|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Tunayo furaha katika Roho
Mtakatifu kukuandikia barua ya mwezi huu ambayo ni mwanzo wa mfululuzo
wa barua nne zenye ujumbe muhimu sana. Je, unajua kiwango cha umuhimu wa
maombi yako unapoombea toka katika nafasi ya mfalme na kuhani katika
Kristo? Swali hili tutalijibu katika barua hizi nne kuanzia na hii
unayoisoma sasa. Neno la Mungu katika biblia linatuambia ya kuwa tunapokuwa
katika Kristo Yesu tunafanyika pia kuwa Wafalme
na Makuhani kwa Mungu wetu.
Ufunuo wa Yohana 5:9,10 inasema ya kuwa; “Ukamnunulia
Mungu kwa damu yako watu wa kila kabila na lugha na jamaa na taifa,
ukawafanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu wetu, nao wanamiliki juu ya
nchi”.
Ufunuo wa Yohana 1:5,6 inasema ya kuwa; “....Yeye
atupendaye na kutuosha dhambi zetu katika damu yake, na kutufanya kuwa ufalme na makuhani kwa Mungu.....”.
Maneno haya “wafalme na makuhani” katika tafsiri zingine za awali za biblia
yanasomeka hivi “wafalme
na makuhani”. Ndiyo – katika Kristo Yesu tunafanyika wafalme
na makuhani kwa Mungu wetu.
Kwa kuwa walio ndani ya Kristo wamefanyika “wafalme
na makuhani” – biblia inasema kwa sababu hiyo “wanamiliki
katika nchi” (Ufunuo wa Yohana 5:10), na tena kufuatana na
Warumi 5:17 wanatawala katika maisha haya
kwa uzima wa Kristo uliomo ndani yao!
Kufanyika na kuwa mfalme
na kuhani kwa wakati mmoja ni nafasi
kubwa na heshima kubwa ambayo
Mungu anampa mtu kati ya watu
wengine ili wamiliki na kutawala pamoja naye katika eneo alilomkabidhi.
Tena, kuwa mfalme na kuhani ni
wajibu mkubwa sana ambao katika agano la kale walipewa watu wachache
sana….wakati katika agano jipya wengi amepewa ila hawajui! Na wale
wanaojua juu ya wajibu huu hawautumii ipasavyo.
Mungu analiheshimu sana Neno
linalotoka katika maombi ya mtu ambaye amesimama katika nafasi
ya mfalme na kuhani! Hii ni kwa sababu hayo yanakuwa si maombi ya kawaida, kwa
kuwa ni maombi yanayotoka kwenye kinywa cha mtu ambaye yuko kwenye
nafasi ya mfalme na kuhani.
Ni muhimu kujua ya kuwa nguvu ya neno asemalo mtu, inatoka kwenye
nafasi ya mtu asemaye neno
hilo, kulielekeza kwenye eneo linalohusika na nafasi
hiyo.
Kwa mfano; mke wangu ni mwanamke kama wanawake wengine lakini
nafasi aliyonayo kwangu inafanya neno lake analolisema kwangu liwe na
uzito kwangu kuliko neno atakalolisema mwanamke mwingine. Hii si kwa
sababu neno la mwanamke mwingine si la maana bali linakosa nguvu kwa
sababu ya nafasi aliyonayo kwangu – ni tofauti na nafasi aliyonayo mke
wangu.
Ukiangalia mfano wa Rais wa nchi, utaona ya kuwa kuna marais
wengi duniani, lakini si kila neno la kila Rais lina uzito ule ule kwa
kila nchi! Lakini neno la Rais lina uzito zaidi katika nchi ambayo yeye
ni Rais! Neno la Rais, au la mkuu wa mkoa lina nguvu na sauti katika
eneo lile tu analiongoza, kufuatana na katiba ya nchi na heshima
aliyonayo kwa watu walio katika eneo analoliongoza. Ndiyo maana nauliza swali hili muhimu - ikiwa unajua kiwango
cha umuhimu wa maombi yako unayoomba ukiwa katika nafasi ya mfalme na
kuhani katika Kristo Yesu. Hebu tuangalie na kutafakari kwa undani mifano ifuatayo ya
biblia: Mfano
wa maombi Katika kitabu cha Yakobo 5:10 – 18 tunasoma ya kuwa “….kuomba
kwake mwenye haki kwafaa sana, akiomba kwa bidii. Eliya alikuwa
mwanadamu mwenye tabia moja na sisi, akaomba kwa bidii mvua isinye; na
mvua haikunya juu ya nchi muda wa miaka mitatu na miezi sita. Akaomba
tena, mbingu zikatoa mvua, nayo nchi ikazaa matunda yake”. Mistari hii inataka tujue ya kuwa pamoja na kwamba nabii
Eliya alikuwa kwa jinsi ya nje mtu wa kawaida kama sisi – lakini
kuomba au kutokuomba kwa nabii Eliya ndiko kulikokuwa na uamuzi wa
mwisho juu ya mvua inyeshe au isinyeshe katika eneo alilokuwepo! Hujakosea – umesoma sawa sawa ya kuwa; kuomba au kutokuomba kwa nabii
Eliya ndiko kulikokuwa na uamuzi wa mwisho juu ya mvua inyeshe au
isinyeshe katika eneo alilokuwepo! Neno
lake
linakuwa amri ya mwisho juu ya mvua katika taifa lile – na Mungu akalisimamia.
