hakuna mtu awezaye kuzifanya ishara hizi uzifanyazo wewe, isipokuwa
Mungu yu pamoja naye” (Yohana 3:2). Kwa hiyo tunajua ya kwamba
kilichomvuta Nikodemo amfuate Yesu ni zile ishara alizoziona na kusikia
Yesu Kristo akizifanya. Je! unafikiri Yesu aliyekuwa ndani ya wanafunzi wa kwanza,
akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha neno walilohubiri na
kufundisha kwa ishara na miujiza amebadilika? Hapana! Ikiwa hajabadilika
siku hizi je! yuko wapi? Hata leo inawezekana! Tunajua Yesu yuko hai leo. Hajabadilika. Alichofanya “jana”
anao uwezo wa kukifanya hata “leo”. Utaona mara nyingine kama kukitokea muujiza au ishara watu
wanakusanyika kutaka kujua “kulikoni”. Hapo ndipo nafasi
nzuri yakuwaambia habari za Yesu anayefanya ishara mpaka leo. Tumeona
hili likitokea mara kwa mara. Wakati fulani tulipokuwa Tanga mjini tuliona watu wengi
wakiongezeka kuja kwenye semina tuliyokuwa tunafundisha mwanzoni mwa
mwaka huo waliposikia jinsi wagonjwa walivyokuwa wanapona. Mtu mmoja
ambaye alikuwa hajaokoka alikuja akitaka uponyaji katika sikio lake
lililokuwa limeziba na kutokusikia kwa muda wa miaka mitatu. Wakati wa
maombi ya wagonjwa akapona na akaanza kusikia tena katika sikio
lililokuwa limeziba. Na wagonjwa wengine walipona pia. Tulipotangaza ya
kuwa wanaotaka kumpokea Yesu huyu anayeponya apate kuwaokoa, wengi
walitoka mbele kuombewa ili waokoke, pamoja na yule aliyepona sikio! Usiseme mimi siwezi! Nenda kasome katika Biblia alichosema
Yesu! Katika Marko 16:17-20 alisema; “Kila aaminiye….”.
Kama unamwamini Yesu ya kuwa ni Mwana wa Mungu, amefufuka na ni Mwokozi
– neno ‘kila’ linakuhusisha na wewe! Katika Yohana 14:12
anasema, “ Yeye aniaminiye mimi ……” Hii inakuhusisha na
wewe! Chukua hatua. Tumia nafasi Mungu anayokupa unapokutana na mgonjwa.
Mwombee akikuruhusu umwombee au ndugu zake wakikuruhusu. Kazi yako ni
kuomba. Kazi ya Bwana Yesu uliye naye ni kuponya. Sifa na heshima si
zako bali za Bwana Yesu anayeponya hata leo! La kukusaidia! Inawezekana una hofu. Ujasiri wa kuchukua hatua huna. Au
uliwahi kuombea mtu hakupona au ulipata vitisho. Jizoeze kuomba maombi
haya: “Basi, Bwana, yaangalie matisho ya wanaonitisha na
kunikatisha tamaa katika huduma hii. Unijalie mtumishi wako kunena neno
lako kwa ujasiri wote, ukinyoosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu
vifanyike kwa jina la Mtumishi wako Mtakatifu Yesu. Amina”. Sala hii tumeichukua katika maneno ya maombi ya wanafunzi
katika kitabu cha Matendo 4:29-31. Sisi wenyewe tumekuwa tukiomba mara
kwa mara kwa ajili yetu na mahali tunapokwenda kuhudumu. Na tumeona
matokeo yake yanavyozidi kujitokeza, na bado tunaendelea kuomba sala hii
mara kwa mara. Unaweza na wewe ukaomba sala hii au kwa maneno mengine
jinsi Roho Mtakatifu atakavyokupa. Omba kwa ajili yako; na omba kwa
ajili ya mahali unaposali au unapoabudu. Lengo: Yesu aonekane watu
wamwamini. Anza leo! Shukrani. Mzigo
ulio nao wa kutusaidia katika maombi kwa ajili ya huduma ambayo Mungu
ametupa – zidi kuwa nayo na Mungu akutie nguvu uendelee. Tunahitaji
hayo maombi. Ahsante pia kwa kila mtu aliyejitoa kwa mali na/au muda
wake kutusaidia tufanikiwe katika huduma ya Bwana. Mungu wetu na azidi
kukuzidishia sawa sawa na ahadi zake. ni sisi katika utumishi wa Kristo, Christopher na Diana Mwakasege |
|