Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma

Barua ya Mwezi Juni 2007                                                            Kutoka kwa Christopher na Diana Mwakasege


Bwana Yesu Asifiwe Sana!

Tunakusalimu katika jina la Yesu Kristo. Karibu katika kuisoma barua yetu hii ya mwezi huu ambayo ni mfululuzo wa pili katika kukujulisha na kukufundisha juu ya uhusiano uliopo kati ya kumtumikia Mungu na taifa la Israeli.

Katika barua ya kwanza katika mfululuzo huu tuliyoitoa mwezi uliopita tuliuliza maswali mawili muhimu nayo ni haya:

Swali la kwanza: je, unajua uhusiano uliopo kati ya wito wa kumtumikia Mungu katika nyakati hizi za mwisho na Taifa la Israeli?

Swali la kwanza: je, unajua ya kuwa usipomtumikia Mungu ipasavyo kuna uwezekano wa kuikosa mbingu?

Mwezi huu tunaendelea kuchambua kwa undani juu ya jambo hili.

Wakati ni muhimu katika uhusiano 
wa kumtumikia Mungu na kurudi kwa 
Yesu Kristo.

  Yesu Kristo alipokuwa anaelezea juu ya ujio wake wa kurudi kuja kulichukua Kanisa aliweka msisitizo sana katika wakati.

            Katika Mathayo Sura ya 24 Yesu Kristo amezungumza na kusisitiza juu ya wakati mara kumi na mbili kwa kutumia maneno tofauti – tofauti!

            Na ilipofika kuzungumzia juu ya watumishi wake, anataka  muda wake au wakati wake wa kurudi utakapofika, anatarajia awakute watumishi wake wakiendelea “kuwapa watu chakula kwa wakati wake”.

            Kwa “wakati wake” akiwa ana maana ya kuwa kuwapa watu chakula cha neno la Mungu katika wakati unaotakiwa! Kila mtu anatakiwa afanye jukumu linalomhusu, na wajibu unaomhusu, katika wakati unaotakiwa, huku akijua ya kuwa kurudi kwa Yesu Kristo kumekaribia sana!

            Kwa nini? Kwa sababu kujali ukaribu “wakati” wa kurudi wa Bwana Yesu Kristo ni muhimu sana – unapounganishwa na kupeleka chakula cha neno la Mungu kwa watu.

            Kwa Mfano; kwa kuwa hakuna aijuaye “siku ile wala saa ile” – neno la Mungu linasaidia kuwapa watu “utayari” wa kujua ya kuwa “wakati wa mavuno karibu”, na ya kwamba Yesu Kristo “yu karibu milangoni”.

            Lakini pia neno la Mungu linatuambia ya kuwa kurudi kwa Yesu Kristo kunategemea kuhubiriwa kwa “habari njema ya Ufalme … katika Ulimwengu wote” (Mathayo 24:14).

            Hii ikiwa na maana ya kwamba, ikiwa tunataka Yesu Kristo arudi haraka, basi ni muhimu kila mtu “kwa wakati wake”, ashike zamu ya utumishi wake ipasavyo, bila kuzembea wala kulegea! Kumbuka Biblia inasema; “Na alaaniwe mtu afanyaye kazi ya Bwana kwa ulegevu ….” (Yeremia 48:10).

            Tena ni lazima kila amtumikiaye Mungu katika ngazi yo yote ile, ajue hana muda wote anaodhani ya kuwa anao wa kumtumikia Mungu. Yesu Kristo alisema; “Imetupasa kuzifanya kazi zake yeye aliyenipeleka maadamu ni mchana; usiku waja asipoweza mtu kufanya kazi” (Yohana 9:4).

            Unataka siku ile Yesu Kristo atakaporudi akuambie nini kama mtumishi wake? Tafakari maneno yafuatayo;

“ … mtumwa (mtumishi) mwaminifu na mwenye akili …” (Mathayo 24:45).

“ … mtumwa (mtumishi) … mbaya …” (Mathayo 24:48).

