|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Mwezi huu tunamalizia maelezo ya
kimafundisho juu ya uhusiano uliopo kati ya kumtumikia Mungu na taifa la
Israeli. Sasa endelea… Mtini ni Taifa
Ukisoma katika Kitabu cha Yoeli 1:6, 7 utaona ya kuwa Mungu
ameulinganisha mti wa mtini na Taifa la Israeli – anaposema hivi; “maana
Taifa limepanda juu ya nchi yangu, lenye nguvu, tena halina hesabu; meno
yake ni kama meno ya simba, yana ana magego ya simba mkubwa. Ameuharibu
mzabibu wangu; ameuvunja mtini wangu …”
Mungu anaposema; “Nchi yangu” na kuifananisha na “mzabibu
wangu” na “mtini wangu” – tunajua ya kuwa anazungumzia juu ya
Taifa la Israeli au nchi ya Israeli.
Tunaliona wazo hili likijitokeza tunaposoma Hosea 9:10 hivi; “Mimi nilimkuta Israeli kama zabibu nyikani; nami naliwaona baba zenu
kama matunda ya mtini yaliyoiva kwanza …”
Ikiwa mti wa mtini wakati mwingine katika Biblia unatumika
kuelezea juu ya nchi ya Israeli – basi tujue ya kuwa Yesu Kristo
alipokuwa anasema “kwa mtini tujifunzeni mfano” alitaka na anataka tujifunze
kutoka kwa taifa la Israeli!
Tujifunze jambo gani kutoka kwa taifa la Israeli? Ni muhimu kwanza tujue kwa mtini alitaka tujifunze nini! Yesu Kristo alisema
juu ya mtini hivi; “tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa
wakati wa mavuno u karibu”.
Kufuatana na ukuaji wa mtini, tawi lake huwa linapukutisha majani
yake wakati wa msimu wa baridi kali (winter),
na huwa linachipuka na kuchanua majani wakati wa kipindi cha joto
kinapoanza. Mabadiliko haya ya tawi la mtini ni
matokeo ya mabadiliko ya majira na nyakati ambazo Mungu aliziamuru
ziwepo juu ya eneo ambalo mtini unaota!
Yesu Kristo baada ya kuelezea mabadiliko ya tawi la mtini akasema;
“nanyi
kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu milangoni”
(Mathayo 24:33).
Lakini tukumbuke ya kuwa “tawi” la mtini haliwezi likawa na
mabadiliko au haliwezi kuwepo kama tawi ikiwa mtini “haujapandwa na
kuota”.
Kwa hiyo, ikiwa Yesu Kristo alipotoa mfano wa mtini alikuwa
anaulinganisha na Taifa la Israeli, basi, ni muhimu tujue alitaka tufahamu ya kuwa Israeli itakapokuwa Taifa na
kujitawala katika nchi yake yenyewe, ndipo tunapotakiwa kuangalia
mabadiliko yaliyotabiriwa kutokea juu yake! Kwa kuwa mabadiliko
hayo yanaonyesha na kuashiria ukaribu wa kurudi kwa Yesu Kristo
kulichukua Kanisa. Tawi
linapochipua halileti mabadiliko, bali linatoa taarifa juu ya mabadiliko,
yaliyokwisha kutokea katika eneo mtini ulipo! Umepata tunachotaka ukione hapa?
Ngoja turudie! Tawi linapochipuka huwa halileti mabadiliko ya msimu kwa
kuchipia kwake, bali kwa kuchipua kwake, tawi hilo huwa linatoa taarifa
kwa walitazamao ya kuwa kuna mabadiliko ya msimu au nyakati katika eneo
ambalo mti huo umepandwa!
Israeli “imepandwa” lini na kuwa Taifa? Ilipandwa mwaka 1948
kwa tamko rasmi la Umoja wa Mataifa ulio na makao makuu yake nchini
Marekani katika jiji la New York. Kwa hiyo tunaweza kusema 1948 ni mwaka
ambao mtini (Israeli) ulipandwa!
Yesu Kristo anatuambia tuagalie mabadiliko yanayotokea juu ya
tawi la mtini kutokana na majira yaliyowekwa juu yake. Halafu akasema “nanyi kadhalika, myaonapo
hayo yote …” tuyaonapo yote – yapi? … ni yale yaliyatabiriwa kutokea juu ya Taifa la Israeli kuanzia mwaka 1948!.
Ni mambo gani yaliyotabiriwa kutokea juu ya Taifa la Israeli
baada ya mwaka 1948? Pamoja na kwamba yako mambo kadhaa yaliyotabiriwa
juu ya Israeli juu ya siku za mwisho, kabla na baada ya mwaka 1948,
itakusaidia ukifuatilia kwa karibu maeneo yafuatayo:- 1.
