|
|
| ||
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
|
Tunakusalimu
katika Jina la Yesu Kristo,
Umepewa
nafasi katika ulimwengu wa roho ili uitumie
Ndiyo!
Ndivyo ilivyo wala usishangae! Ikiwa
umeokoka, basi ujue ya kuwa unayo nafasi katika ulimwengu wa roho,
unayotakiwa uitumie ikusaidie kufanikiwa katika nafasi uliyonayo
katika ulimwengu wa kimwili. Kwa
mantiki hii, maana yake Mungu anapokupa nafasi katika ulimwengu wa
kimwili, anataka uitumie kufanikisha makusudi yake yaliyomo katika
kuuleta ufalme wake hapa duniani.
Aina
mojawapo ya hizi nafasi ni hizi za kufanyika wafalme na makuhani kwa
Mungu wetu. Imeandikwa hivi: “Nao
waimba wimbo mpya wakisema,
wastahili wewe kukitwaa hicho kitabu na
kuzifungua muhuri zake; kwa kuwa ulichinjwa,
ukamnunulia Mungu kwa damu yako watu wa
kila kabila na lugha na jamaa na taifa,
ukawafanya kuwa ufalme na makuhani
kwa Mungu wetu; nao wanamiliki juu
ya nchi”
(Ufunuo wa Yohana 5:9,10) Haya
maneno “ukawafanya kuwa
ufalme na makuhani kwa Mungu wetu…..”, yanasomeka kwa sura
tofauti unapoyasoma toka katika tafsiri ya kiingereza ya King
James Version. Katika tafsiri hii ya kiingereza yanasomeka hivi: “
And has made us unto our God kings and priests….”
Maneno
hayo kwa Kiswahili tunayatafsiri hivi “Na
ametufanya sisi kwa Mungu wetu tuwe wafalme na makuhani…..” Ninalotaka
ulione hapa ni maneno haya “Wafalme
na Makuhani”. Hizi ni nafasi mbili ambazo Yesu Kristo anampa mtu
anayemwokoa kwa kumnunua kwa damu yake ya thamani.
Nafasi
hizi mbili zinauhusiano wa karibu sana na nafasi ambayo mtu anakuwa
nayo anapookolewa au baada ya kuokolewa. Nafasi ambayo anakuwa nayo
ndani ya kabila, au
katika lugha, au katika jamaa,
(ukoo) au katika taifa.
Ukiusoma
mstari huu wa Ufunuo wa Yohana 5:9,10 kuanzia mstari wa 9 na ndipo
uende mstari wa 10, si rahisi sana kuliona jambo hili ninalotaka
ulione hapa. Lakini
Roho Mtakatifu aliponiongoza kuusoma na kuutafakari kwa kuanzia mstari
wa 10 na halafu wa 9 – nikaona waziwazi alichotaka nikione ndani
yake.
Angalia!
Anawafanya wawe wafalme
na makuhani
wale ambao amewanunua wakiwa ndani ya kabila zao, lugha zao, jamaa zao
na taifa lao!
Wanazo
nafasi zao katika ulimwengu wa kimwili ndani ya kabila zao, na ndani
ya lugha zao, na ndani ya jamaa zao, na ndani ya taifa lao. Lakini
hapo hapo anaamua kuwapa nafasi za kuwa wafalme na makuhani katika
ulimwengu wa roho!
Kwa
hiyo, mara tu wanapookoka wanajikuta wamepewa nafasi zingine katika
ulimwengu wa roho, wakati bado wanazo nafasi pia katika ulimwengu wa
kimwili. Mtu
anapookoka anajikuta anaishi maisha ya aina mbili kwa wakati mmoja (2
Wakorintho 5:15,16,17). Pia, anajikuta anaishi katika falme mbili kwa
wakati huo huo ( Yohana 14:30).
Mtu
ni roho, anayo nafsi na anaishi katika mwili (1 Wathesalonike 5:23).
Mungu amemuumba mtu kwa namna ambayo anatakiwa awe na uwezo wa kuishi
kwa mafanikio katika ulimwengu wa kiroho na katika ulimwengu wa kiroho
kwa wakati mmoja!
Ukiangalia
mistari hii ya Ufunuo wa Yohana 5:9,10 utaona ya kuwa Mungu
anamwezesha mtu katika Yesu Kristo ashike nafasi mbili katika ulimwengu
wa roho wakati pia katika ulimwengu wa kimwili anazo nafasi au
katika kabila; au katika lugha; au katika jamaa (ukoo wake)yake; na au
katika taifa lake!
Kusudi
mojawapo la Bwana Yesu kutoa nafasi hizo zilizoko katika ulimwengu wa
roho kwa watu wake, ni ili waweze kufanikiwa katika maeneo yote
yanayowahusu ya ulimwengu wa roho na yale yanayowahusu ya ulimwengu wa
kimwili.
Hivi
ndivyo mtu alivyoumbwa – ya kwamba, kwa
wakati huo huo aweze kuishi katika ulimwengu wa kiroho na ule
ulimwengu wa kimwili, bila kikwazo cho chote.
