|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Tunaamini Mungu anaendelea kukusaidia. Tena tunamshukuru Mungu
kwa kukupa nafasi ya kusoma barua yetu ya mwezi huu.
Barua hii ni mwanzo wa mfululizo wa barua tatu tunazolenga
kukushirikisha juu ya uhusiano uliopo kati ya kumtumikia Mungu na taifa
la Israeli. Tunaamini utapata mengi ya kukusaidia.
Maswali
mawili ya msingi: Swali la Kwanza:
Je,
unajua uhusiano uliopo kati ya wito wa kumtumikia Mungu katika nyakati
hizi za siku za mwisho na Taifa la Israeli? Swali la Pili: Je, unajua ya kuwa usipomtumikia
Mungu ipasavyo kuna uwezekano wa kuikosa Mbingu? Swali hili la pili ndilo
linalotufanya tutoe angalizo hili kwa wale wanaomtumikia Mungu katika
kizazi hiki. Angalizo lenyewe ni hili – ya kwamba – usipomtumikia Mungu ipasavyo kuna
uwezekano wa kuikosa Mbingu!
Ni kitu gani kinatufanya tufikie uamuzi huu wa kutoa angalizo
hili kwa wanaomtumikia Mungu?
Haya ni baadhi ya matokeo ya kuanza kuisoma upya Biblia ili kuona
jinsi inavyoioanisha nchi ya Israeli na Kanisa. Mwanzoni
mwa mwezi Mei mwaka 2007 tulipata nafasi ya kuitembelea Nchi ya Israeli
kwa mara ya kwanza katika maisha yetu. Safari hiyo tuliyoongozana na
wenzetu kadhaa, – jumla tukiwa watu arobaini, – iliweka ndani yetu
hamu mpya ya kutaka kujua umuhimu wa uhusiano wa Taifa la Israeli kwa
Kanisa, kwa kuisoma Biblia kwa upya; tukitaka kujua inasema nini juu ya
jambo hili.
Jambo mojawapo tuliloliona kwa upya, na tunalotaka kukushirikisha
hapa, ni lile la uhusiano uliopo kati ya wito wa kumtumikia Mungu na
Taifa la Israeli; na jambo hili la uwezekano wa mtumishi wa Mungu
kuikosa Mbingu kwa kutokumtumikia Mungu ipasavyo.
Je unajua kitu alichosema Yesu Kristo juu ya mtumishi wake
atakayemkuta hafanyi mapenzi ya Mungu “kwa
wakati wake” katika kuwapa watu wake “Posho
au chakula”?
Hebu kwanza tuangalie Yesu Kristo alisema nini juu ya ujio wake
wa kulichukua Kanisa – alisema hivi: “Kesheni
basi; kwa maana hamjui ni siku ipi atakayokuja Bwana wenu. Lakini
fahamuni neno hili; kama mwenye nyumba angalijua ile zamu mwivi
atakayokuja, angalikesha, wala asingeliacha nyumba yake kuvunjwa. Kwa
sababu hiyo ninyi nanyi jiwekeni tayari; kwa kuwa katika saa msiyodhani
Mwana wa Adamu yuaja” (Mathayo 24:42 – 44). Baada
ya kusema maneno hayo – ndipo Yesu Kristo alipoweka angalizo hili kwa
watumishi wa Mungu.
“Ni nani basi yule
mtumwa mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya nyumba
yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumwa yule, ambaye bwana
wake ajapo atamkuta akifanya hivyo. Amini, nawaambieni, atamweka juu ya
vitu vyake vyote”.
“Lakini mtumwa yule mbaya akisema moyoni mwake, Bwana wangu
anakawia; akaanza kuwapiga wajoli wake, na kula na kunywa pamoja na
walevi; bwana wake mtumwa huyo atakuja siku asivyodhani, na saa asiyojua,
atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wanafiki;
ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno” (Mathayo
24:45 – 51).
Ukitaka kutafakari angalizo hili la Yesu Kristo kwa uzito na
umuhimu unaostahili – basi ondoa neno “mtumwa”
weka badala yake neno “mtumishi”.
Hii ni kwa sababu neno mtumwa hapa limetumika likiwa na maana ya
mtumishi!
Ukitafakari maneno haya ya Bwana Yesu Kristo utaona ya kuwa hili
ni angalizo linalokwenda moja kwa moja kwa watumishi wa Mungu!
Kwa Mfano – hebu soma maneno haya kwa upya; “Ni nani basi mtumishi mwaminifu mwenye akili, ambaye bwana wake alimweka juu ya
nyumba yake, awape watu chakula kwa wakati wake? Heri mtumishi yule, ambaye bwana wake ajapo atamkuta akifanya hivyo”.
Ni dhahiri ya kwamba Chanzo cha watumishi wa Mungu kupoa kiroho na kuzembea katika
kazi ya Mungu ya kuwapa “watu chakula kwa wakati wake” ni kule kutokujali muda wa ukaribu
wa ujio wa Bwana Yesu kuja kulichukua Kanisa!.
Yesu Kristo alisema; “bwana wake mtumishi huyo atakuja siku
asiyodhani, na saa asiyojua, atamkata vipande viwili, na kumwekea fungu
lake pamoja na wanafiki; ndiko kutakuwako kilio na kusaga meno”.
