Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
BARUA ZA MWEZI


B
arua ya Mwezi Januari 2003 

ANACHOFANYA MUNGU AKITUMIA SEMINA ZA NENO LA
 MUNGU KWA NJIA YA RADIO

Salamu katika Jina la Yesu,

            Mwaka 1985 Mungu alisema na sisi mambo mengi yaliyokuwa yanahusu huduma aliyokuwa ametupa na kutupangia. Kati ya mambo hayo ilikuwa ni juu ya huduma hiyo kwamba ataitumia “kuiponya nchi yetu”. Wakati huo hatukuelewa maana yake nini maneno hayo, na ni kwa jinsi gani yatatimizwa. Na isitoshe tulikuwa hata bado hatujaanza semina hizi tunazofanya sehemu mbalimbali katika miaka hii ya sasa. Jambo tulilolifanya ni kuendelea kuomba.

            Lakini siku moja tulipokuwa tukisoma biblia tulikutana na mstari huu:

“Wakamlilia Bwana katika dhiki zao, Akawaponya na shida zao. Hulituma Neno lake, huwaponya; huwatoa katika maangamizo yao” (Zaburi 107:19,20)

            Kwa hiyo tulijua ya kuwa Mungu ataitumia huduma aliyotupa kuiponya nchi yetu kwa kutumia Neno alilotupa na analotupa kulifundisha.

            Mwaka 2001 mwezi wa nane – ukurasa mpya ulifunguka katika huduma hii ya kufundisha neno la Mungu – wakati tulipofunguliwa mlango wa kuanza kutangaza mafundisho ya neno kwa njia ya Radio Sauti ya Injili – Moshi. Wakati huo matangazo yake yalikuwa yanaifikia mikoa ya Kilimanjaro na Arusha tu – na kwa sasa mkoa wa Tanga umeongezeka. Tunafundisha kila Jumamosi na Jumapili saa 3 had saa 4 usiku.

            Mwezi wa Tisa mwaka 2001, kanisa Katoliki Jimbo la Shinyanga lilitupa nafasi ya kurusha vipindi vyetu vya neno la Mungu kupitia radio yao ya ‘Radio Faraja”. Hadi sasa tunaendelea kurusha vipindi hivi mara mbili kila wiki siku ya Jumamosi na Jumapili kwa saa moja – moja (saa 3 hadi saa 4 usiku).

            Mwaka 2002 mwezi wa sita tukaanza kurusha vipindi vya semina ya Neno la Mungu kwa kutumia ‘Radio Free Africa’ (RFA). Kwa hiyo tangu wakati huo kila jumapili kwa saa moja (saa 12.30 – 1.30 jioni) tumekuwa hewani katika nchi sita ambazo RFA inasikika kwa kutumia mitambo yake ya (MW/AM) masafa ya kati – mitabendi 1377.

            Mwezi Januari 2003 tumeanza kurusha vipindi vya semina ya Neno la Mungu kupitia ‘Radio WAPO’ ya mjini Dar es Salaam, kila wiki siku ya Jumatano saa 3 hadi saa 4 usiku.

            Hakika huu ni ukurasa mpya ambao hatua kwa hatua unatuonyesha mwanzo wa udhihirisho wa maneno ambayo Mungu alisema nasi mwaka 1985 – juu ya kuiponya nchi yetu kwa kutumia neno analotupa kulifundisha. Maana kwa njia hii tunawafikia maelfu maelfu ya watu na neno la Mungu kila wiki.

-           Uponyaji wa Miili      -

            Tulipokuwa Moshi mjini kwa semina ya siku tisa mwezi Januari 2002, mtu mmoja alisimama kushuhudia alivyopona baada ya kupokea maombi kupitia vipindi vyetu vya Radio Sauti ya Injili (RSI). Alisema mbele ya umati wa maelfu ya watu waliokuwapo wakati huo ya kuwa yeye ni mlinzi wa usiku, na wikiendi moja alipokuwa akisikiliza kipindi chetu usiku wakati wa maombi aliweka mkono juu ya kichwa chake maana alikuwa anaumwa homa. Akasema baada ya maombi homa ilimwacha na akapona kabisa tangu saa ile. Na akaanza kuwaeleza walinzi wengine usiku huo huo mambo ambayo Yesu ameyatenda na kumponya kwa njia ya maombi katika RSI.

            Mwezi wa saba 2002, tulikuwa Iringa mjini kwenye semina ya siku sita. Wakati wa shuhuda, mama mmoja alisimama na kusema ya kuwa alipona wakati wa maombi ya wagonjwa kupitia kipindi chetu cha RFA kila Jumapili jioni. Alisema kwanza hakuamini ya kuwa anaweza kupona, lakini wakati wa maombi aliweka mkono wake kwenye kiuno upande wa kulia mahali ambapo amekuwa na maumivu kwa muda mrefu sana. Alishangaa sana na kumshukuru Mungu baada ya kuona amepona na maumivu kutoweka mara tu baada ya maombi hayo ya radioni tunayoyafanya katika kipindi hicho kila mwisho wa mafundisho.