Dhambi
ilipoingia kwa mwanadamu wa kwanza, alipoteza nafasi aliyokuwa nayo
katika ulimwengu wa roho. Ndio maana katika kitabu cha Mwanzo 2:9
tunaona Mungu akimwita Adamu, akisema, “Uko
wapi”.
Mungu
hakumuuliza Adamu “unafanya
nini”, bali alimuuliza “uko
wapi”! Hii
ni kwa sababu, anachofanya mtu na anavyoishi na anavyozungumza –
vinategemea nafasi aliyonayo! Hii inahusu pia uhusiano wa mtu na Mungu
– unagusa nafasi kwanza
kabla ya matendo yake!
Kwa
hiyo Mungu anapomtembelea mtu, au anapotembelea nchi, - anaangalia kwanza
nafasi ambayo mtu wake, au watu wake,
wameishika katika ulimwengu wa roho na ulimwengu wa kimwili kabla
ya kuangalia matendo yao.
Kwa
mantiki hiyo ni rahisi kuelewa umuhimu wa nafasi ambayo mtu anapewa
katika ulimwengu wa roho wakati anapookoka!
Waefeso
2:6 inasema hivi juu ya kinachotokea mtu anapookoka: “
Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa
roho, katika Kristo Yesu”. Maana
yake nini kuketi “pamoja
naye katika ulimwengu wa roho katika Kristo Yesu?” Waefeso
1:19, 20 inatuelezea juu ya nguvu za Mungu zilizomfufua Yesu Kristo
kutoka kwa wafu, ndizo pia zilizomo ndani yetu baada ya kuzipokea
wakati tulipokuwa tunaokoka!
Maneno
hayo yanasema hivi: “na
ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa
kadri ya utendaji wa nguvu za uweza wake; aliotenda katika Kristo
alipomfufua katika wafu, akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu
wa roho”.
Warumi
8:11 inaeleza wazo hili hili inaposema “Lakini,
ikiwa Roho wake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu…. Huyo
Roho wa ufufuo anayekaa ndani yetu – anafanya ndani yetu jambo lile
lile alilofanya kwa Yesu alipomfufua kwa wafu! …. Alifanya jambo
gani? Waefeso 2:6 inasema; “akatufufua
pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho katika
Kristo Yesu”.
Waefeso
1:21 inatueleza zaidi kuhusu nafasi hiyo tuliyoketi pamoja na Kristo
katika ulimwengu wa roho inaposema: “juu
sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila
jina litajwalo, wala si ulimwengu humu tu, bali katika ule ujao pia”.
Unaposoma
yaliyoandikwa katika Wakolosai 1:13, na kuyaunganisha na yaliyoandikwa
katika Waefeso 2:6, na yale ya Waefeso 1:19 – 21; utaona ya kuwa mtu
anapookoka, si tu kwamba anakuwa mtoto wa Mungu, bali pia anaingizwa
katika uongozi wa juu wa serikali ya ufalme wa Mungu! Umelipata hili?
Unapookoka unaingizwa katika uongozi wa juu wa Serikali ya Ufalme wa
mbinguni. Wakolosai
1:13 inasema hivi juu ya kile kinachotokea tunapookoka ya kwamba: “Naye
alituokoa katika nguvu za giza, akatuhamisha na kutuingiza katika
ufalme wa Mwana wa pendo lake”.
Kwa
hiyo basi, ni muhimu tujue na tuamini na kuupokea ukweli huu ya kuwa
– Tunapookoka si tu kwamba tunazaliwa mara ya pili na kuingizwa
katika familia ya Mungu,
na kuwa ndugu moja tulio warithi pamoja na Kristo; lakini pia
tunapookoka tunaingizwa katika serikali
ya ufalme wa Mungu, na kuwa wamiliki
na watawala pamoja na Kristo!
Ndiyo!
Tunapookoka tunafanyika “Wafalme
na Makuhani” kufuatana na Ufunuo wa Yohana 5:10. Hii ikiwa na
maana ya kuwa tunapewa nafasi za utawala katika ulimwengu wa roho
katika “nafasi” ambazo
Yesu ametupa “kuketi”
pamoja naye.
Hizi
nafasi zinatupa kuwa wamiliki na watawala juu ya “ufalme
wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala
si ulimwengu humu tu, bali katika ulimwengu ujao pia” ….tena…..
“juu ya vitu vyote …..”
(Waefeso 1:21,22).
Unaliona
jambo hili? Ina maana wakati una nafasi yako katika jamii katika
ulimwengu wa kimwili; Mungu anakupa pia nafasi zingine za kiutawala
katika ulimwengu wa roho juu ya eneo hilo! Yesu
anataka uzitumie nafasi hizi alizokupa katika ulimwengu wa roho
kwa kiwango ambacho zitakufanikisha katika nafasi uliyonayo katika
ulimwengu wa kimwili – katika kabila lako, katika lugha yako, katika
ukoo wako na katika taifa lako!
Fahamu
hili na ukumbuke daima ya kwamba: Mungu anaitaka nafasi uliyonayo
katika ulimwengu wa kimwili ili aitumie katika kulitimiza kusudi lake
alilokupa katika nafasi zake alizokuweka katika ulimwengu wa roho. Tuzidi
Kuombeana. Christopher
na Diana Mwakasege |
|