|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
KUFUNGA HUKO
KUNAKUBALIKA? Salamu
katika Jina la Yesu Kristo. Kuna Faida katika kufunga Tunasoma katika Biblia kuwa watu wa Ninawi waliposikia
maonyo ya Nabii Yona, ya kuwa Mungu amekusudia kuwaangamiza wasipotubu
na kuacha dhambi, wakatangaza maombi ya kufunga.
“Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; Wakatangaza kufunga,
wakajivika nguo za magunia, tangu yeye aliye mkubwa hata aliye mdogo”.
(Yona 3:5)
“Mungu akaona matendo yao, ya kuwa wameiacha njia yao mbaya Basi
Mungu alighairi neno lile baya, ambalo alisema atawatenda, asilitende”.
(Yona 3:10)
Watu wa Ninawi, walifanya maombi ya kufunga wakamlilia Mungu kwa nguvu,
na Mungu akawasamehe.
Yesu Kristo alipokuwa hapa duniani, kabla ya kuanza kazi yake rasmi,
alifunga.
“Kisha Yesu alipandishwa na Roho nyikani, ili ajaribiwe na Ibilisi.
Akafunga siku arobaini mchana na usiku, mwisho akaona njaa” (Mathayo
4:12)
Huko nyikani alikuwa anajaribiwa na Ibilisi – lakini alishinda.
“Kisha Ibilisi akamwacha na Tazama, wakaja malaika wakamtumikia” (Mathayo
4:1)
Pia, wanafunzi wa Yesu walikuwa na tabia ya kufanya maombi ya kufunga,
baada ya Yesu kupaa. “Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana Ibada
na kufunga Roho Mtakatifu akasema nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi
ile niliyowaitia. Ndipo wakiisha kufunga na kuomba wakaweka mikono yao
juu yao, wakawaacha waende zao” (Matendo 13:2,3).
Hata siku hizi watu wengi wanafanya maombi ya kufunga. Wengine
wanajibiwa na wengine hawajibiwi. Wengine ni Wakristo na wengine si
wakristo. Mara nyingi mtu anapokuwa katika kufunga, huacha kula chakula
kabisa kwa muda fulani au kuacha kula vyakula fulani fulani tu, na
vingine anakula kama kawaida.
Maombi ya namna hii, kuna wakati hufanya baadhi ya watu kudhoofu miili
yao licha ya hayo, wakati mwingine hakuna baraka zozote zinazopatikana
wala maombi hayajibiwi. Hata ukimuamuru pepo amtoke mtu hukataa, ingawa
uliifanya maombi ya kufunga. Wakati mwingine unafunga, na maombi yako
yanajibiwa. Je kuna mtu yeyote katika Biblia ambaye
aliomba kwa kufunga na kuona mambo hayabadiliki?
Ndiyo! Mmojawapo ni Mfalme Daudi.
Wakati wa mwaka mpya, huko Yerusalemu, Mfalme Daudi alianguka katika
dhambi ya uzinzi, baada ya kumtamani mke wa askari wake Uria, Mhiti;
Huyo mwanamke aliitwa Bath-Sheba, binti Eliamu.
“Basi Daudi akapeleka wajumbe, wakamtwaa; naye akaingia kwake, naye
akalala naye……kisha akarudi nyumbani kwake. Yule mwanamke akachukua
mimba basi akapeleka na kumwambia Daudi akasema ni mjamzito”
(2 Samweli 11:4.5)
“Hata ikawa asubuhi, Daudi akamwandikia Yoabu waraka, akaupeleka
kwa mkono wa Uria. Akaandika katika Waraka huo, akasema, mwekeni Uria
mbele ya watu penye vita vikali, kisha ondokeni, ili apigwe akafe”
( 2 Samweli 11:14,15)
Uria Mhiti, akafa vitani, Daudi akamchukua mke wake na akamzalia mtoto.
“Lakini jambo lile alilolitenda Daudi likamchukiza Bwana”
(2 Samweli11:27)
Bwana akamkemea Daudi kupitia kwa Nabii Nathani “Daudi akamwambia
Nathani, Nimemfanyia Bwana dhambi. Nathani akamwambia Daudi, Bwana naye
ameiondoa dhambi yako; hutakufa. Lakini kwa kuwa kwa tendo hili umewapa
adui za Bwana nafasi kubwa ya kukufuru, mtoto atayezaliwa hakika yake
atakufa” (2 Samweli 12:13,14)
“Basi Daudi akamwomba Mungu kwa ajili ya mtoto Daudi akafunga
akaingia akalala usiku kucha chini. Nao wazee wa nyumba yake wakaondoka
wakasimama karibu naye, ili wamwinue katika nchi, lakini hakukubali wala
hakula chakula pamoja nao. Ikawa siku ya saba yule mtoto akafa” (2
Samweli 12:16,17).