Mipaka ya ardhi ya nchi ya Israeli. 2.
Umiliki wa mji wa Yerusalemu. 3.
Ujenzi wa hekalu la tatu. 4.
Mabadiliko ya uongozi wa juu wa Taifa la Israeli.
Kumbuka jambo hili unapofuatilia mambo haya: Tawi la mtini
linapochipuka na kuchanua huwa – halileti mabadiliko ya msimu
– bali linatoa taarifa ya mabadiliko ya msimu
yaliyokwisha kutokea tayari!
Kwa hiyo basi unapofuatilia mambo hayo manne makubwa fahamu ya
kuwa kutokea kwa mabadiliko yaliyotabiriwa kutokea juu ya taifa la
Israeli- ni njia ya Mungu kuliarifu Kanisa, watumishi wake, na ulimwengu
wote ya kuwa kurudi kwa Yesu Kristo kuja kilichukua Kanisa kumekaribia
sana!
Kwa maneno mengine, Mungu anataka tuiangalie Israeli kama “saa
ya nyakati za” au “Kipima muda cha” siku za mwisho; na mabadiliko
yaliyotabiriwa kutokea baada ya Israeli kuwa Taifa mwaka 1948 yatakuwa
yanatuonyesha ukaribu wa ‘siku ile na saa ile” ambayo “hakuna aijuaye – hata malaika walio mbinguni wala Mwana, ila Baba
peke yake” (Mathayo 24: 36).
Vita vilivyodumu siku sita ambavyo Israeli ilipigana na majeshi
ya nchi za Kiarabu Juni 1967 vilikuwa ni vita vilivyotoa taarifa kwa
Kanisa, kwa watumishi wa Mungu, na kwa ulimwengu wote ya kuwa msimu
mpya katika siku za mwisho umeujilia ulimwengu, na kurudi kwa Yesu
Kristo kunazidi kukaribia sana!
Hivi vita viligusa mambo yote manne tuliyoyaorodhesha hapo juu,
kwa hiyo ni muhimu uyafuatilie unapojifunza juu ya Taifa la Israeli.
Vita hivyo vya siku sita vya Juni 1967 vilipokoma, na Israeli
ikiwa imeshinda vita hivyo, mambo ya kinabii yaliyotabiriwa yalitokea ni
kama ifuatavyo:- 1.
Mipaka
ya Nchi ya Israeli.
Israeli ilipopewa utaifa na Umoja wa Mataifa – mipaka ya Nchi
yake haikuwa sawa na ile ambayo Mungu alikuwa ameiweka ya kuwa itakuwa
mipaka ya nchi ya Israeli katika siku hizi za mwisho.
Lakini vita vya Juni 1967 vilimalizika kwa namna ambayo nchi ya
Israeli ilipanua au “ilichanua kama mtini” mipaka yake na kujikuta
imepanua ukubwa wa nchi yake hadi kufikiwa kwa sehemu kubwa kwa mipaka ambayo Mungu aliwapa kama tusomavyo
katika Kitabu cha Hesabu 34: 1-12. 2.
Umiliki
wa mji wa Yerusalemu.
Umoja wa Mataifa ulipokuwa unaipa Israeli utaifa katika nchi ya
kaanani, mwaka 1948 pia uliugawa mji wa Yerusalemu katika umiliki wa
mataifa mawili. Upande wa Magharibi wa mji wa Yerusalemu ndio
uliokabidhiwa kwa Taifa la Israeli, na upande wa Mashariki mji wa
Yerusalemu lilikabidhiwa Taifa la Jordani.
Upande wa mashariki mwa mji wa Yerusalemu ndiko kulikokuwa na
maeneo muhimu sana yaliyohusu historia ya Taifa la Israeli. Huko ndiko
uliko mlima mtakatifu – ambako hekalu za Mfalme Sulemani na Herode
zilijengwa. Pia, ndiko kuliko na mlima wa Mzeituni, bustani ya Getsemani,
na chuo kikuu cha Kiebrania (Hebrew
University).
Kwa ajili hiyo, Umoja wa Mataifa ukatengeneza mkataba mwaka huo
wa 1948 ulioitaka Serikali ya Jordani kuwaruhusu Wayahudi wanaotaka
kwenda kuabudu kwenye Mlima mtakatifu wawe na uhuru wa kufanya hivyo.
Lakini serikali ya Jordani ya wakati huo, licha ya kuridhia na kutia
sahihi mapatano hayo, ilikataa kuwaruhusu Wayahudi kwenda kuabudu katika
mlima mtakatifu uliokuwa mashariki mwa mji wa Yerusalemu. Kukataa huku
kulifanya Wayahudi washindwe kwenda kuabudu kwenye mlima mtakatifu kwa
muda wa miaka 19.
