BARUA YA MWEZI MEI 2005
Bwana Yesu Asifiwe!
Salamu
kwako katika Jina la Yesu Kristo ambalo linastahili kusifiwa na
kuheshimiwa na kila mtu anayempenda Mungu wa kweli.
Mungu
amekusudia kuitembelea Tanzania. Na katika utaratibu wake analeta kwanza
upako wa utajiri kabla ya upako wa uamsho. Katika barua hii
tunakuonyesha uthibitisho wa nne wa kibiblia juu ya uhalisi na uhalali
wa jambo hili kutokea nchini.
Uthibitisho wa Nne
2 Wakorintho
9:10 –13
Ngoja tuangalie
2Kor.9:10-13 inasema hivi, “Na yeye ampaye mbegu mwenye kupanda, na
mkate uwe chakula, atawapa mbegu za kupanda na kuzizidisha, naye
atayaongeza mazao ya haki yenu. Mkitajirishwa katika vitu vyote, mpate
kuwa na ukarimu wote, umpatiao Mungu shukrani kwa kazi yetu. Maana
utumishi wa huduma hii hauwatimizii watakatifu riziki walizopungukiwa tu,
bali huzidi sana kuwa na faida kwa shukrani nyingi apewazo Mungu. Kwa
kuwa mkijaribiwa kwa utumishi huo wanamtukuza Mungu”.
Hapa anaangalia
habari ya utumishi kwa jinsi ya utoaji, watoaji ni watumishi, utoaji ni
utumishi! Anasema “mkijaribiwa kwa utumishi huo”! Labda nisome
ule mstari wa kumi na moja, labda hujawahi kuuona kwa namna hii, anasema,
“Mkitajirishwa katika vitu vyote (hebu sema vitu vyote)
anasema “mpate kuwa na ukarimu wote (sema ukarimu wote).
Unisikilize, huwezi kuwa na ukarimu wote isipokuwa umekuwa tajiri katika
vitu vyote!
Hainisaidii sana
kuniambia Mwakasege nilitaka kukusaidia kwenye huduma lakini sina fedha
za kukupa. Ndani ya moyo wako unataka sana kunisaidia kwa kulipia sehemu
ya gharama na huduma niliyonayo lakini huna fedha hizo!
Mungu anataka
akufungue kwenye hilo, ili uwe tajiri katika vitu vyote uweze kuwa na
ukarimu wote. Hasaidii kusema kwa kweli nitakuombea tu peke yake
siihitaji maombi tu peke yake ila nahitaji maombi pamoja na fedha.
Sasa, sikuambii ya
kuwa maombi hayana sehemu yake, lazima ufahamu ya kwamba maombi yana
sehemu yake, lakini Mungu hakusema toa maombi wakati unatakiwa kutoa
fedha! Watumishi wengi watakuambia juu ya hali hii. Wana watu wengi
wanaowaombea lakini wana watu wachache ambao wako tayari kuwapa fedha za
kugharimia huo utumishi walionao unaoombewa. Matokeo ni kazi ya Mungu
kukwama au kwenda polepole pamoja na maombi mengi kufanyika juu ya hiyo
kazi.
Mungu anataka
akufikishe mahali ndani ya moyo wako akikugusa kutoa uwe una kitu cha
kutoa; hapo ndipo mahali Mungu anapokupeleka. Hana sababu ya kukuwekea
mzigo kwa ajili ya kuigharamia huduma fulani halafu asikupe pesa za
kuisadia hiyo huduma. Lazima kuna tatizo mahali fulani linalosababisha
hali hii kwako.
Kwa sababu ule
upako unaompeleka yule mtumishi lazima kuna mahali unakusanya fedha
atazozihitaji kwenye utumishi huo.Lazima huu uhusiano uwepo. Au
hujatumwa na Mungu katika hilo unalofanya au umepewa fedha lakini
umezitumia si katika kugharamia huduma Mungu aliyokupa.
Ngoja nikuambie
namna hii; serikali za huku duniani zinavyoendesha mambo yao ni kivuli
cha serikali ya mbinguni. Kama vile huku duniani kuna bajeti, na
serikali ya mbinguni ina bajeti. Kama vile huku duniani kuna
‘ministries’, zinazoitwa Wizara, na mbinguni kuna ‘ministries’, kibiblia
haziitwi wizara bali zinaitwa huduma.
Kila mwaka serikali
inapanga mgawo wa fedha kwa ajili ya wizara zake kufuatana na mipango
iliyoko ili kutimiza kusudi la serikali; na mbinguni vile vile kuna
mgawo wa fedha unayopangwa kwa ajili ya ministries au huduma zilizoko
huku duniani kutimiza kusudi la Mungu, - kumbuka hili siku zote!
