Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma

Barua ya Mwezi Januari 2004                                                            Kutoka kwa Christopher na Diana Mwakasege


Unafanyaje matumizi yako yanapokuwa
makubwa kuliko kipato chako?

          Hiki ndicho kilichokuwa kichwa cha semina yetu ya mwisho ya mwaka 2003 tuliyoifanya Dar es Salaam tarehe 17 – 21 Disemba katika ukumbi wa PTA uliomo katika viwanja vya maonyesho ya Sabasaba.

          Hii ilikuwa mojawapo ya semina muhimu sana katika kujifunza biblia inavyofundisha juu ya uchumi na maisha yetu ya kila siku.

          Nia hasa ya semina hii katika kulenga somo hili ilikuwa ni kutaka kujua kama biblia ina ushauri wo wote juu ya tatizo hili ambalo linawasumbua watu wengi – wakristo hata ambao si wakristo. Mfululizo wa masomo hayo ulituonyesha ya kuwa biblia inao ushauri mzuri sana juu ya tatizo hili. Tuliangalia mambo mawili tu kwa sababu ya muda kuwa hautoshi – nayo ni haya:

  1. Jiwazie mwenyewe sawasawa na jinsi Mungu anavyokuwazia wewe juu ya mapato na matumizi yako ya kila siku.
  2. Tambua kipawa ambacho Mungu amekupa na uijue thamani yake ili ukitumie ipasavyo.

Maelfu ya watu waliohudhuria semina hiyo, ni mashahidi pamoja nasi katika yale ambayo Mungu aliyasema na kutufanyia katika semina hii.

          Tunamshukuru Mungu kwa ajili ya kila mtu ambaye amekuwa akitusaidia kwa kutuombea, kwa kutoa sadaka yake ya fedha au mali au muda wake – na tukaweza kuumaliza mwaka 2003 vizuri. Tunaamini utakuwa pamoja nasi tena mwaka 2004. Semina yetu ya kwanza inaanzia Moshi mjini tarehe 18 – 25 Januari 2004 itakayofanyika ndani ya hema katika Uwanja wa Mashujaa.

JIANDAE KUFANIKIWA….
….. ZAIDI SANA!

Salamu,

          Tunakusalimu katika Jina la Yesu Kristo, aliye Bwana na Mwokozi wa maisha yetu ya kila siku, na ya siku zote. Tunamshukuru Mungu aliyetupa nafasi hii tena, ili kuwasiliana na wewe kwa njia hii. Tuna uhakika ya kuwa unayasoma haya tuliyoyaandika kwa sababu Mungu amepanga hivyo – ili kile alichotuongoza kukiandika upate kukisoma! Kabla ya kukuletea ujumbe huu tunataka tukuambie ya kuwa semina yetu ya kwanza mwaka huu itakuwa tarehe 18-25 Januari 2004 pale Moshi mjini. Tuombee ili kusudi la Mungu litimie na Jina la Yesu litukuzwe.

Umeanzaje mwaka huu?

          Tunaamini kila mtu huwa anauanza mwaka mpya kwa staili yake, kufuatana na kile ambacho amekitafsiri juu ya kile ambacho anataka kukifanikisha katika mwaka huu mpya. Mwingine anaanza kwa kujiwekea malengo mapya, baada ya kutathmini mambo aliyoyafanya miaka ya nyuma. Mwingine anaweka malengo ya mbele bila kutathmini, wala kujali yaliyofanyika katika miaka iliyopita. Lakini pia kuna mtu mwingine haoni mabadiliko yo yote; maana kwake tofauti za miaka hazitofautishi umuhimu wa tofauti za siku zilizomo!

Mbinu za kufanikiwa – Kibiblia!

          Kati ya mambo ambayo sisi tulifanya mwanzoni kabisa mwa  mwaka, ni kumwomba Mungu apate kutupa neno lake katika biblia kwa ajili ya mwaka huu. Hili jambo tumekuwa tukimwomba Mungu karibu kila mwaka mpya kwa kipindi kirefu sasa.

          Tunaamini kile ambacho biblia inasema juu ya neno la Mungu – hasa linavyotujengea mahusiano yetu na Mungu. Kwa mfano, Mungu anapotupa neno lake kila mwaka – tunakuwa na uhakika ya kuwa:

  • Tukiliangalia hilo neno – tutakuwa tunaangalia mwelekeo wa mwaka huo kama vile Mungu anavyoangalia. Kwa sababu mungu anasema; “… kwa maana ninaliangalia neno langu, ili nilitimize” (Yeremia 1:12)
  • Tukifuata maelekezo ya hilo neno tutakuwa tunatembea katika mpango wake kwa mwaka huo – mpango wenye uhakika wa kufanikiwa. Kwa sababu Mungu amesema; “….ndivyo litakavyokuwa neno langu litokalo katika kinywa changu, halitanirudia bure, bali litatimiza mapenzi yangu, nalo litafanikiwa katika mambo yale niliyolituma” (Isaya 55:11)
  • Tukilifuata hilo neno katika maisha, Mungu atalithibitisha ya kuwa ni neno lake – na tena ya kuwa ni la kweli. Kwa sababu Mungu wetu hajabadilika “ni Yeye yule, jana, na leo, na hata milele” (Waebrania 13:8). Alichokifanya zamani kwa watu waliotembea na neno lake, anaweza kukifanya hata hivi leo. Maana imeandikwa katika kitabu cha Marko 16:20 ya kuwa, “Nao wale wakatoka, wakahubiri kotekote, Bwana akitenda kazi pamoja nao, na kulithibitisha lile neno kwa ishara zilizofuatana nalo”
  • Tena tunajua tukilifuata hilo neno analotupa kwa mwaka huo tunakuwa na uhakika wa mahali tunakoelekea au njia tutakayoipitia. Kwa sababu imeandikiwa, “neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia yangu” (Zaburi 119:105)

