Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma

Barua ya Mwezi Desemba 2004                                                            Kutoka kwa Christopher na Diana Mwakasege


Salamu za Krismas

KRISMASI HII JIFUNZE JAMBO TOKA KWA MARIAMU

Salamu katika Jina la Yesu.

Kila wakati tunaposoma habari za mambo mbalimbali yaliyotokea Yesu alipozaliwa huwa tunapata jambo au mambo ya kujifunza. Katika mwezi huu wa Disemba, hata wale ambao si wakristo wanafuatilia kwa karibu sherehe zinazoambatana na kuzaliwa kwa Yesu; bila kutafakari kwa undani juu ya ujumbe unaopatikana wakati tunapokumbuka kuzaliwa kwa Yesu.

Kwa mwaka huu tunataka tujifunze alichofanya Mariamu alipoambiwa juu ya kuzaliwa kwa Yesu duniani.

Mungu alimtuma Malaika Gabrieli kwa Mariamu kusema hivi: “Tazama, utachukua mimba  na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu” (Luka 1:31).

Hili lilikuwa neno la ahadi kwa Mariamu toka kwa Mungu. Mariamu akataka kujua jambo hili litatokeaje katika maisha yake; naye akamuuliza malaika, “Litakuwaje neno hili, maana sijui mume?” (Luka 1:34)

Malaika Gabrieli akamweleza Mariamu jinsi ambavyo nguvu za au upako wa Roho Mtakatifu utakavyohusika katika kuifanya hiyo ahadi ya Mungu ya kuzaliwa kwa Yesu katika maisha yake itakavyodhihirika katika maisha yake. Malaika Gabrieli akamwambia, “Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu” (Luka 1:35)

Mariamu aliposikia hayo alisema hivi: “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema” (Luka 1:38)

Hakuna neno lisilowezekana
kwa Mungu

Kabla Mariamu hajajibu alivyojibu, Malaika Gabrieli alimwambia ya kuwa;  “…. Hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu” (Luka 1: 37)

Mariamu aliambiwa hivi kwa sababu ndani ya moyo wake alikuwa anajiuliza kama jambo hilo linawezekana. Alijiuliza jambo hilo kwa sababu kibinadamu alikuwa ni bikira – hamjui mume kwa hiyo isingekuwa rahisi kupata mtoto!

Unaona kabisa ya kuwa alikuwa anatafakari juu ya upatikanaji wa ahadi au neno la Mungu kwake kwa jinsi ya kibinadamu. Katika kutafakari huko akagundua ya kuwa jambo hilo haliwezekani!

Hii ndio sababu iliyomfanya Malaika Gabrieli atoe ushuhuda kwanza juu jambo kama hilo lilivyotokea kwa Elizabeti aliyekuwa jamaa ya Mariamu ya Karibu. Na baada ya ushuhuda huo akasema yametokea hayo kwa Elizabeti; kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu (Luka 1:37)

Kwa kusema maneno hayo alitaka Mariamu pia alitazame jambo la kuipata ahadi yake ya kuzaliwa kwa Yesu – ya kuwa  litafanyika kwa msaada wa Mungu vile vile. Alitakiwa aone na akubali ya kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu.

Mariamu alipotambua hivyo akasema; “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema”. Nasi tunajua alipokea alichosema, maana baada ya miezi tisa, alizaa mtoto mwanamume, na jina lake akamwita Yesu.

Inawezekana Krismasi hii imekukuta katika hali ya subira – ukisubiri ahadi ya Mungu itimie kwako; - na inawezekana imechukua muda mrefu kutimia kwako.

Sisi tunataka tukuulize hivi; je! Umewahi kusema kama Mariamu alivyosema ya kuwa “na iwe kwangu kama ahadi ya Mungu inavyosema”?

Inawezekana unasita kusema namna hii kwa sababu unajaribu kufikiri ni kwa namna gani ahadi hiyo itatimia – na ukitafakari kibinadamu unaona haliwezekani kabisa.

Kumbuka hata Mariamu alifika mahali pa kuwaza namna hii. Kibinadamu ahadi aliyopewa isingewezekana kutimia.

Inawezekana unaumwa ugonjwa ambao kidaktari inaonekana huwezi kupona – lakini kumbuka ahadi ya Mungu juu ya uponyaji. Mungu atakuponya! Kwa nini? Kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu! Ni neno gani hilo lisilowezekana kwa Mungu? Ni neno lile la ahadi alilolisema katika biblia juu ya kutuponya magonjwa. Kwa mfano Marko 16:17,18; Mathayo 8:16,17, Kutoka 15:26; 1Petro 2:24.

Tunazungumza juu ya uponyaji kama mfano mmoja wapo tu. Lakini eneo lolote lile ambalo kibinadamu ni vigumu kuona ni kwa namna gani ahadi ya Mungu inaweza kutimia – linaweza kutazamwa kwa namna hii. Kwa nini? Kwa kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu!

Kama unaona tatizo kuamini hivi tafakari shuhuda mbalimbali Krismasi hii, zile ambazo zinaonyesha jinsi ambavyo Mungu amefanikisha jambo kama hilo hilo unalotaka lifanikiwe kwako. Kama hakuna shuhuda zo zote unazozijua – tafakari zilizomo katika biblia!

Tunaamini mwishoni utakubaliana na Malaika Gabrieli ya kuwa hakuna neno lisilowezekana kwa Mungu. Na ukifikia mawazo haya ndani yako ni rahisi kwako kusema kama Mariamu alivyosema ya kuwa “….. na iwe kwangu kama ulivyosema”

Kupokea ahadi za Mungu kuna
gharama zake – je uko
tayari kuzilipa?

Mariamu alipoamua kuipokea ahadi ya kuzaliwa kwa Yesu katika maisha yake alijua gharama ambazo zilikuwa zimeambatana na uamuzi huo; na alikuwa tayari kuzilipa.

Kuna  gharama kadhaa ambazo Mariamu alikuwa tayari kuzilipa ili tu aipate ahadi ya Mungu katika maisha yake.

Kwa mfano: Alikuwa tayari kulipokea neno aliloahidiwa pamoja na kwamba ubikira wake ungeharibika na angekupata uja uzito nje ya ndoa! Gharama ya matukio haya kwa msichana wakati huo ilikuwa kubwa – kwake mwenyewe na kwa ndugu na marafiki zake!

Lakini Mariamu akijua hilo bado alikubali kuipokea ahadi ya Mungu na neno la ahadi hiyo lijidhihirishe katika maisha yake.

·         Alikuwa tayari kumkosa mume wake mtarajiwa lakini alipate neno aliloahidiwa!

·         Alikuwa tayari kuharibu uhusiano wake na wazazi wake, ili mradi aipate ahadi aliyoahidiwa.

·         Alikuwa tayari kuharibu usichana wake na kuhama rika toka kwenye usichana kwenda kwenye umama. Kikawaida unapohama rika moja kwenda rika jingine hata marafiki wanabadilika! Lakini pamoja na hayo yote Mariamu alikuwa tayari kula gharama hiyo ili aipate ahadi ya Mungu iliyokuwa imesemwa kwa ajili yako.

Je! Wewe uko tayari kula gharama ya kiasi gani ili tu ahadi ya neno la Mungu litimie katika maisha yako?

Krisimas hii usitafakari tu baraka inayokuja kwa Yesu kuzaliwa katika maisha yako, na neno lake kudhihirishwa kwako; lakini pia tafakari gharama zinazoambatana na udhihirisho huo.

Tunakutakia sherehe njema. Tuzidi kuombeana.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.