“vema, mtumwa (mtumishi) mwema na mwaminifu; ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya bwana wako”

(Mathayo 25:21).

“Wewe mtumwa (mtumishi) mbaya na mlegevu …” (Mathayo 25:26).

“Na mtumwa (mtumishi) yule asiyefaa, mtupeni mbali katika giza la nje; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno” (Mathayo 25:30).

            Unataka maneno gani yawe yako kati ya hayo tuliyosoma hapa juu Yesu Kristo atakapokuwa “anawalipa” watu kwa utumishi ule waliomtumikia? Je, itakuwaje kwako ukijikuta unaikosa furaha ya mbingu kwa ajili ya kutokumtumikia Mungu kwa kujali “wakati wake”.

            Kwa nini uikose mbingu kwa kutokumtumikia Mungu ipasavyo kwa “wakati wake”?

Tunaujua “wakati wake” kwa
kuangalia nini?

            “Wakati wake” maana yake “wakati wa Mungu” Si wakati wetu- Hapana! Bali wakati wake!

            Mungu anataka tuwape watu chakula cha neno la Mungu kwa wakati wake na siyo kwa wakati wetu sisi.

            Mungu anajua watu wanahitaji chakula kipi cha neno lake, na kwa wakati wake upi! Na ndilo analotaka watumishi wake wajue, na ndilo analotaka walifuate – kuwapa watu chakula cha neno la Mungu kwa wakati wake!

            Watumishi wanapojichagulia chakula cha neno lolote la Mungu na kuwapa watu kwa wakati wao na si wakati wa Mungu – ni kwenda kinyume na mapenzi ya Mungu!

            Kwa kuwa hakuna aijuaye siku ile na saa ile itakuwa lini, Yesu Kristo alihakikisha anawapa watumishi wake mahali pa kuangalia ili wapate kujua ukaribu wa wakati wa ujio wake.

            Kabla Yesu Kristo hajatoa angalizo lake kwa watumishi wake katika siku hizi za mwisho juu ya kujali “wakati wake” katika kuwapa watu neno la Mungu, tunaona kwanza akitoa angalizo la  jambo la kutokuijua siku ile wala saa ile!

            “Walakini habari ya siku ile na saa ile hakuna aijuaye, hata malaika walio Mbinguni, wala Mwana, ila Baba peke yake. Kwa maana kama vile ilivyokuwa siku za Nuhu, … kama vile siku zile zilizokuwa kabla ya Gharika … ndivyo kutakavyokuwa kuja kwake Mwana wa Adamu, wakati ule … mmoja atwaliwa, mmoja aachwa” (Mathayo 24: 36 – 41).

            Hili lilikuwa angalizo muhimu, ili mtu awaye ye yote asije akaweka tarehe na saa ya “Siku ile na saa ile”. Lakini kwa kuwa kujua ukaribu wa siku ile na saa ile ni muhimu kwa kila mtu nasi kwa watumishi wa Mungu tu – Yesu Kristo alihakikisha anatueleza mahali pa kuangalia juu ya ukaribu wa wakati wa ujio wake!

            Yesu Kristo alisema hivi juu ya jambo hili. “Basi kwa mtini jifunzeni mfano; tawi lake likiisha kuchipuka na kuchanua majani, mwatambua ya kuwa wakati wa mavuno ukaribu; nanyi kadhalika, myaonapo hayo yote, tambueni ya kuwa yu karibu, milangoni” (Mathayo 24: 32 – 33).

            Yesu Kristo alitaka na anataka tujue ya kuwa ili kufahamu ya kuwa “yu karibu milangoni” akiwa na mama ya “ukaribu wa kurudi kwake” – basi ni muhimu tujifunze kutoka kwenye mabadiliko yanayotokea katika mti wa mtini!

            Mwezi huu tunaishia hapa. Soma barua yetu ya mwezi ujao ili upate mambo tuliyoyatayarisha katika kuhitimisha maelezo juu ya uhusiano uliopo kati ya kumtumikia Mungu na taifa la Israeli.

            Tuzidi kuombeana.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.