UMOJA WA ROHO HAUTOSHI
BILA
UMOJA WA IMANI
Salamu katika Jina
la Yesu.
Katika kitabu cha
Waefeso 4: 3 tunasoma habari za “Umoja wa Roho” na katika Waefeso
4: 13 tunasoma habari za “Umoja wa Imani”. Kwa hiyo katika kanisa
tunahitaji si tu umoja wa Roho bali umoja wa Roho pamoja na umoja wa
imani. Watumishi mbalimbali tunahitaji kushirikiana ili kuimarisha umoja
wa imani.
Imeandikwa katika
kitabu cha Waebrania sura ya kumi na moja na mstari wa kwanza kuwa; "
Basi imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo
yasiyoonekana."
Na pia tuna soma
katika Warumi 10:17 kuwa:
"Basi imani,
chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo".
Kwa kutumia maana
ya neno imani kama tulivyosoma hapa juu tunaona ya kuwa umoja wa imani
ni umoja wa 'kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo na bayana ya mambo
yasiyoonekana.'
Ni kazi ya Mtume,
manabii, wainjilisti, wachungaji na waalimu wakifanya kazi wote kwa
kushirikiana, kutufikisha wakristo wote katika umoja wa 'kuwa na
hakika ya mambo yatarajiwayo, na bayana ya mambo yasi yoonekana.'
Kuna kuwa na
tofauti kati ya wakristo juu ya hakika ya mambo yatarajiwayo, na tofauti
yakuyangalia mambo yasiyoonekana, matokeo yake ni ukosefu wa umoja imani.
Na chanzo cha
umoja wa imani ya kikristo ni kusikia na huku huja kwa
neno la Kristo.
lkiwa
tunafundishwa neno la Kristo na Roho mmoja wote, na kulisikia wote,
tutakuwa na imani ya aina moja; na Roho huyo aliyetufundisha neno la
Kristo hilo atatufikisha katika umoja wa imani.
Huwa inashangaza
kuona kuwa wakristo wa madhehebu mbali mbali ulimwenguni, wanatumia
Biblia ya aina moja wote, na wanadai wote kuongozwa na Roho wa Mungu,
lakini wanapingana juu ya tafsiri ya maandiko. Ni lazima pana tatizo
katika kuitafsiri na kuifafanua Biblia.
Siku hizi ingawa
wengi wanaitwa wakristo utaona wazi ya kuwa umoja wa imani ya kikristo
KIMATENDO haupo. Na hii imetokana na tofauti ya mafundisho yanayotolewa
ya neno la Kristo.
Na ndipo hapa
tunahitaji huduma zote zifanye kazi. Kila mtumishi wa Kristo awe mtume
au nabii au mwinjilisti, au mchungaji au mwalimu amepewa sehemu tu ya
neno la Kristo. Huduma zote zikifanya kazi tunapata sehemu tu ya neno la
Kristo.
Na ili tuwe na
umoja wa imani tunalihitaji neno la Kristo lote na lililo kamilifu.
Tukipata sehemu tu ya neno la Kristo tunapata ugonjwa wa utapiamlo wa
Kiroho, hasara yake ni kukosa Umoja wa imani kati ya wakristo.
Na Roho wa Mungu
anawaunganisha wakristo katika umoja wa imani,
kwa kulitumia neno
la Kristo.
Na tujifunze toka
kwa Yesu Kristo alipowagawia wanafunzi wake mkate;
Imeandikwa: "Akatwaa
mkate, akashukuru, akaumega, akawapa akisema, Huu ndio mwili wangu
unaotolewa kwa ajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu." (Luka
22: 19)
Biblia haisemi
alitwaa 'Mikate' bali alitwaa 'Mkate'.
Hii ina maana ni
mkate mmoja tu ambao aliugawanya vipande kumi na
vitatu na kuwapa
wanafunzi wake na kipande kingine akala yeye. Kila mmoja alipata sehemu
ya mkate huo. Hakuna aliyepewa mkate mzima. Na vipande hivyo vya mkate
vikikusanywa unapata mkate mzima.
Hapa
kuna jambo kubwa la kujifunza.
Vivyo
hivyo Yesu Kristo alipopaa aliteka mateka, na akagawa vipawa. Alimpa
mtume sehemu, na nabii sehemu, na mwinjilisti sehemu na mchungaji sehemu,
na mwalimu sehemu. Na wote hawa wakikusanywa na kila mmoja atoe sehemu
ya Neno la Kristo alilopewa, utapata neno zima la Kristo; na ndilo
litakalotufikisha katika umoja wa imani.
“Kwa
maana tunafahamu kwa sehemu; na tunafanya unabii kwa sehemu; lakini
ijapo ile iliyo kamili, iliyo kwa sehemu itabatilika.” (1 Wakorintho
13:9,10)
Tatizo
huwa linaanza kutokea mara tu mtu anaposikia wito wa kumtumika Mungu
ukiwaka ndani yake. Na kwa sababu ya mazingira tuliyolelewa, wazo la
kwanza linalomjia ni kutaka kuwa mchungaji.
Lakini
ni lazima tufahamu ya kuwa si wote walioitwa na Mungu kumtumikia,
wameitwa wawe wachungaji.
Kuna
wengine wameitwa wawe mitume lakini hawajui na kama wanajua hawaifanyi
kazi hiyo kwa kuwaogopa wanadamu.