Licha ya kwamba Daudi alifunga siku saba usiku na mchana, bila kula na
kunywa chochote maombi yake hayakukubalika. Kumbuka alikuwa Mfalme
mteule wa Israeli, Taifa la Mungu, aliyepakwa mafuta, na aliyesaidiwa
sana na Mungu. Lakini wakati huu Mungu hakusikia maombi yake.
Je kuna wakati katika maisha yako umewahi kuwa na hali kama ya Daudi?
Ingawa umeokoka, umeomba kwa kufunga na kwa kulia siku nyingi lakini
hujajibiwa? Tatizo ulilotaka litatuliwe na Mungu, bado unalo na limekuwa
mwiba maishani mwako.
Wakati mwengine umeomba kwa kufunga ili ubarikiwe kiroho – unaona
hakuna kitu. Unaona ni kama unapiga ukuta. Na wengine wameomba kwa
kufunga juu ya wokovu wa ndugu zao na watoto wao lakini wanaona hakuna
mabadiliko.
Umewahi kujiuliza ni kwa nini haya yatokee? Je umewahi kuwa na mawazo ya
namna hii ya kumuuliza Mungu? Mbona tumefunga, lakini huoni? “Mbona
tumejitaabisha nafsi zetu, lakini huangalii?” (Isaya 58:3)
Kama umewahi kuwa na maswali ya namna hii, Bwana anakujibu hivi katika
Isaya 58:3-5 “Fahamuni siku ya kufunga kwenu mnatafuta anasa zenu
wenyewe na kuwalemea wote watendao kazi kwenu. Tazama ninyi mwafunga
mpate kushindana na kugombana na kupiga kwa ngumi ya uovu. Hamfungi siku
hii ya leo hata kuisikizisha sauti yenu juu. Je kufunga namna hii ni
saumu niliyochagua mimi? Je! ni siku ya mtu kujitaabisha Nafsi yake? Ni
kuinama kichwa cha unyasi, na kutanda nguo za magunia na majibu chini
yake? Je! utasema ni siku ya kufunga, na ya kukubaliwa na Bwana.”
Hebu soma tena maswali haya “Je! kufunga namna hii ni saumu
niliyochaugua mimi? ……. Je! utasema ni siku ya kufunga, na ya
kukubaliwa na Bwana?”
Maana yake nini maswali haya? Maana yake ni kwamba si kila maombi ya
kufunga yanakubalika mbele ya uso wa Bwana. Na yasipokubalika mbele ya
Mungu, hayawezi kujibiwa.
Inawezekana kabisa kuwa, maombi yako uliyofanya kwa kufunga hayajajibiwa,
kwa kuwa kufunga ulikofanya hakujakubalika mbele za Bwana. Una uhakika
gani kuwa, Mungu anakufurahia kujinyima chakula kwako unapoomba juu ya
jambo fulani? Je! kufunga namna hiyo ni Bwana amekuongoza, au umeona
wenzio wakifanya hivyo na wewe ukafuata. Kwa nini ufanye maombi ya kufunga?
Maombi ya kufunga ni maombi ya wito. Hakuna mtu anayefanya maombi ya
kufunga bure. Lazima kunakuwa na sababu.
Kuna wito wa kutoka nje. Mtu anaambiwa kufunga kwa kusikia toka kwa mtu
mwingine. Watu wa Ninawi walisikia wito toka nje nao wakafunga “
Basi watu wa Ninawi wakamsadiki Mungu; wakatangaza kufunga…..” (Yona
3:5)
Yesu Kristo alipofunga siku arobaini usiku na mchana, hakuamua kwa akili
yake. Alisikia wito wa Roho Mtakatifu toka ndani yake, kuwa anahitaji
kufunga.
Biblia inasema hivi, “Kisha Yesu alipandishwa na Roho Nyikani ili
ajaribiwe na ibilisi. Akafunga siku arobaini mchana na usiku” (Mathayo
4:12)
Yesu alipandishwa na Roho wa Mungu ili apate kufanya maombi ya kufunga,
yatakayomwandaa kwa makabiliano na Ibilisi. Yesu hakuambiwa na mtu
yeyote. Huo ulikuwa wito wa kutoka ndani yake kwa uongozi wa Roho wa
Mungu aliyekuwa ndani yake. Hata siku hizi wengi wanasikia wito wa namna
hii, wanatii na kufunga.
