|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Ndani ya mfululizo wa barua zetu za miezi miwili iliyopita
tumekuwa tukikuelezea umuhimu wa maombi yako unapoombea toka kwenye
nafasi ya mfalme na kuhani katika Kristo. Tulikupa mifano ya maombi ya nabii Eliya katika kukufundisha
juu ya jambo hili. Mambo mawili tuliyoyaona katika mfano huu ni kwamba:
kuomba au kutokuomba kwa nabii Eliya ndiko kulikokuwa na uamuzi wa
mwisho juu ya 1. Kunyesha au
kutokunyesha kwa mvua katika kipindi cha utumishi wake, na 2. ndiko
kulikokuwa na uamuzi wa mwisho juu ya kuendelea au kutokuendelea kwa
malumbano ya kidini katika kizazi chake! Ni dhahiri pia ya kuwa heshima ya Mungu wake katika eneo
hilo yalitegemea maombi ya nabii Eliya wakati ule. Mwezi huu tuangalie
mfano wa maombi ya nabii Musa. Unaposoma habari iliyoko katika kitabu cha Kutoka 17:8-13
utaona ya kuwa; kuomba au kutokuomba kwa Musa ndiko kulikokuwa na uamuzi
wa mwisho juu ya matokeo ya vita iliyotokea kati ya wana wa Israeli
wakiongozwa na Yoshua walipopigana na Waamaleki. Vita hivi vilitokea huko Refidimu. Yoshua alipokuwa
anaongoza jeshi kwenda kupigana na Waamaleki, Musa akiwa na Haruni na
Huri alipanda mlimani “kuombea” hiyo vita. Biblia inatuambia katika Kutoka 17:11 ya kuwa; “Ikawa
Musa alipoinua mkono wake, Israeli walishinda; na alipoushusha mkono
wake, Amaleki walishinda” “Kuinua mikono”
kwa Musa ilikuwa ni ishara ya kuomba kwake juu ya vita iliyokuwa
inaendelea kati ya wana wa Israeli na Waamaleki. Kwa hiyo tunaweza
kusema; “Ikawa, Musa alipoomba, Israeli
walishinda, na alipoacha kuomba, Amaleki alishinda” Ni kama vile maombi ya Musa ndiyo yaliyokuwa yanamfanya
Mungu apigane upande wa wana wa Israeli, kwa kuwa tunasoma ya kuwa Musa
alipoinua mkono wake, au alipoomba Israeli walishinda, na alipoushusha
mkono wake, au alipoacha kuomba, Amaleki walishinda. Umewahi kujiuliza ya kuwa kwa nini Mungu ategemee na asubiri
maombi ya Musa ili kuwasaidia watu wake – wana wa Israeli wapate
kushinda vita walivyokuwanavyo? Kwa nini Mungu asiwasaidie tu bila
kusubiri maombi ya Musa? Unapoisoma habari hii unaona ya kuwa kama Musa asingeomba ni
wazi ya kuwa Yoshua asingeshinda vita hivyo – bali angeshindwa! Kutoka 17:13 inasema; “Yoshua
akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga”. Kwa hiyo kilichofanya upanga wa Yoshua uwe “mkali”
au uwe “butu” ni kuomba au kutokuomba kwa Musa. Alipoomba upanga wa
Yoshua ulikuwa unakuwa mkali na kushinda vita, lakini Musa alipokuwa
anaacha kuomba, upanga wa Yoshua ulikuwa unakuwa butu na kufanya Yoshua
ashindwe vita! Tunajifunza nini hapa? Waefeso 6:17 inasema “na
upanga wa Roho…….ni neno la Mungu”. Kwa hiyo tunaweza kusema “kushinda”
au “kushindwa” kwa “neno
la Mungu” linalohubiriwa au kufundishwa au kusemwa – kunategemea
maombi yanayolisindikiza hilo neno! Hili linaonekana wazi tunapolinganisha matokeo kati ya neno
la Mungu linalohubiriwa katika ibada za Jumapili na lile linalohubiriwa
katika mikutano ya injili au semina za neno la Mungu. Kiwango cha “kuombewa”
kwa mikutano ya injili ni kikubwa kuliko kiwango cha kuombewa kwa ibada
– na kwa ajili hiyo ushindi wa neno la Mungu katika mikutano ya injili
ni mkubwa kuliko ule wa katika ibada. Kwa hiyo kuombea au kutoombea neno la Mungu linalopelekwa
mahali fulani ndiko kunakoamu matokeo ya kushinda au kushindwa kwa neno
hilo! Ndivyo ilivyokuwa Musa alipopanda mlimani kuomba! Heshima ya
wanajeshi wa Israeli na heshima ya Mungu wao vilitegemea maombi ya Musa!
(What a position of authority God has given His people through prayer!) Fikiria ungekuwa upande wa jeshi la Waamaleki walipokuwa
wanapigana na wana wa Israeli na ukatambua ya kuwa kuna wakati walikuwa
wanakushinda, na kuna wakati ulikuwa unawashinda – je, ungechukua
hatua gani? Ni wazi ungetaka kujua siri ya mabadiliko hayo ya kushindwa
na kushinda kwao kulikokuwa kunatokea wakati wa vita! Fikiria utambue ya kuwa kushinda au kushindwa wa wana wa
Israeli kulitegemea “kuomba na
kuendelea kuomba au kutokuomba” kwa Musa – je, ungechukua hatua
gani? Ni wazi ya kwamba ungetafuta mbinu zote utakazopata kuzuia
Musa asiombe wala asiendelee kuomba! Kwa nini? Kwa sababu ingawa vita
vilikuwa vinapiganwa bondeni lakini mwamuzi wa mwisho juu ya nani
ashinde vita hivyo ni Musa aliyekuwa mlimani akiombea vita hivyo! Kwa hiyo tunaweza kusema ya kuwa ikiwa Shetani anataka
kuzuia neno la Mungu lisiwe na nguvu ya kushinda makanisani, anachofanya
ni kuzuia maombi yasifanyike ya kutosha makanisani ili kulisindikiza
hilo neno! Ikiwa neno la Mungu halina nguvu kanisani kwako unaposali,
na halileti ushindi uliotarajiwa, basi ina maana hakuna anayeliombea vya
kutosha! Na je, mtu huyo ni wewe uliyepaswa kuomba na sasa huombi
ipasavyo? Ndio maana Mungu anapokupa mzigo wa kuwaombea watumishi wa
Mungu, tafadhali sana, usipuuzie wala usilegee wala usibebe mzigo huu
kivivu. Hii ni kwa sababu kufanikiwa au kutofanikiwa kwa neno la Mungu
linalotoka katika vinywa vya watumishi hao kunategemea kiwango cha
maombi wanachoombewa kila siku. Kwa mwezi huu tunaishia hapa. Lakini usiache kuisoma barua
yetu tutakayokuandikia mwezi ujao – maana tutakuletea mfano wa maombi
ya Ibrahimu na kuhitimisha ujumbe huu muhimu. Mungu azidi kukubariki. |
|