Kuna
wengine wameitwa wawe wainjilisti lakini utakuta wanakwenda kwenye vyuo
vya biblia kusomea uchungaji. Na hawafahamu ya kuwa uinjilisti ni huduma
nyingine tofauti na uchungaji.Na mara nyingi watu wa namna hii wanapata
shida katika utumishi. Utakuta mtu amebarikiwa kuwa mchungaji lakini
kuishi kwake, kusema kwake na kuenenda kwake anaenenda kama mwinjilisti.
Na anashindwa kufanya kazi ya uchungaji vizuri.
Ni kitu
gani kinakuwa kimetokea?
Hebu
soma mstari huu wa Waefeso 4:1
“Kwa
hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, mwenende kama
inavyoustahili wito wenu mlioitiwa.”
Maana ya
mstari huu ni hii: Ikiwa umeitwa kuwa nabii enenda kama nabii. Ikiwa
umeitwa kuwa mwinjilisti, enenda kama mwinjilisti. Ikiwa umeitwa kuwa
mchungaji enenda kama mchungaji. Ikiwa umeitwa kuwa mtume, enenda kama
mtume. Na ikiwa umeitwa kuwa mwalimu, enenda kama mwalimu.
Tusichanganye huduma kama vile ambavyo wengine wanataka wao wenyewe wawe
wachungaji, wainjilisti, manabii, mitume, na waalimu kwa wakati mmoja.
Huu ni uchoyo na ni ubinafsi.
“Mkaribishane ninyi kwa ninyi, pasipo kunung’unika kila mmoja kwa kadiri
alivyoipokea karama, itumieni kwa kuhudumiana; kama mawakili wema wa
neema mbali mbali za Mungu. Mtu akisema, na aseme kama mausia ya Mungu;
mtu akihudumu, na ahudumu kwa nguvu anazojaliwa na Mungu; ili Mungu
atukuzwe katika mambo yote kwa Yesu Kristo. Utukufu na uweza una yeye
hata milele na milele. Amina.” ( 1Petro 4:9-11)
Na tena
tunasoma yafuatayo:
"Kwa kuwa kama
vile katika mwili mmoja tuna viungo vingi, vyote havitendi kazi moja;
vivyo na sisi tulio wengi tu mwili mmoja katika Kristo, na viungo kila
mmoja kwa mwenzake. Basi kwa kuwa tuna karama zilizo mbali mbali, kwa
kadiri ya neema tuliyopewa; ikiwa unabii, tutoe unabii kwa kadiri ya
imani; ikiwa huduma, tuwemo katika huduma yetu; mwenye kufundisha,
katika kufundisha kwake mwenye kuonya katika kuonya kwake; mwenye
kukirimu , kwa moyo mweupe; mwenye kusimamia, kwa bidii; mwenye kurehemu,
kwa furaha. Pendo na lisiwe na unafiki; lichukieni lililo ovu,
mkiambatana na lililo jema. Kwa pendo la udugu, mpendane ninyi kwa ninyi;
Kwa heshima mkiwatanguliza wenzenu."
(Warumi 12:4-10)
Laiti basi
tungekuwa waaminifu kuyatii na kuyafuata maongozi ya neno la Mungu,
matatizo mengi tuliyonayo yasingekuwapo.
Tafadhali
tusichanganye huduma na karama tulizopewa. Kama vile mafundisho
yaliyochanganywa, yanavyowachanganya wanafunzi vile vile na huduma
zilizochanganywa, zinawachanganya wanaohudumiwa. Na kwa kuwa kuna
kuchanganisha huduma na karama katikati ya wakristo, na wakristo, nao
wamechanganishwa. Hawajui waamini lipi na wamwamini nani. Kila dhehebu
lina mikazo yake, na wakristo wengi wanaifuata bila kujiuliza. Matokeo
yake ni kukosa umoja wa imani kati ya wakristo wa madhehebu mbali mbali.
Kitu gani
kimetutenganisha?
Ni mafundisho
yanayotoka kwa baadhi ya wafundishaji wa neno la Kristo, ambao huingiza
kipengele cha kuwadharau wakristo wengine katika mafundisho yao.
Wanapanda chuki
badala ya upendo. Wanapanda ugomvi badala ya amani. Wanapanda utengano
badala ya Umoja.
Kukosekana kwa
huduma zingine katika kanisa kumeathiri sana maisha ya kiroho ya
wakristo.
Kwa mfano biblia
inasema;
"Basi tangu sasa
ninyi si wageni wala wapitaji, bali ninyi ni wenyeji pamoja na
watakatifu, watu wa nyumbani mwake Mungu. Mmejengwa juu ya msingi wa
mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni."
(Waefeso 2:19-20)
Ndani ya mitume na
manabii, Kristo ameweka Neno lake lililo na kazi ya kujenga msingi wa
maisha ya kiroho ya wakristo. Mitume na manabii, wakikosekana siku hizi
za leo, wakristo wanakosa msingi ulio imara na mara nyingi huyumbishwa,
na wakati mwingine hata kuanguka kiroho. Tukiwa kama viungo vya Kristo,
kila mmoja na afanye wajibu wake, na Kristo atauunganisha na kuukuza
mwili wake yaani kanisa, ili upate kujijenga wenyewe katika upendo (Waefeso
3:16) .
Tuzidi kuombeana.