Kuna wito wa kutoka ndani na nje, ambao unawafikia watu na wanafanya
maombi ya kufunga “Ndipo nikaamuru kufunga, hapo penye mto Ahava,
ili tupate kujinyenyekeza mbele za Mungu na kutafuta kwake njia
iliyonyoka, kwa ajili yetu sisi wenyewe na kwa ajili ya watoto wetu, na
kwa mali yetu yote. Maana naliona haya kumwomba mfalme kikosi cha askari
na wapanda farasi, ili kutusaidia juu ya adui njiani, kwa maana tulikuwa
tumesema juu na mfalme, tukinena, Mkono wa Mungu u juu ya watu wote
wamtafutao, kuwatendea mema; bali uwezo wake na ghadhabu yake ni kinyume
cha wote wamwachao. Basi tukafunga, tukamsihi Mungu wetu kwa ajili ya
hayo; naye akatutakabali” (Ezra 8:21 – 23)
Anayesema maneno hayo ni Ezra, kuhani, “mwandishi wa torati ya
Mungu wa Mbinguni” (Ezra 7:21)
Ezra alikuwa na Roho wa Mungu, kama vile watumishi wote wa Mungu,
walivyokuwa naye wakati wa agano la kale.
Ezra alikuwa kiongozi, aliyekabiliwa na safari ambayo alikuwa
anahitajika kuwaongoza watu waifanye. Akasema, “Ndipo nikaamuru
kufunga ……maana naliona……..”
Kwa namna nyingine tunaweza kusema, “aliona kwanza ndipo akaamuru
kufunga.”
Alisikia kwanza wito wa ndani, ndipo wito wa nje ukajitokeza, ili yeye
na wenzie wajikabidhi mbele za Bwana kwa maombi ya kufunga.
Neno “nikaamuru” linasimama kwa ajili ya wito wa nje. Neno “naliona”
linasimama kwa ajili ya wito wa ndani.
Kitu kikubwa kinachojitokeza hapa ni kwamba maombi ya kufunga
yanaongozwa na Roho Mtakatifu. Ni maombi yanayosimamiwa na Mungu
mwenyewe kwa njia ya Roho wake. Hebu soma na kutafakari maneno yafuatayo:
“Mtumaini Bwana kwa moyo wako wote, Wala usizitegemee akili zako
mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, Naye atayanyosha mapito yako”
(Mithali 3:5,6) “Kwa
kuwa watu wote wanaoongozwa na Roho wa Mungu, hao ndio wana wa Mungu….Roho
mwenyewe hushuhudia pamoja na roho zetu ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu”
(Warumi 8:14,16).
“Yesu alipandishwa na Roho nyikani……akafunga siku arobaini
mchana na usiku” (Mathayo 4:1,2)
Wanafunzi wa Yohana Mbatizaji, walimwendea Yesu na kutaka kujua kwa nini
wanafunzi wake hawafungi wakati wao na Mafarisayo walikuwa wakifunga.
“Yesu akawaambia, walioalikwa arusini wawezaje kuomboleza, muda
Bwana arusi akiwapo pamoja nao? Lakini siku zitakuja watakapoondolewa
Bwana arusi; ndipo watakapofunga”. (Mathayo 9:15)
Kwa nini Yesu alisema hivyo?
Yesu alikuwa ana uhakika kuwa hawana haja ya kuacha kula na kunywa
wakati yeye bado yupo kimwili.
“Lakini yeye atakapokuja, huyo Roho wa Kweli atawaongoza awatie
kwenye kweli yote kwa maana hatanena kwa shauri lake mwenyewe, lakini
yote atakayoyasikia atayanena, na mambo yajayo, atawapasha habari yake”
(Yohana 16:13).
Yesu Kristo anatuambia kuwa kazi kubwa ya Roho Mtakatifu ni kututia
katika kweli yote. Kweli hiyo ni ipi?
Neno la Mungu ndiyo kweli tunayotakiwa kuifahamu. “Uwatakase kwa
ile kweli, neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17). Hii ni sehemu
ya sala ambayo Yesu aliwaombea wanafunzi wake popote walipo ulimwenguni.
Baada ya Yesu Kristo kupaa na Roho Mtakatifu, kuwashukia ndipo,
wanafunzi wake walipoanza kufunga. Kwa mfano tunasoma hivi:
“Basi hawa walipokuwa wakimfanyia Bwana Ibada ya kufunga, Roho
Mtakatifu akasema, nitengeeni Barnaba na Sauli kwa kazi ile niliyowaitia.
Ndipo wakiisha kufunga na kuomba, wakaweka mikono yao juu yao,
wakawaacha waende zao” (Matendo ya Mitume 13:2,3) Tunauliza tena……Kwa nini mtu
inakubidi ufunge?
