Barua ya Mwezi wa Machi 2003
UNAFANYAJE MUNGU ANAPOFANYA
MAKUBWA KULIKO ULIVYOTEGEMEA?
Salamu
katika Jina la Yesu Kristo;
Ndiyo kwanza tumemaliza semina ya siku nane iliyofanyika Arusha tarehe
16 – 23 Februari 2003 tuliyoifanya katika viwanja vya shule ya
sekondari ya Arusha – Meru – ndani ya hema. Mungu amefanya mambo
makubwa kuliko mawazo yetu yalivyotegemea. Imeandikwa katika kitabu cha
Waefeso 3:20,21 ya kuwa:
“Basi
atukuzwe yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote
tuyaombayo au tuyawazayo, kwa kadri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu;
naam, atukuzwe katika kanisa na katika Kristo Yesu hata
vizazi vyote vya milele na milele. Amina”
Tunaamini Mtume Paulo aliongozwa na Roho wa Mungu kuandika maneno haya
baada ya kuona Mungu amemfanyia mambo makubwa mno kuliko yote
aliyoyaomba au aliyoyawaza! Ndivyo yalivyotokea katika siku nane za
semina ya Arusha – Mungu amefanya mambo makubwa mno kuliko tulivyoomba
au tulivyowaza! Paulo akaandika, “Basi atukuzwe yeye …..”
Kwa hiyo
Na Sisi tunamtukuza Yesu!
Sisi tunamtukuza Mungu katika Yesu Kristo ambaye ametufanyia mambo
makubwa sana wakati wa semina. Si rahisi kukueleza yote kwa jinsi
yalivyo mengi, lakini tutajitahidi kukueleza mambo kadhaa. Nia yetu ya
kukueleza haya yote ni ili na wewe upate kumtukuza Mungu pamoja nasi!
Lakini pia upate kujua ya kuwa kama umekuwa ukituombea basi Mungu
amejibu maombi yako. Kama umekuwa ukimtolea Mungu sadaka kutusaidia
kuifanya kazi hii ya Mungu, basi ujue katika ulimwengu wa roho ulikuwa
pamoja nasi katika semina hiyo tukihudumu pamoja. Na Mungu wetu
atakujaza kila unachokihitaji kwa kadri ya utajiri wake “katika
utukufu, ndani ya Kristo Yesu” (Wafilipi 4:19)
Ishara ya mambo
mazuri mbele!
Siku ya kwanza ya semina kulizuka ghafula upepo na mvua
kubwa ambayo kwa muda mfupi iliharibu baadhi ya mahema tuliyokuwa
tumeyafunga. Watu kadhaa wakanyeshewa na mvua. Lakini watu wakamwomba
Mungu kwa pamoja na kumkemea shetani kwa nguvu – na baada ya muda
mfupi tu upepo ulitulia na mvua ikanyamaza.
Kwetu sisi hii ilikuwa ishara. Ishara ya mambo mazuri yaliyokuwa mbele
yetu katika semina hiyo. Tulijua shetani ameona ushindi tuliopewa na
Yesu katika semina na hakufurahi. Kwa hiyo alitaka kuivuruga semina
tokea siku ya kwanza. Lakini Mungu akatupigania – hila za shetani
zikakwama. Siku hiyo semina iliendelea na watu wakazidi kumiminika kuja
kwenye kiwanja tulichofanyia semina. Neno likafundishwa, wagonjwa
wakaponywa wengi na mamia kwa mamia ya watu wakaokoka siku hiyo hiyo ya
kwanza ya semina
Miujiza yathibitisha
Yesu Yuko hai!
Katika Yohana 20:30,31 imeandikwa ya kuwa; “Basi kuna
ishara nyingine nyingi alizozifanya Yesu mbele ya wanafunzi wake,
zisizoandikwa katika kitabu hiki. Lakini hizi zimeandikwa; ili mpate
kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe
na uzima kwa jina lake”
Mungu anapolithibitisha neno lake kwa ishara na miujiza – jina la Yesu
hutukuzwa sana. Kwa hiyo katika semina hizi tunazofanya sehemu ya
shuhuda ni muhimu sana. Tatizo tunaloliona ni kwamba muda tunaokuwa
naona unakuwa hautoshi kumpa nafasi kila mtu aliyepona kutoa ushuhuda
wake. Hata katika waraka huu tutakushirikisha shuhuda chache ili kila
mtu apate kujua ya kuwa Yesu Kristo yuko hai, tena ya kwamba ndiye
Kristo, Mwana wa Mungu.
Watu waliojitokeza kushuhudia matendo makuu ya Mungu katika maisha,
wengine walikuwa wamepokea miujiza yao katika semina za mwaka jana;
wengine walipona kupitia kwenye vipindi vyetu vya radio; na wengine
walipona katika semina hii ya mwezi Februari 2003.
