|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
HUWEZI
KUONDOA JAMBO LA UCHUMI NDANI
YA DAMU YA YESU Barua ya mwezi uliopita (Machi 2007) tulizungumza na wewe
ya kuwa mtu hawezi kuondoa jambo la uchumi ndani ya damu ya Yesu. Tulianza kwa kukupa sababu mbili zinazotufanya tuamini ya
kuwa hakuna mtu anayeweza kuondoa jambo la uchumi ndani ya damu ya Yesu. Tulikwambia ya kuwa sababu ya Kwanza ni kwamba: Agano jipya
katika damu ya Yesu linahusisha pia jambo la uchumi. Na sababu ya Pili
ni ya kuwa: Kile kinachokumbukwa
wakati wa kusherehekea sikukuu ya pasaka – ni pamoja na mtu
kukombolewa ki-uchumi. Leo tunataka tuzungumze na wewe juu
ya sababu ya Tatu ambayo ni: Kupokea baraka ya Ibrahimu kupitia katika damu ya Yesu. Wagalatia
3:13,14 inatuambia hivi: “Kristo alitukomboa
katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana
imeandikwa, amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka
ya Ibrahimu iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo…….” Kwa lugha nyepesi au kwa tafsiri nyepesi tunaambiwa hapa ya
kuwa, kule kusulubiwa kwa Kristo msalabani kumefungua mlango kwa kila
atakaye kupokea urithi wa baraka ya Ibrahimu – katika Yesu Kristo. Tafsiri hii inathibitishwa na maneno ya Wagalatia 3:29
yanayosema; “Na kama ninyi ni
wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi”. Ikiwa kwa kumwamini Yesu Kristo juu ya kile alichofanya
msalabani na damu kumwagika kwa ajili yetu, kunatufanya pia tuwe “uzao
wa Ibrahimu na warithi sawasawa na ahadi” – ni muhimu
tuifuatilie ahadi hiyo ya urithi ya Ibrahimu, ili tujue tumerithi mambo
gani. Tunasoma katika Warumi 4:13,16 ya kuwa; “kwa
maana ahadi ile ya kwamba atakuwa mrithi wa ulimwengu alipewa Ibrahimu
na uzao wake, si kwa sheria bali kwa haki aliyohesabiwa kwa imani ….
Kwa hiyo ilitoka kwa imani, iwe kwa njia ya neema, ili kwamba ile ahadi
iwe imara kwa wazao wote, si kwa wale wa torati tu, ila na kwa wale wa
imani ya Ibrahimu; aliye baba yetu sisi sote” Ni ahadi gani ambayo Ibrahimu alipewa na Mungu? Ni hii ya
kuwa “mrithi wa ulimwengu”.
Kwa hiyo ikiwa na sisi ni uzao wa Ibrahimu kwa imani ndani yake Kristo
Yesu, ina maana basi na sisi ni “warithi
wa ulimwengu”. “Ulimwengu”
ndio “baraka” aliyopewa Ibrahimu na Mungu kama ahadi ya urithi kwa
ajili yake, na uzao wake – pamoja na sisi tulio uzao wake kwa imani
katika Kristo Yesu. “Mrithi wa
ulimwengu”
maana yake nini? Ni mrithi wa “baraka”
ipi hiyo inayojulikana kama “ulimwengu”? Hii ina maana baraka isemwayo hapa ilikuwa inahusu vitu
vya hapa ulimwenguni! Ndiyo maana katika kitabu cha Mwanzo 22:14,
Mungu alijifunua kwa Ibrahimu kama “Yehova-yire”. “Yehova- yire” maana
yake ni Mungu au Bwana ambaye anapata katika ulimwengu huu kila anachohitaji
kupata kwa ajili ya kuwabariki au kuwafanikisha watu wake hapa ulimwengu. Ndiyo maana baada ya Mungu kujifunua kwa Ibrahimu kama “Yehova
– yire” katika Mwanzo 22:14; tunaona chini yake katika mstari wa
17-18 akimwambia Ibrahimu ya kuwa: “katika