Kuna sababu nyingi, lakini zinaweza kujumulishwa katika maneno yafuatayo:.
Tunafanya maombi ya kufunga, ili tupate “kujinyenyekeza mbele za
Mungu na kutafuta kwake njia iliyonyooka kwa ajili yetu sisi wenyewe na
kwa ajili ya watoto wetu, na kwa mali yetu yote” (Ezra 8:21)
Duniani tumo safarini lengo letu ni kufika mbinguni kwa Mungu kwenye
makao ya milele. Kila wakati tunakuwa na haja ya kuyafahamu mapenzi ya
Mungu juu ya maisha yetu ili tupite katika njia iliyonyooka. Mapenzi ya
Mungu tunayapata katika Biblia, ambayo ni neno la Mungu kwa wanadamu.
Yesu Kristo alisema, “Basi mimi nikienda na kuwaandalia mahali,
nitakuja tena niwakaribishe kwangu, ili nilipo mimi, nanyi mwepo. Nami
niendako mwajua njia. Tomaso akamwambia, Bwana, sisi hatujui uendako;
nasi twaijuaje njia? Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia na kweli, na uzima;
mtu haji kwa baba, ila kwa njia ya mimi” (Yohana 14:3-6)
Yesu ni “njia iliyonyooka” tunayoitafuta tunapofanya maombi
ya kufunga.
Sasa unaweza kuelewa kwa nini Yesu alisema wanafunzi wake hawawezi
kufunga wakati yeye yupo kimwili. Ni kwa sababu yeye alikuwa Njia yao
iliyonyooka. Hawakuhitaji kufunga ili wamuone au kumuuliza wafanye
nini.Yeye Kristo alikuwa pamoja nao, akiwaongoza, akiwafundisha,
akiwaonya na kuwaagiza.
Hawakuwa na haja ya kuacha kula na kunywa wakati Yesu yupo pamoja nao.
Katika torati ya Musa kufunga ilikuwa ni Lazima – ni sheria. Lakini
sisi tulio ndani ya Kristo hatufungwi na Sheria (Warumi 8:1-4).
Wanafunzi wa Yesu hawakufungwa na Sheria hasa Yesu alipokuwa pamoja nao.
Wanafunzi wa Yohana na Mafarisayo walikuwa bado chini ya sheria ndiyo
maana iliwabidi wafunge.
Baada ya Yesu Kristo kupaa, Roho Mtakatifu alichukua nafasi ya Kristo
ndani ya wanafunzi. Roho Mtakatifu anaongoza (Wagalatia 5:16,18, 25),
anafundisha (Yohana 16:13) anaonya (Ufunuo 2:7,11,17,29), na anaagiza (Ufunuo
22:17)
Roho Mtakatifu peke yake ndiye chanzo cha wito wa kufunga katika
Kanisa la Kristo na siyo sheria. Lakini utaona watu wengi wanafanya
maombi ya kufunga kwa sababu wamesikia au wameona au wameambiwa na watu
juu ya kufunga. Na kwa sababu hiyo wanakuta wanajitesa muda mrefu bila
kula wala kunywa na maombi yasijibiwe. Wengi wanafanya maombi ya kufunga
kimazoea tu bila ya kuongozwa na Roho Mtakatifu. Matokeo yake ni
kutokujibiwa na Mungu.
Biblia inakataza watu kutegemea akili zao wenyewe na kuwategemea
binadamu wengine katika safari hii ya Mbinguni (Mithali 3:5,6).
Mtegemee Roho Mtakatifu peke yake ambaye atakufunulia Yesu alivyo katika
maandiko. Na Yesu ni Njia unayoitafuta ili kutatua tatizo ulilo nalo. Lengo Letu
Lengo letu ni kuona ya kuwa kila mtu anayemjua Yesu kama Bwana na
Mwokozi wake – anaongonzwa na Roho Mtakatifu katika kila jambo
kufuatana na Warumi 8:14. Hii ni pamoja na maombi yanayohusisha kufunga
pia. Maombi ya kufunga yanafaida kubwa ikiwa yatafanyika kwa kusudi la
Mungu na kwa uongozi wa Roho Mtakatifu.
Kwa hiyo jitahidi kusoma biblia kwa makini ili upate kujifunza zaidi juu
ya jambo hili. Tunaamini Roho Mtakatifu atakuonyesha mambo mengi –
sisi tulichotaka katika waraka huu ni kuchokoza fikra zako ili
kulitazama jambo hili la maombi ya kufunga kwa jicho la neno la Mungu na
si kwa jicho la mazoea. Kwa mfano:
Tuzidi kuombeana ni sisi katika utumishi wa Kristo, Christopher na Diana Mwakasege |
|