Kwa mfano; kuna mama mmoja alishuhudia ya kuwa alikuwa anaumwa na ukimwi
na Mungu amemponya. Tulipomuuliza ya kuwa amejuaje ya kuwa amepona, -
akasema ni kwa sababu dalili zote za ugonjwa wa ukimwi alizokuwa nazo
mwilini zimeondoka baada ya maombi. Tukamshukuru Mungu pamoja naye na
kumshauri aende hospitalini akapime tena – ili vipimo vya hospitali
vikithibitisha uponyaji – wengine wapate kumwamini Yesu na kumfuata.
Kuna mwanamke mwingine aliyekuwa na shida ya ‘kutokwa damu’ kwa muda
wa miaka mitatu mfululizo, alishuhudia jinsi Mungu alivyomponya katika
semina ya Novemba 2002. Na tangu wakati huo ni mzima na shida hiyo
haijamrudia tena!
Kijana mmoja alieleza mbele ya maelfu ya watu jinsi mguu wake wa kushoto
ulivyokuwa na matatizo; na jinsi alivyokuwa amekwenda hospitali kubwa za
Shinyanga, Mwanza, Musoma na Arusha bila kufanikiwa kupona. Na alikuwa
anajiandaa kwenda hospitali ya KCMC ya Moshi aliposikia habari za semina
na akaamua kuja. Matokeo yake Mungu alimponya. Akiwa madhabahuni akasema
ingawa mguu wake huo wa kushoto ulikuwa umepona, bado alikuwa anatembea
kwa shida maana ulikuwa mfupi. Kwa hiyo tukamwomba Mungu ili mguu huo
mfupi ukue na kuongezeka urefu. Mbele ya maelfu ya watu tuliona mguu
ukitingishwa kwa nguvu za Mungu na kukua hadi kufikia urefu wa kufanana
na ule mwingine wa kulia uliokuwa mzima. Maelfu ya watu walioshuhudia
muujiza huo walishangilia na kumtukuza Mungu sana.
Kuna mama mwingine alishuhudia Mungu alivyomponya katika semina hiyo
hali ya kupoteza fahamu na kukosa nguvu upande wake wa kushoto kutoka na
ugonjwa wa ‘stroke’. Hiyo ‘stroke’ ilifanya mdomo wake upindie
upande mmoja alipokuwa anaongea na jicho la kushoto kushindwa kufunguka
na kutokuwa nafahamu akiguswa upande huo wa kushoto. Na alikuwa
anatembea kwa shida sana. Lakini Mungu alivyo mwingi wa rehema akamponya
katika semina hii na akaweza kuona tena vizuri, mdomo ukarudi mahali
pake, na fahamu zikarudi katika upande wake wa kushoto – na akaweza
kutembea vizuri.
Shuhuda zilikuwa nyingi sana. Kuna walioshuhudia mifupa iliyounga na
kupona; kuna waliopona matatizo ya macho, na magonjwa mwengine mengi.
Sisi tunamtukuza Mungu sana kwa uponyaji huu wa ajabu. Jina la Yesu
libarikiwe milele!
Waliojazwa Roho Mtakatifu
ni wengi sana!
Katika eneo hili Bwana Yesu alifanya mambo ya ajabu sana. Si tu kwamba
aliwajaza Roho Mtakatifu wale waliokuwa na kiu naye; bali hata wale
ambao walikuwa wanapinga habari za kunena kwa lugha mpya; na hata wale
ambao hawakujua kilichokuwa kinaendelea.
Kuna watu waliotueleza jinsi walivyosubiri kwa hamu wapate ‘Double
Dose’ ya upako lakini hawakufanikiwa. Walipokuwa wakirudi nyumbani
kwao wakiwa ndani ya ‘taxi’ walianza kusimuliana habari za yule
kijana aliyepona mguu na wakauona ukikua. Wakiwa katika kuongea juu ya
habari hiyo wakataja jina la Yesu – na mara hiyo hiyo wakashukiwa na
nguvu za Mungu na kuanza kuomba hadi walipofikishwa nyumbani, kwao, na
hata hivyo mmoja wao alishindwa kutembea maana alipotelemka tu toka
kwenye ‘taxi’ alianguka chini na kuendelea kuomba. Watu wengi
wakawazunguka na kushangaa kulikoni! Pamoja na kwamba Yesu hakuwapa
‘Double Dose’ ya upako pale uwanjani, aliamua kuwapa ndani ya
‘taxi’!