            Mwezi Novemba 2002 tulipokuwa na semina ya siku nane Arusha Mjini tulipokea shuhuda zingine zaidi. Kwa mfano, mama mmoja aliyekuwa ametoka Moshi Mjini na kuja Arusha kwa ajili ya semina, alishuhudia mbele ya umati wa watu zaidi ya elfu kumi waliokuwapo hapo. Huyu mama alisema alikuwa ameugua ugonjwa wa saratani (cancer) ya ulimi kiasi cha kushindwa kula vizuri na kuongea vizuri. Baada ya kulazwa hospitali mbalimbali bila mafanikio alirudishwa nyumbani kwao akiwa katika hali mbaya sana. Akasema siku moja alikuwa anasikiliza moja ya kipindi chetu cha radio kilichorushwa mwezi wa saba 2002 na kituo cha Radio Sauti ya Injili (Moshi). Wakati wa maombi, yaliyoambatana na somo lile na yeye alipokea uponyaji! Nyama iliyokuwa imeota katika ulimi ilikatika na kudondoka. Kuanzia hapo maumivu yalinyamaza na akapata nguvu. Alipokuwa anakuja Arusha kushuhudia, alikuwa bado anasumbuliwa na masikio kwani saratani hiyo ilimfanya asisikie pia vizuri. Lakini katika maombi ya wagonjwa katika semina hiyo ya Arusha – alipona masikio na akaondoka anasikia vizuri. Jina la Yesu liponyalo libarikiwe sana!

            Pia katika semina hiyo ya Arusha ya mwezi Novemba 2002 kijana mmoja alishuhudia jinsi Mungu alivyomponya ugonjwa wa ukimwi kwa kupitia maombi tuliyoomba katika kipindi kimojawapo cha mafundisho yetu kwa njia ya radio.

            Hebu sasa soma baadhi ya shuhuda zifuatazo tulizozipata kwa njia ya barua tunazopata kila siku. Lengo letu ni kwamba umshukuru Mungu pamoja nasi, na pia utiwe moyo katika kuendelea kutusaidia katika kuifikisha huduma ya neno la Mungu kwa watu kwa kutumia radio mbalimbali hapa nchini.

Kutoka Geita (Mwanza)

Ndugu …. Bwana Asifiwe …….

Awali ya yote ningependa kukupongeza kwanza wewe kwa kazi nzuri sana unayoifanya ya kuhubiri watu kwa njia ya redio. Pili, ningependa kuwapongeza wafanyakazi wa Radio Free Africa kwa kupeperusha matangazo ya mahubiri redioni.

            Mimi binafsi nimependezwa sana na mahubiri yako niliyoyasikia mara tatu mfululizo tarehe 6/10, 13/10 na 20/10 na bado ukasema tutakuwa tena pamoja endapo Mungu atatujalia Jumapili ijayo. Nami bado nasubiri ili niweze kupata zaidi na zaidi kuhusu neno la Mungu.

            Mahubiri yako, ndugu, yamenifurahisha sana na kuniingia sana; lakini nimeona nimepungukiwa kiasi kwani sijui ulianza lini na utaendelea hadi lini. Nimeona ni vyema endapo kuna utaratibu wa kupata kanda za mahubiri hayo, basi itakuwa vyema zaidi kama nitazipata ili niweze kufaidika vizuri zaidi na kwa karibu zaidi …..

Kutoka Singida

….Bwana Yesu Asifiwe sana.

            Ubarikiwe na huduma unayoitoa ya Neno kwa njia ya redio. Mimi nina shida kubwa sana ya kiroho ambayo inahitaji maombi ya hali ya juu sana. Maana ni heri uugue mwili na ufe kulikoni kuugua dhambi; pia ni bora ufarakane na wafalme wa dunia hii kulikoni kufarakana na ufalme wa Mungu …. Shida yangu ni hii …….. Niliwahi kumwomba Mungu anipe kazi kwa kufunga na kuomba, na baada ya miaka mitatu nikapata kazi. Baada ya kuanza hiyo kazi mwaka 1998 nilifunga na kuomba kwa siku 7 (saba) ili Bwana anisaidie nisife kiroho na anieleze kusudi la kuniweka hapo kazini lakini hakunijibu. Nikaomba na kufunga tena kwa siku 21, lakini sikupata jibu. Nikaomba tena na kufunga kwa siku 40, lakini pia sikupata jibu. Kwa kweli nilikata tamaa nikajua Bwana hayuko nami tena, lakini nikiwa katika kuomba nilisikia unahubiri kwa njia ya Radio Free Africa – nilitubu upya. Lakini bado sina amani, nahitaji maombi – sina tumaini, biblia nashindwa kusoma, natamani niwe kama mwanzo …..

