Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma

Barua ya Mwezi Oktoba 2007                                                            Kutoka kwa Christopher na Diana Mwakasege


Tunakusalimu katika Jina la Yesu Kristo.

Ndani ya mfululizo wa barua zetu za miezi miwili iliyopita tumekuwa tukikuelezea umuhimu wa maombi yako unapoombea toka kwenye nafasi ya mfalme na kuhani katika Kristo.

Tulikupa mifano ya maombi ya nabii Eliya katika kukufundisha juu ya jambo hili. Mambo mawili tuliyoyaona katika mfano huu ni kwamba: kuomba au kutokuomba kwa nabii Eliya ndiko kulikokuwa na uamuzi wa mwisho juu ya 1. Kunyesha au kutokunyesha kwa mvua katika kipindi cha utumishi wake, na 2. ndiko kulikokuwa na uamuzi wa mwisho juu ya kuendelea au kutokuendelea kwa malumbano ya kidini katika kizazi chake!

Ni dhahiri pia ya kuwa heshima ya Mungu wake katika eneo hilo yalitegemea maombi ya nabii Eliya wakati ule. Mwezi huu tuangalie mfano wa maombi ya nabii Musa.

Unaposoma habari iliyoko katika kitabu cha Kutoka 17:8-13 utaona ya kuwa; kuomba au kutokuomba kwa Musa ndiko kulikokuwa na uamuzi wa mwisho juu ya matokeo ya vita iliyotokea kati ya wana wa Israeli wakiongozwa na Yoshua walipopigana na Waamaleki.

Vita hivi vilitokea huko Refidimu. Yoshua alipokuwa anaongoza jeshi kwenda kupigana na Waamaleki, Musa akiwa na Haruni na Huri alipanda mlimani “kuombea” hiyo vita.

Biblia inatuambia katika Kutoka 17:11 ya kuwa; “Ikawa Musa alipoinua mkono wake, Israeli walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda”

“Kuinua mikono” kwa Musa ilikuwa ni ishara ya kuomba kwake juu ya vita iliyokuwa inaendelea kati ya wana wa Israeli na Waamaleki. Kwa hiyo tunaweza kusema; “Ikawa, Musa alipoomba, Israeli walishinda, na alipoacha kuomba, Amaleki alishinda”

Ni kama vile maombi ya Musa ndiyo yaliyokuwa yanamfanya Mungu apigane upande wa wana wa Israeli, kwa kuwa tunasoma ya kuwa Musa alipoinua mkono wake, au alipoomba Israeli walishinda, na alipoushusha mkono wake, au alipoacha kuomba, Amaleki walishinda.

Umewahi kujiuliza ya kuwa kwa nini Mungu ategemee na asubiri maombi ya Musa ili kuwasaidia watu wake – wana wa Israeli wapate kushinda vita walivyokuwanavyo? Kwa nini Mungu asiwasaidie tu bila kusubiri maombi ya Musa?

Unapoisoma habari hii unaona ya kuwa kama Musa asingeomba ni wazi ya kuwa Yoshua asingeshinda vita hivyo – bali angeshindwa!

Kutoka 17:13 inasema; “Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake kwa ukali wa upanga”.

Kwa hiyo kilichofanya upanga wa Yoshua uwe “mkali” au uwe “butu” ni kuomba au kutokuomba kwa Musa. Alipoomba upanga wa Yoshua ulikuwa unakuwa mkali na kushinda vita, lakini Musa alipokuwa anaacha kuomba, upanga wa Yoshua ulikuwa unakuwa butu na kufanya Yoshua ashindwe vita!

Tunajifunza nini hapa? Waefeso 6:17 inasema “na upanga wa Roho…….ni neno la Mungu”. Kwa hiyo tunaweza kusema “kushinda” au “kushindwa” kwa “neno la Mungu” linalohubiriwa au kufundishwa au kusemwa – kunategemea maombi yanayolisindikiza hilo neno!

Hili linaonekana wazi tunapolinganisha matokeo kati ya neno la Mungu linalohubiriwa katika ibada za Jumapili na lile linalohubiriwa katika mikutano ya injili au semina za neno la Mungu.

Kiwango cha “kuombewa” kwa mikutano ya injili ni kikubwa kuliko kiwango cha kuombewa kwa ibada – na kwa ajili hiyo ushindi wa neno la Mungu katika mikutano ya injili ni mkubwa kuliko ule wa katika ibada.

Kwa hiyo kuombea au kutoombea neno la Mungu linalopelekwa mahali fulani ndiko kunakoamu matokeo ya kushinda au kushindwa kwa neno hilo!

Ndivyo ilivyokuwa Musa alipopanda mlimani kuomba! Heshima ya wanajeshi wa Israeli na heshima ya Mungu wao vilitegemea maombi ya Musa! (What a position of authority God has given His people through prayer!)

Fikiria ungekuwa upande wa jeshi la Waamaleki walipokuwa wanapigana na wana wa Israeli na ukatambua ya kuwa kuna wakati walikuwa wanakushinda, na kuna wakati ulikuwa unawashinda – je, ungechukua hatua gani?

Ni wazi ungetaka kujua siri ya mabadiliko hayo ya kushindwa na kushinda kwao kulikokuwa kunatokea wakati wa vita!

Fikiria utambue ya kuwa kushinda au kushindwa wa wana wa Israeli kulitegemea “kuomba na kuendelea kuomba au kutokuomba” kwa Musa – je, ungechukua hatua gani?

Ni wazi ya kwamba ungetafuta mbinu zote utakazopata kuzuia Musa asiombe wala asiendelee kuomba! Kwa nini? Kwa sababu ingawa vita vilikuwa vinapiganwa bondeni lakini mwamuzi wa mwisho juu ya nani ashinde vita hivyo ni Musa aliyekuwa mlimani akiombea vita hivyo!

Kwa hiyo tunaweza kusema ya kuwa ikiwa Shetani anataka kuzuia neno la Mungu lisiwe na nguvu ya kushinda makanisani, anachofanya ni kuzuia maombi yasifanyike ya kutosha makanisani ili kulisindikiza hilo neno!

Ikiwa neno la Mungu halina nguvu kanisani kwako unaposali, na halileti ushindi uliotarajiwa, basi ina maana hakuna anayeliombea vya kutosha! Na je, mtu huyo ni wewe uliyepaswa kuomba na sasa huombi ipasavyo?

Ndio maana Mungu anapokupa mzigo wa kuwaombea watumishi wa Mungu, tafadhali sana, usipuuzie wala usilegee wala usibebe mzigo huu kivivu. Hii ni kwa sababu kufanikiwa au kutofanikiwa kwa neno la Mungu linalotoka katika vinywa vya watumishi hao kunategemea kiwango cha maombi wanachoombewa kila siku.

Kwa mwezi huu tunaishia hapa. Lakini usiache kuisoma barua yetu tutakayokuandikia mwezi ujao – maana tutakuletea mfano wa maombi ya Ibrahimu na kuhitimisha ujumbe huu muhimu. Mungu azidi kukubariki.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.