Pamoja na mambo haya tuliyokuambia hapa juu, zipo sababu nyingine nyingi zinazotufanya karibu kila mwaka tunajikuta tunaomba kwa Mungu atupe neno la kutembea nalo katika mwaka mpya. Lakini tunaamini sababu hizi tulizoziandika zinatosha kwa sasa kukufahamisha kwa nini tunaomba tunavyoomba kila mwanzoni mwa mwaka mpya. Lakini pia, jambo hili likutie changamoto ya wewe kuwa na maombi ya jinsi hii maana tunaamini ni jambo zuri.

     Kwa hiyo tulipofanya maombi haya tena mwanzoni mwa mwaka huu – Mungu alitujibu na kutupa mstari huu wa 3 Yohana 1:2, unaosema “Mpenzi, naomba ufanikiwe katika mambo yote, na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo”

     Sasa unaweza ukaelewa kilicho mbele yetu mwaka huu. Lakini kwa sababu ya nafasi ambayo Mungu ametupa katika jamii, tunajua ya kuwa Mungu akitupa neno la kutembea nalo halitugusi tu sisi peke yetu, lakini na wote wale ambao tunahusiana nao kwa namna moja au nyingine katika kulitafakari neno la  Mungu kwa njia mbalimbali kama semina, radio, video au kwa njia ya maandiko au kwa njia ya mazungumzo ya kawaida tu tunapokutana. Ndiyo maana tunakuambia “Jiandae kufanikiwa….zaidi sana!” Hii ni kwa sababu ikiwa ulikuwa hufanikiwi, basi mwaka huu mambo yataanza kubadilika na utaona mafanikio katika maeneo ambayo ulikuwa huoni mafanikio. Na kama ulikuwa unafanikiwa tayari katika maeneo mbalimbali ya maisha yako – basi jiandae kufanikiwa zaidi sana mwaka huu kuliko ulivyofanikiwa huko nyuma!

Mbinu za kufanikiwa – kibiblia!

     Si kila kufanikiwa anakofanikiwa mwanadamu kunatokana na uongozi wa Mungu huyu tunayemwabudu katika roho na kweli ndani ya Yesu Kristo. Mithali 1:32b inasema, “Na kufanikiwa kwao wapumbavu kutawaangamiza”.

 Mungu hawezi kukuongoza na ukafanikiwa kwa kufuata mapenzi yake na uongozi wake katika maisha yako – halafu akuangamize au akuache uangamie kwa mafanikio hayo hayo! La sivyo itakuwa lazima kuna mahali fulani katika maisha yako – kwa kujua au kwa kutokujua, utakuwa hujafuata utaratibu wake sawa sawa juu ya kufanikiwa huko. Maana Mungu haichanganyi baraka anayokupa na huzuni! Ndivyo ilivyoandikwa katika Mithali 10:22 ya kuwa “ Baraka ya Bwana hutajirisha, wala hachanganyi huzuni nayo!”

     Ndiyo maana katika biblia zimewekwa wazi mbinu za kufanikiwa – ambazo Mungu anataka tukizifuata – tuweze kuwa na mafanikio makubwa na mazuri – na si mafanikio yanayotufanya tuje tuangamie na kuukosa uzima wa milele. Baadhi ya mbinu hizo ni hizi zifuatazo:

  1. Lenga kuifanikisha nafsi yako KWANZA….

Hii ni kwa sababu kipimo au kiwango cha kufanikiwa kwako kinategemea kipimo au kiwango cha kufanikiwa cha nafsi yako katika eneo hilo. 3 Yohana 1:2 inatupa neno hilo anaposema “…ufanikiwe katika mambo yote, na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo”. Tafsiri nyingine za biblia zinaweka neno sahihi zaidi zinaposema “…kama vile nafsi yako ifanikiwavyo na si kama roho yako ifanikiwavyo!”

  1. Unapoisoma biblia usisome tu maneno yake na kuachia hapo!

Lakini fanya hivi zaidi:

    • Maneno uliyoyasoma – yasiondoke kinywani mwako au yaseme siku zote,
    • Maneno hayo yatafakari au yafikirie usiku na mchana,
    • Yaweke maneno hayo katika matendo, au yatekeleze katika maisha yako; na kitabu cha Yoshua 1:8 kinasema “…. Ndipo utakapoifanikisha njia yako, kisha ndipo utakapositawi sana!”

Ndani ya neno la Mungu utakuta umuhimu wa kutii neno katika kufanikiwa (Kumbukumbu ya Torati 28:1-14); utakuta pia umuhimu wa umoja katika kupokea baraka (Zaburi 133:1-3); utakuta pia biblia inakuonyesha umuhimu wa kuomba kwa lengo la kumtafuta Mungu ili akufanikishe (2 Mambo ya Nyakati 26:5); na pia utaona biblia inakuonya usije ukamsahau Mungu utakapokuwa umefanikiwa, maana mafanikio hayo yatapukutika mara moja (Kumbukumbu ya Torati 8:18-20 na Yeremia 22:21)

Mwisho

          Tunakutakia mafanikio mema na makubwa zaidi mwaka huu kuliko ulivyowahi kufanikiwa. Tuzidi kuombeana.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.