Ukiyasoma maneno hayo kwa jinsi yalivyoandikwa na Luka Mtakatifu
utaona yanasomeka hivi; “bwana
wake mtumwa huyo atakuja siku asiyodhani na saa asiyojua, atamkata
vipande viwili, na kumwekea fungu lake pamoja na wasioamini” (Luka
12:46).
Wasomaji wa Biblia wanajua ya kuwa fungu la wasioamini baada ya
kufa au Yesu Kristo atakaporudi – ni
Motoni, au Jehanam, au Ziwa la Moto!
Kwa hiyo mtumishi wa Mungu asipojali muda wa ukaribu wa Ujio wa
kurudi kwa Yesu Kristo kuja kulichukua kanisa, na akaacha kuwapa watu
chakula kwa wakati wake; -
Yesu Kristo akirudi atamwekea fungu lake pamoja na wasioamini – ikiwa
na maana ya kuwa mtumishi huyo atahukumiwa
sawasawa na wasioamini! Hii
maana yake mtumishi wa Mungu anaweza kuikosa Mbingu kwa sababu hakuwa
makini kujali uhusiano uliopo
kati ya ukaribu wa muda wa ujio wa Yesu Kristo kulichukua Kanisa na wito
alionao wa kumtumikia Mungu katika nyakati hizi. Una Sehemu gani katika kuwapa
Ikiwa utumishi wa kutumikia Mungu katika nyakati hizi za sasa una
uhusiano mkubwa na ujio wa kurudi kwa Yesu – basi vile vile lazima
utumishi huu una uhusiano mkubwa na matukio yaliyotabiliwa kutokea juu
ya Taifa la Israeli katika siku hizi za mwisho.
Lakini kabla – hatujaangalia uhusiano
huu kwa undani – hebu tuchambue kwanza sehemu ulinayo katika
kuwapa “watu chakula” kwa “wakati wake”. Kujua – huku kutaweka
ndani yako umuhimu mpya ndani yako wa kujali ukaribu wa muda wa ujio wa
kurudi kwa Yesu Kristo, katika jambo unalolifanya kwa sasa.
Tukiuangalia mfano wa kula chakula hotelini au nyumbani, utakuwa
unaelewa ya kuwa wale waliohusika na kuhakikisha umepata “chakula”
kwa “wakati wake” ni wengi sana! Si kazi ya mtu mmoja, bali ni
mahusiano ya kikazi yanayohusisha watu wengi sana.
Kwa mfano; kuna anayekupa chakula mezani, kuna waliohusika na
kupika, kuna walionunua chakula hicho, kuna waliohusika na kulima mazao
ya chakula hicho, kuna madreva waliohusika, kuna watoa fedha, kuna
waliokinunua toka kwa wakulima na kukiuza kwa walaji, kuna waliohusika
na stoo, nakadhalika.
Kwa hiyo unapoona umewekewa chakula mezani na unakula kwa
“wakati wake” ujue ni watu wengi sana sana wamehusika!
Na inapokuja kwenye “Chakula”
cha “Neno la Mungu” ni
hivyo hivyo. Watu wanapojikuta wanakula chakula cha neno la Mungu “kwa wakati wake” – basi wajue ni watu wengi sana sana
wanahusika.
Inasikitisha kuona ya kuwa kuna watu wanahusika na kuwapa watu
chakula cha neno la Mungu katika ngazi mojawapo ya mlolongo wa Utumishi
huu – lakini – hawajui ya kuwa wao pia ni watumishi wa Mungu. Na kwa
sababu hiyo wanajiondoa kwenye orodha ya watumishi wa Mungu, kwa kuwa
wanajiona si wahubiri basi wao si watumishi wa Mungu! Hawajui ya kuwa
kwa kufanya wanachofanya kuwasaidia wahubiri, na kwa ajili hiyo wao pia
wanamtumikia Mungu kwa njia hiyo!
Ukiutazama utumishi huu kwa njia hii ni dhahiri ya kwamba
mtumishi aliyepewa kufikisha chakula cha neno la Mungu kwa walaji “kwa
wakati wake” – haifanyi kazi hii peke yake! Ni watu wengi sana sana
wanahusika katika mlolongo wa utumishi huu hadi neno la Mungu lifike kwa
anayetakiwa kulipata.
Je, wewe unahusika katika nafasi ipi ndani ya mtiririko huu wa
kufikisha chakula cha neno la Mungu kwa walaji kwa wakati wake? Je, wewe
ni mtoa sadak? ni mwombaji? ni mwanakamati? ni mhudumu? ni mlinzi? ni
fundi umeme? ni fundi mitambo? ni mwimbaji? ni mfanya usafi? mali yako
yoyote imetumika? ni mtoa kibali? ni mjenzi? ni mtunza watumishi?,
nakadhalika.
Kwa vyo vyote vile unavyohusika kwa sasa, au unavyojisikia moyoni
mwako kuhusika katika kupeleka neno la Mungu kwa watu kwa wakati wake; -
ujue unahusika na angalizo – hili la Bwana Yesu Kristo!
Usije ukajikuta umeikosa mbingu kwa sababu ya kuzembea katika
zamu yako, kwa kuwa tu umeshindwa kuihusisha zamu yako katika wajibu wa
utumishi wako, pamoja na ukaribu wa ujio wa kurudi kwa Yesu Kristo
kulichukua Kanisa lake!
Kwa mwezi huu tunaishia hapa. Usikose kusoma barua yetu ya mwezi
ujao ili uweze kujifunza zaidi juu ya jambo hili.
Mungu akubariki sana. |
|