Tunasoma katika 1 Wafalme 17:1 ya kuwa nabii Eliya alimwambia Ahabu hivi;
“Kama Bwana, Mungu wa
Israeli, aishivyo, ambaye ninasimama mbele zake hakutakuwa na umande
wala mvua miaka hii, ila kwa neno langu”. Nabii Eliya asingekuwa na ujasiri wa kusema neno la jinsi
hii kama
asingekuwa na uhakika na nafasi aliyokuwa nayo kwa Mungu wake! Ukisoma Wafalme wa kwanza sura ya 18 utaona ya kuwa katika
mstari wa 1 Mungu anamwambia nabii Eliya ya kuwa, “Enenda ukajionyeshe kwa Ahabu; nami nitaleta mvua juu ya nchi”. Kumbuka kufuatana na Yakobo 5:17 neno la nabii Eliya
liliifunga mvua kwa miaka mitatu na nusu, lakini mara baada ya kupita
miaka mitatu - Mungu alimwambia nabii Eliya akajionyeshe kwa Ahabu
ataleta mvua! Nabii Eliya na Ahabu walipokutana mvua haikunyesha! Soma
mwenyewe katika 1 Wafalme 18:17,18. Pamoja na kwamba Mungu alimwambia nabii Eliya ataleta mvua
atakapojionyesha kwa Ahabu, bado mvua haikunyesha walipokutana hadi
nabii Eliya alipochukua hatua ya kuomba ili mvua inyeshe – ndipo Mungu
akaleta mvua! Hivi ndivyo tunavyosoma katika 1 Wafalme 18:41 – 45 na
Yakobo 5:18 kwa nini Mungu aheshimu neno na maombi ya nabii Eliya kwa kiwango
kikubwa hivi? Jibu lake ni kwa sababu nabii Eliya alisema neno alilosema
akiwa katika nafasi ya mfalme
kwa Mungu; na alipoomba alichoomba aliomba akiwa katika nafasi
ya kuhani kwa Mungu. Nafasi hizi mbili zilimpa nabii Eliya uwezo wa kumiliki na
kutawala juu ya kunyesha au kutokunyesha kwa mvua katika eneo alilokuwa
anaishi wakati huo. Kumbuka mfalme ni
mtu yule anayeongoza katika maamuzi katika eneo ambalo yeye ni mfalme.
Neno lake ni la mwisho, na
neno lake ni sheria, na
linaweka utaratibu anaotaka ufuatwe na wote waliochini ya himaya yake. Kumbuka kuhani ni
mtu yule anayefanya maombi kwa ajili yake au kwa ajili ya mwingine kwa
nia ya kumkaribisha Mungu ahusike na hicho anachokiombea. Pamoja na kwamba wakati wa utawala wa Ahabu, manabii wengi
walikuwepo (1
Wafalme 18:4), lakini si wote walipewa na Mungu kushika nafasi ya mfalme
na kuhani katika ulimwengu wa roho – isipokuwa nabii Eliya peke yake! Nafasi hizi mbili ndizo zilizomfanya nabii Eliya aseme neno
na aombe maombi kwa namna ambavyo Mungu alisimama upande wake! Je itakuwa ni sawa sasa tukijuliza kwa mfano, ikiwa nchi
inasumbuliwa na hali mbaya ya hewa kama ukame au mafuriko basi kuna mtu
aliyetakiwa asimame kwenye zamu yake ya kuombea hali ya hewa nchini iwe
inakuwa nzuri lakini hakuomba, au ikiwa aliomba basi hakuomba ipasavyo?
Je, mtu huyo ni wewe? Mfalme Ahabu alipomwona nabii Eliya, akamwambia “Je!ni
wewe, ewe mtaabishaji wa Israeli?” (1 Wafalme 18:17). Ahabu
alimwona Eliya ya kuwa ni “mtaabishaji wa Israeli”
kwa kuwa alijua ya kuwa kunyesha au kutokunyesha kwa mvua katika nchi
yao kulitegemea maombi ya Eliya – lakini Eliya alikaa kimya! Je! wewe ni mwombaji au mtaabishaji juu ya eneo ambalo Mungu
amekuweka ukae hapo, au ufanya kazi hapo, au ufanye huduma hapo, au
uishi hapo? Usikose kuisoma barua yetu ya mwezi ujao ambayo tutaendelea
kukuletea mwendelezo wa ujumbe huu muhimu. Usisahau kutuombea – Mungu azidi kututunza na kututumia
sawa na mapenzi yake juu ya maisha yetu. |
|