Wakati wa vita vya Juni 1967, Jeshi la Israeli liliteka upande wa
mashariki wa mji wa Yerusalemu, na kwa kufanya hivyo kutimiza unabii wa
Yesu juu ya mji wa Yesuralemu aliosema; “na
Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia”
(Luka 21: 24).
“Majira ya Mataifa” yalitimia Juni 1967! Mji
wa Yerusalemu ukaanza kuhesabu siku za majira mapya juu yake kama mji
mmoja ulio “kiti” cha utawala cha mfalme Daudi, na cha Taifa la
Israeli! 3.
Mabadiliko
ya Uongozi wa juu wa Taifa la Israeli.
Kama tulivyokwisha kukueleza juu ya mji wa Yerusalemu, fahamu ya
kuwa Juni 1967 kuliingia kipindi kipya cha kinabii juu ya uongozi wa
Taifa la Israeli.
Hii ni kwa sababu mji wa Yerusalemu ndipo panapotakiwa pawe
“kiti” cha utawala wa taifa la Israeli katika siku hizi za mwisho.
Kabla ya Juni 1967 ilikuwa vigumu kuzungumzia jambo hili, maana mji wa
Yerusalemu ulikuwa umegawanywa kwa mataifa mawili – Israeli na Jordani.
Vita hivyo vilipomalizika vilirudisha sehemu ya mashariki ya mji
wa Yerusalemu mikononi mwa taifa la Israeli, na kutimiza andiko la Luka
21:24 linalosema “na
Yerusalemu utakanyagwa na Mataifa, hata majira ya Mataifa yatakapotimia”.
Kwa matiki hii miaka ya kinabii ya Uongozi juu ya Taifa la
Israeli yaliingia ukurasa mpya Juni 1967.
Mtu anayefuatilia kwa karibu juu ya miaka ya uongozi juu ya Taifa
la Israeli, atakuwa anajua ya kuwa miaka arobaini – arobaini
imejitokeza katika historia ya taifa la Israeli kuwa ni
kipindi muhimu.
Kwa Mfano: Wana wa Israeli walikuwa chini ya Utawala wa uongozi
wa Mwamuzi Othinieli kwa miaka arobaini (Waamuzi
3: 9 – 11). Pia wana wa Israeli walikaa chini ya uongozi wa
Mwamuzi Baraka kwa miaka arobaini (Waamuzi
5: 31). Tena wakawa chini ya uongozi wa Gedioni kwa muda wa miaka
aroabaini (Waamuzi 8: 28).
Halafu wakawa chini ya uongozi wa Wafilisti kwa jumla ya miaka arobaini (Waamuzi 13:1).
Umewahi kujiuliza kwa nini miaka arobaini – arobaini ijurudie – rudie, kwa jinsi hii,
– tena katika taifa moja?
Ukiendelea kufuatilia historia ya wana wa Israeli utaona ya kuwa
waliwahi kuwa chini ya uongozi wa kuhani Mkuu Eli kwa muda wa miaka
arobaini (1 Samweli 4: 18). Tena wakawa chini ya Mfalme Sauli kwa muda wa
miaka arobaini (Matendo ya Mitume
13: 21). Mfalme Daudi alitawala juu ya wana wa Israeli kwa miaka
arobaini (2 Samweli 5:4). Mfalme
Sulemani aliyechukuwa utawala baada ya Mfalme Daudi – naye alitawala
juu ya wana wa Israeli kwa miaka arobaini (1
Wafalme 11:42). Halafu wana wa Israeli waliwahi kuwa chini ya Mfalme
Yoashi kwa miaka arobaini pia (2
Mambo ya Nyakati 24:1).
Kipindi hicho cha miaka arobaini katika
mara zote tulizozinukuu, kilikuwa kinaashiria mwisho wa kipindi
kimojawapo cha utawala na kuanza kwa kipindi kingine cha utawala.
Na ikiwa tutaamua kujifunza kutoka kwa mtini kama Yesu alivyosema
– tutaelewa
ya kuwa mabadiliko ya tawi la mtini yanatoa taarifa ya mabadiliko ya
msimu.
Kwa hiyo “miaka arobaini” juu ya “kiti” cha “Daudi”
yaani mji wa Yerusalemu ni kipindi muhimu sana.
Ukichukua Juni 1967, kipindi ambacho mji wa Yerusalemu ulipokuwa
unamaliza “msimu wa kukanyagwa
na Wamataifa”, hii ilikuwa taarifa ya kinabii ya mwisho wa msimu
wa utawala mmoja na mwanzo wa msimu wa utawala mwingine! Na ukijumlisha
miaka arobaini tokea Juni 1967 utajikuta unafika Juni 2007!