Mama mwingine alishuhudia mbele ya maelfu ya watu kuwa alikuwa anapinga
habari za kunena kwa lugha, na kwamba wale waliokuwa wanadai wananena
kwa lugha mpya walikuwa wakijifanya tu. Lakini Mungu aliamua
kumthibitishia jinsi alivyokosea katika kuwaza kwake! Alisimulia ya kuwa
alikuwa amekaa kwenye kiti wakati wa somo likiendelea alishitukia
ameanza kunena kwa lugha mpya! Na wakati wa maombi mwishoni mwa somo
alisogea na yeye mbele ya jukwaa, nguvu zikamshukia na kunena tena kwa
lugha mpya lakini pia na kucheka sana. Aliondoka uwanjani kwenda
nyumbani na kupanda basi huku akiendelea kucheka katika Roho Mtakatifu.
Tangu siku hiyo ubishi ulikwisha na ana uhakika wanaonena kwa lugha
hawajifanya – bali ni halisi na ni kweli tupu!
Mama mwingine alitusimulia jinsi alivyojikuta anazungumza ‘lugha
asiyoijua’ akiwa amekaa kwenye kiti wakati wa maombi ya ujazo wa Roho
Mtakatifu. Hakujua ni kitu gani kimetokea hadi tulipokutana naye baada
ya semina na kutueleza kulichotokea. Tukamwambia ya kuwa kilichotokea ni
kwamba alijazwa Roho Mtakatifu na ishara iliyotokea kuthibitisha hili ni
yeye kunena kwa lugha mpya. Alipopata ufafanuzi huo alifurahi sana. Na
sisi tunamtukuza Mungu pamoja naye! Sifa ni kwa Yesu Kristo!
Maelfu ya watu walijazwa Roho Mtakatifu hata wengine kushindwa kutembea
na kubebwa kwenda nyumbani; na wengine kushindwa hata kuongea kwa muda!
Laiti ungekuwepo na uone jinsi Mungu alivyotembelea na kuwajaza upako wa
Roho Mtakatifu vijana!
Utayari wa kuokoka ulikuwa mkubwa!
Watu walivyokuwa wanaokoka ‘kirahisi’ utadhani walikuwa wanatoka
nyumbani wakiwa wamepania kuokoka! Maana ilikuwa haijalishi unaita watu
kuokoka wakati gani, kabla au baada ya neno – walikuwa wanaokoka tena
kwa uwingi sana. Kwa siku nane zote ni wastani wa watu 9500 waliokoka!
Siku zingine walikuwa wanaokoka watu wengi kiasi ambacho wahudumu
hawakuweza kuwaandika wote. Lakini tuna uhakika mbinguni wana kumbukumbu
nzuri zaidi ya majina ya wote waliookoka katika semina hiyo!
Siku moja baba mmoja ambaye alikuwa hajaokoka alielezea ushuhuda
uliofanya watu wengi waokoke pamoja na yeye mwenyewe! Alisema siku moja
aliamua ‘kunyata’ usiku ili asimwamshe mke wake aliyekuwa amelala, -
akachukua mkanda wa video wa moja ya semina zetu na kwenda sebuleni
kuuangalia. Wakati wa maombi ulipofika katika video, naye akasimama na
kuweka mkono juu ya kifua chake – kwani alikuwa anasumbuliwa na
ugonjwa wa moyo na wa shinikizo la damu. Baada ya maombi hayo ya kwenye
video akapona! Kwa hiyo wakati wa semina akaamua kutoa ushuhuda wa
uponyaji huo, na kuomba aombewe aokoke pia! Watu waliosikia
wakashangilia kwa nguvu, na sisi tukakaribisha watu wengine ambao
hawajaokoka waje mbele ili waombewe na waokoke pamoja naye. Mamia ya
watu walijitokeza kuokoka! Mke wa baba huyo ambaye yeye alikuwa ameokoka
alikuja mbele kushuhudia kwa macho yake na masikio mume wake akiokoka!
Jina la Yesu lihimidiwe milele!
Mwisho
Tunatamani tuendelee kukueleza mambo mengi zaidi ambayo Bwana aliyofanya
– lakini tunaona tuliyokuandikia hapa yanatosha kwa leo. Watu
waliohudhuria walikuwa wengi sana – si chini ya 10,000 kila siku. Siku
ya mwisho wa semina walikuwa wengi zaidi kiasi kama 20,000!
Tuzidi kuombeana. Ni kweli Mungu amefanya kuliko tulivyokuwa tumetegemea.
Sifa na utukufu ni wake. Semina zinazofuatana ni Dar es Salaam tarehe 1
–9 Machi 2003 (Kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee) na tarehe 18 – 24
Machi 2003 Tanga mjini. Tuombee ili Mungu akajitukuze tena. Ukiweza
kufika kwenye semina hizo karibu sana tushirikiane baraka za Mungu.
ni sisi katika utumishi wa Kristo,
Christopher
na Diana Mwakasege