kubariki nitakubariki, na katika kuzidisha nitauzidisha uzao wako kama
nyota za mbinguni, na kama mchanga ulioko pwani; na uzao wako utamiliki
mlango wa adui zao; na katika uzao wako mataifa yote ya dunia
watajibarikia, kwa sababu umetii sauti yangu” Kilichomfanya Mungu ajifunue kwa Ibrahimu na kuitamka hiyo
ya baraka- ni kumwagika kwa damu ya kondoo kama sadaka badala ya mtoto
wake Isaka. Ukiifuatilia habari hii ya Ibrahimu kupokea baraka za “Yehova
– yire” juu ya kuishi kwake hapa ulimwenguni, utaona ya kuwa
Mungu alimbariki “Ibrahimu katika vitu vyote” (Mwanzo 24:10.) Mjakazi wa Ibrahimu aliorodhesha baraka za Ibrahimu
aliposema; “Bwana amembarikia
sana Bwana wangu, amekuwa mtu mkuu; amempa kondoo, na ng’ombe, na
fedha, na dhahabu, na watumwa, na wajakazi, na ngamia, na punda”. Kila unapozisoma baraka za Ibrahimu ni muhimu uwe
unajikumbusha ya kuwa hizo baraka ni urithi wako pia ukiwa ndani ya
Kristo. Kwa sababu ya damu ya Yesu iliyomwagika kwa ajili yetu! Umeziangalia vizuri hizo baraka? Utaona zinahusu uchumi wa
Ibrahimu na uzao wake, hii ni ikiwa pamoja na wewe kama Yesu Kristo ni
Bwana na Mwokozi wako. Kutoka sura ya 13:14-18 na sura ya 15:1-21 inatuonyesha ya
kuwa “kumiliki ardhi” ni
sehemu ya “urithi wa ulimwengu”
aliopewa Ibrahimu na uzao wake. Kwa sababu ya undugu uliopo kati ya Ibrahimu na Yesu Kristo
kwa njia ya damu ya Yesu, ni vigumu mtu kuweza kuondoa jambo la uchumi
ndani ya damu ya Yesu. Pamoja na mambo
mengine ambayo damu ya Yesu inafanya kwa mwanadamu, tukumbuke
ilimwagika pia ili kutusaidia hali zetu za uchumi ziwe nzuri.
Ndivyo biblia inavyotuambia – ya kwamba mtu anapokuwa
ndani ya Yesu, anakuwa mrithi mara mbili! Kufuatana na Wagalatia 3:29 mtu anapokuwa ndani ya Yesu
Kristo anakuwa “mrithi wa
Ibrahimu” Imeandikwa; “Na kama ninyi ni
wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi”. Tena kufuatana na Wagalatia 4:6-7 na Warumi 8:16,17 mtu
anapokuwa ndani ya Kristo anakuwa “mrithi
wa Mungu”. Imeandikwa juu ya jambo hili ya kwamba: “Na
kwa kuwa ninyi mmekuwa wana, Mungu alimtuma Roho wa Mwanawe mioyoni
mwetu, aliaye, Aba, yaani, Baba. Kama ni hivyo, wewe si mtumwa tena bali
u mwana; na kama u mwana, basi, u mrithi kwa Mungu”. “Roho mwenyewe
hushuhudia pamoja na roho zetu, ya kuwa sisi tu watoto wa Mungu; na kama
tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo;
naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja naye” Hii inatufanya tuwe warithi mara mbili! Warithi wa Ibrahimu
na warithi wa Mungu, warithio pamoja na Kristo. Ndani ya urithi wa Ibrahimu, tunarithi baraka za Ibrahimu.
Na ndani ya urithi wa Mungu, tunaourithi pamoja na Kristo, tunarithi “baraka
zote za rohoni, katika ulimwengu wa roho ndani yake Kristo” (Waefeso
1:3) Ikiwa katika baraka za Ibrahimu tunarithi “ulimwengu”,
- au tunarithi “mafanikio ya
ulimwengu huu”, na ikiwa katika Mungu tunarithi pamoja na Kristo baraka
zote za rohoni – basi
hakuna sababu kwa nini mtu aliye ndani ya Kristo asifanikiwe katika
mambo yake yote – kiroho , kiakili, kimwili na ki-uchumi. |
|