Kutoka Mtwara

Kwako Mtumishi wa Mungu,

            Nia ya barua hii ni kutaka kukufahamisha ya kwamba nami nimeokoka nampenda Yesu Kristo kama Bwana na Mwokozi wa maisha yangu. Nilifurahi sana baada ya kusikia injili inahubiriwa kwa njia ya Radio Free Africa na Mungu akikutumia kama chombo. Hii inaonyesha jinsi injili inavyohubiriwa kwa njia ya pekee na hata watu wa vijijini wanaweza sasa kusikia injili ya Yesu Kristo kwa urahisi – kwa hilo Mungu akubariki sana.

            Baada ya kusikia mahubiri yako kwa njia ya redio nilikuwa nipo wilaya moja nikifanya kazi za kutafuta maisha. Baada ya muda walikuja watu wawili kunitembelea na ikabidi na wao wasikilize hiyo injili iliyo kamili ya Yesu Kristo. Watu hawa walikuwa wapagani wasioamini habari za Yesu Kristo. Baada ya kusikia, walipenda wapate mafundisho kwa njia ya posta kutoka kwako ikiwa ni pamoja na kanda zenye mafundisho na masomo ya vitabu.

            Kwa jambo hili namshukuru Mungu kwa sababu anataka kuwaokoa watu kwa njia kama hii. Tunatumaini ya kwamba watu watazidi kufunguka kwa kupitia mtazamo huu ……..

Kutoka Nyanza, Kenya

….. Kusudi la waraka huu ni kuwa ningependa kukujulisha kwamba huduma ya kufundisha “Neno” la Mungu kupitia ‘Radio Free Africa’ inatufikia vizuri hapa mkoani ‘Nyanza – Kenya’, isipokuwa wakati mwingine mawimbi hututatiza tusisikie vizuri. Kwa sababu hiyo ninamshukuru Mungu kwa kukupa maono hayo ya kurekodi kanda za mahubiri, ili yaweze kuwafikia wale ambao hawaipati ‘Radio Free Africa’ kwa wepesi. Shukrani kwa maono hayo.

            Mimi nimejaribu kuwafahamisha wachungaji na watumishi wa Mungu kuhusu mafundisho hayo ya kila Jumapili jioni tunayopata kupitia RFA, na watu wote hao wanashuhuda mbalimbali ya miujiza ambayo Bwana Yesu huitenda wakati unapoomba maombi ya uponyaji na sala ya toba. Mungu aibariki huduma hii ienee “kotekote”

Kutoka Geita, Mwanza

            Ninayofuraha kubwa sana kuweza kuandika kipande hiki cha barua, ili niweze kutoa shukrani na kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa mahubiri yako kwa njia ya ‘Radio Free Africa’ inayosikika kila Jumapili jioni. Ukweli ninafarijika sana kwa mahubiri hayo.

            Mungu azidi kukulinda na kukubariki ili uzidi kutulisha neno lake japo hata kwa njia hii ya redio. Binafsi nimebarikiwa sana na kipindi hiki.

            Pia, nawashukuru wamiliki wa redio hii ya RFA kwa kukupatia kipindi hicho. Niliguswa sana na mahubiri ya tarehe 25 Agosti 2002 ambayo yalikuwa yanahusu ‘Kuguswa mara ya Pili na Bwana Yesu …..’

Kutoka Masasi

            Nakusalimu katika Jina la Bwana Yesu,

            Tunashukuru kuwa tunapata Neno la Mungu kupitia ‘Radio Free Africa’ kila Jumapili kuanzia saa 12:30 jioni.

            Namshukuru Mungu ya kuwa nilikuwa naumwa macho ‘vikope’ – wakati wa kipindi cha maombezi unayoomba redioni mwisho wa kipindi niliweka vidole vyangu kwenye macho na nimepokea uponyaji!

            Tunaomba njia ya kuweza kupata kanda zako, kwa kweli tunahitaji sana! Maana masomo hayo ni ya manufaa sana kwetu.

Mwisho

            Hizi ni baadhi tu ya shuhuda nyingi ambazo tumekuwa tukizipata kwa njia ya barua. Tumekushirikisha ili

(i)       Uzidi kumshukuru Mungu pamoja nasi kwa ajili ya mambo anayofanya kwa kutumia vipindi hivi vya mafundisho katika redio;

(ii)      Uzidi kuomba na kutuombea mafanikio zaidi katika huduma hii;

(iii)      Uzidi kutiwa moyo zaidi wa kutoa mchango wako wa kifedha unaotusaidia sana kulipia gharama za vipindi hivi redioni. Kwa sasa tunalipa wastani wa Shs. 600,000 kila wiki au shs. Millioni 30 kwa mwaka.

Tuzidi kuombeana ili tuzidi kudumu katika Bwana, na tuzidi kuifanya kazi yake kwa ufanisi zaidi chini ya uongozi wa Roho Mtakatifu.

ni sisi katika utumishi wa Kristo,

Christopher na Diana Mwakasege

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.