Huku duniani Waziri
hawezi tu akatumia zile fedha alizopewa kwenye wizara yake, nje ya
bajeti bila maelezo, lazima atajieleza vizuri. Labda atakwenda mpaka
bungeni ajieleze vizuri, kwa nini alitumia kama alivyotumia, na kama
alitumia vibaya Wabunge na mkaguzi wa mahesabu ya serikali watambana kwa
maswali mengi.
Mimi nataka
nikuambie ya kuwa kuna watu wengi sana watakwenda mbinguni na watakuta
bajeti yao haijaguswa, wala haijatumika, kwa sababu Mungu hawezi kutoa
fedha nje kwa kanisa ya kusudi lake.
Kama Rais hawezi
kutoa fedha nje ya kusudi la wizara, kwa nini mnataka Mungu atoe fedha
nje ya matumizi ya kusudi lake?
Ukishapata hiyo
picha utaelewa ninachokueleza hapa.
Mungu anataka
akutajirishe kwanza katika vitu vyote ndipo unapoweza kuwa
na ukarimu wote! Unaweza ukawa na ukarimu wote ndani ya moyo wako lakini
haisaidii sana kama huna vitu vya kutoa, … itakuumiza tu! Ndio maana
kama una moyo wa utoaji inaumiza sana kujua kwamba kuna shida ambayo kwa
kweli ungekuwa nacho ungeweza ukasaidia. Lakini kwa kuwa huna cha kutoa,
huwezi fanya kitu. Ni afadhali usingeijua.
Kwa wale ambao
wanazunguka kama tunavyozunguka wanaelewa hii ni lugha gani ambayo
Mungu anasema katika ujumbe huu.
Tulipokuwa Dodoma
kuna kijana mmoja ambaye alikuwa anavuta bangi ameacha shule, na kila
mtu amemkatia tamaa, akarudi kwa Yesu wakati wa semina tuliyoifanya na
akaacha kuvuta bangi, akataka kurudi shule, lakini nani anamlipia?
Tulipokuwa Moshi
kuna msichana mmoja alikuwa kichaa, akapelekwa hospitali mbalimbali
hakupata msaada wowote wa kupona, akarudishwa kwao kule Moshi.
Tulipokuwa na semina Moshi mjini akaletwa uwanjani kafungwa kamba
mkononi na miguuni. Lakini tulipomwombea akapona.
Akaletwa pale mbele
jukwaani kushuhudia. Akaeleza jinsi alivyoteseka, na jinsi walivyokuwa
wanamfunga kwa kamba. Alipomaliza, akasema, “Mwakasege nataka kusoma
shule, wazazi wangu hawana uwezo wa kunisomesha.”
Nikasema, moyoni “
Mungu nisaidie”, Mungu akasema moyoni mwangu “Yuko mtu nimemwandaa kwa
ajili ya kumlipia”. Nikasema kwa sauti, “yule mtu aliyeandaliwa kwa
ajili ya kumlipia huyu msichana aje mara moja”. Wakatokeza watu wawili.
Nikawaunganisha na
mwenyekiti wa semina ili wafuatilie, wajue ni shule gani alikuwa anasoma,
anataka kusoma kitu gani sasa,na pia wawasiliane na wazazi wake. Ni watu
wengi tunaokutana nao waliona na mahitaji ya namna hiyo na ni wengi,
lakini ni nani atawalipia?
Unaliona hili? Bila
utajiri wa vitu vyote, huwezi ukawa na ukarimu wote.
Tumeangalia hadi
sasa, sehemu nne katika biblia zinazoonyesha ya kuwa neno ambalo Mungu
amesema kwa ajili ya Tanzania – linathibitika kibiblia.
Ni unabii na ujumbe
muhimu kwa ajili ya Tanzania, ni muhimu tuwe na uhakika ya kuwa
unathibitika kibiblia, kabla hatujaanza kuamini, na kujiandaa kwa ujio
wake.
Katika barua za
mwezi inayofuata, tutaangalia kwa mifano ya kibiblia inayofanana na
utekelezaji wa neno hili lililotamkwa kwa ajili ya Tanzania. Tumeona kwa
maandiko katika sehemu nne, uthibitisho wa unabii huu. Mifano
tunayoiangalia katika barua zijazo zinazofuata miezi ijayo itatupa kujua
na kuwa na uhakika ya kuwa ikiwa Mungu aliwahi kufanya jambo kama hili
zamani, basi hata leo anaweza kulifanya tena!
Tuzidi kuombeana.
Neema ya Bwana
Yesu Kristo izidi kuwa juu yako daima.