Kwa hiyo basi, Juni 2007 imeashiria na kutangaza msimu mpya
katika majira na nyakati za Kiroho na za Kisiasa juu taifa la Israeli.
Je, kuna uhusiano wo wote kati ya mabadiliko ya nafasi ya Urais
wa Israeli uliotokea Juni 2007 na msimu mpya wa uongozi katika ratiba ya
Mungu juu ya taifa la Israeli?
Kama watumishi wa Mungu wanaomtumikia Mungu katika kizazi hiki,
tukikazana kwa nia zote, na juhudi zote kuwapa watu chakula cha neno la
Mungu kwa wakati wa Mungu, hatuwezi
kukwepa kuangalia kwa makini matukio ya yale yaliyotabiriwa yanapotokea
juu ya taifa la Israeli!
Kwetu sisi ni ishara muhimu ya ukaribu wa ujio wa Bwana Yesu
Kristo kulichukua Kanisa. Kwa hiyo huu si wakati wa “kulala” au
“kuzembea” au “kulegea” au “kusuasua” au “kuzubaa” au
“kuchelewa” au “kusita” – katika kumtumikia Mungu!. 4.
Ujenzi
wa Hekalu la Tatu.
Yesu Kristo alisema hivi; “Basi
hapo mtakapoliona chukizo la Uharibifu, lile lililonenwa na nabii Daniel
limesimama katika patakatifu (asomaye na afahamu) …” (Mathayo
24:15).
Maneno haya yalikuwa yanaashiria kuwepo kwa hekalu jingine katika
mlima mtakafitu. Jambo la ujenzi wa hekalu la tatu katika milma
mtakatifu lilikuwa ni ndoto ambayo ilikuwa haitekelezeki kabla ya
kumalizika kwa vita vya Juni 1967. Kwanza,
kwa sababu eneo hilo la mlima mtakatifu lilikuwa linamilikiwa na
Serikali ya Jordani kihalali kwa amri ya Umoja wa Mataifa; na pili
kwa sababu eneo la juu ya mlima mtakatifu pamejengwa Msikiti wa Kiislamu!
Lakini ushindi uliotokea kwa Israeli katika vita hiyo ya Juni
1967 kulifungua mlango wa kutimia kwa andiko hili la Biblia la Ufunuo wa
Yohana 11: 1, 2 linalosema:
“Nikapewa mwanzi kama
fimbo; na mmoja akaniambia, Inuka, ukalipime hekalu la Mungu, na
madhabahu, na hao wasujuduo humo. Na behewa iliyo nje ya hekalu uiache
nje wala usipime, kwa maana Mataifa wamepewa hiyo …”
Viongozi wa Israeli wa wakati huo wa Juni 1967 waliamua kuwapa
Waislamu “Kihalali” eneo hilo la mlima mtakatifu, ili waendelee
kulitumia kama sehemu ya ibada zao katika msikiti wao. Na kibali hicho
kilitimiza andiko linalosema; “Na
behewa iliyo nje ya hekalu uiache nje wala usiipime, kwa maana Mataifa
wamepewa hiyo, nao wataukanyaga mji mtakatifu miezi arobaini na miwili”. “… miezi arobaini na miwili”
ni miaka mitatu na nusu ambayo inahusu sehemu ya kipindi cha miaka saba
cha utawala wa Mpinga
Kristo hapa duniani, ambacho bado kiko mbele yetu – hakijatokea bado!
Kwa hiyo, ikiwa katika kipindi hicho kutakuwa na “hekalu na
Msikiti” kwa wakati mmoja, basi ina maana hekalu la tatu ambalo halipo
kwa sasa litajengwa!
Hii ina maana kwa mara ya kwanza tangu Israeli iwe Taifa mwaka
1948, vita vya Juni 1967 vilifungua mlango wa uwezekano mkubwa sana wa
ujenzi wa hekalu la tatu katika mlima mtakatifu, bila kuubomoa msikiti
uliopo! Ni jambo gani linalokupunguzia
Tazama ndani ya moyo wako, utayari wako ulionao wa kumtumikia
Mungu katika zamu yako, na katika eneo lako, je umepungua au umeongezeka?
Ikiwa utayari wako umepungua basi unahitaji kujipanga upya ndani
ya Bwana Yesu Kristo! Je,
umewahi kujiuliza Yesu Kristo akirudi sasa hivi – atakukuta katika
zamu yako ukifanya sehemu yako katika kuwapa watu chakula “kwa wakati
wake” ikiwa ina maana “kwa wakati wa Mungu”?
Je una cha kujitetea? Una kisingizio gani au sababu gani ya
kupunguza utayari wako ndani yako wa kumtumikia Mungu?
Mungu azidi kukuandaa juu ya ujio wa Yesu Kristo. Maranatha! |
|