Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
JIFUNZE KUSAMEHE NA KUSAHAU


Wiki ya Pili

TABIA YA MUNGU YA KUSAMEHE NDANI YAKO

            Ulipompokea Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yako, ulipokea tabia ya aina gani?

"  Bali wote waliompokea (Kristo) aliwapa uwezo wa  kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale waliaminio jina lake; waliozaliwa, si kwa damu, wala si kwa mapenzi ya mwili, wala si kwa mapenzi ya mtu, bali kwa Mungu." (Yohana 1:12,13)

            Ulipozaliwa mara ya pili kwa Neno la Kristo ulifanyika kuwa mtoto wa Mungu.
Watoto wa Mungu wana tabia ya namna gani?
            Kwa kuwa wamehamishwa toka ufalme mwingine na uzazi mwingine, na kuingizwa katika ufalme wa Mungu na uzazi wake (Wakolosai 1:13); watoto hawa wanatakiwa wawe na tabia nyingine.
             Kabla ya kuzaliwa mara ya pili, kabla ya kumkiri Kristo ya kuwa ni Bwana: ulikuwa na tabia ya dunia hii iliyoongozwa na mfalme wa dunia hii ambaye ni shetani.
             Ulipozaliwa mara ya pili na kuukiri wokovu katika Kristo, ulipokea tabia mpya inayoongozwa na Mungu mwenyewe aliye ndani yako.

"  Kwa kuwa uwezo wake wa Uungu umetukirimia  vitu vyote vipasavyo uzima na utauwa (Utakatifu), kwa kumjua yeye aliyetuita kwa utukufu wake na wema wake mwenyewe. Tena kwa hayo ametukirimia ahadi kubwa mno; za thamani,ili kwamba kwa hizo mpate kuwa Washirika wa TABIA YA UUNGU, mkiokolewa na uharibifu uliomo duniani kwa sababu ya tamaa." (2 Petro 1:3,4)

             Mistari hii inatuonyesha wazi kabisa kuwa kwa uweza ule ule uliokuwezesha kuwa mwana wa Mungu, unakuwezesha kuipokea tabia ya Mungu.
             Tabia ya Mungu iliyo wazi ni Upendo kwa kuwa Mungu ni Upendo
(1 Yohana 4:8)

             Ni upendo ambao huvumilia, hufadhili, hauhusudu, hautakabari, haujivuni, haukosi kuwa na adabu, hautafuti mambo yake, hauoni uchungu, hauhesabu mabaya, haufurahii udhalimu, bali hufurahi pamoja na kweli,huvumiliayote,huamini yote, hutumaini yote, hustahimili yote, haupungui neno wakati wowote.Kamailivyoandikwa katika (1 Wakorintho 13:4 - 8)

 Mungu anavyosamehe:
         Ndani ya upendo, kuna tabia ya kusamehe na kusahau. Ili kuifahamu zaidi na tuitafakari tabia ya Mungu ya kusamehe na kusahau. Mungu anasema hivi:

Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; wala sitazikumbuka dhambi zako." (Isaya 43:25)

Na tuitafakari tabia hii ya Mungu katika mafungu mawili yafuatayo:
1. Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe; na;
2. Wala sitazikumbuka dhambi zako.

              Haya ni maneno ya Mungu ambayo aliyasema kwa kutumia kinywa cha nabii Isaya, kwa ajili ya watu, baada ya kufunga agano jipya katika damu ya Yesu Kristo pamoja nao. Kwa kuwa katika agano la kale makosa (au dhambi) yalikuwa hayafutwi ila yanafunikwa tu kwa damu ya wanyama waliotolewa sadaka (Waebrania 10:1 - 25)
             Lakini katika agano jipya, makosa yanafutwa kwa uwezo wa damu ya Yesu iliyomwagika msalabani.
             Kuna tofauti kubwa kati ya kuifunika dhambi kwa damu na kuifuta dhambi kwa damu. Unapofunika, kosa haliondoki linabaki pale pale, lakini linakuwa halionekani. Unapofuta, kosa linaondolewa kabisa, inakuwa kama hakuna kosa lililowahi kufanyika.
             Ukiwa darasani, mwalimu akifuta maandishi ya chaki ubaoni, ubao unabaki hauna maandishi; unakuwa safi. Lakini utakuta yale yaliyokuwa yameandikwa, ingawa hayapo ubaoni, katika akili za watu yanakuwa yapo. Na wakati mwingi inachukua muda kufutika mawazoni.
             Sasa, ile sehemu ya kwanza ya mstari, Mungu anasema anayafuta makosa yetu kwa ajili yake mwenyewe, Mungu hakusema "Anayafunika makosa," bali amesema, "anayafuta makosa".
Soma tena:
"Mimi, naam, mimi, ndimi niyafutaye makosa yako kwa ajili yangu mwenyewe."
Soma na maneno haya:
"Tukiziungama dhambi zetu, yeye ni mwaminifu na wa haki hata atuondolee dhambi zetu, na kutusafisha na udhalimu wote" (1Yohana 1:9)
            Ukitubu dhambi zako kwa Mungu katika Roho na Kweli, Mungu anakusamehe, na anafuta dhambi zako na mbele yake unaonekana kama hukufanya kosa lo lote. Hivyo ndiyo maana ya kuhesabiwa haki mbele za Mungu katika Kristo. Kusamehe ni kufuta au kuondoa kosa na kulisahau au kutokulikumbuka tena.

 Kusamehe kosa = kufuta + kutokulikumbuka kosa

            Wakati huu tunatizama jinsi Mungu anavyotusamehe. Hatua ya kwanza anafuta kosa machoni pake.
             Kwa nini Mungu atusamehe?
             Kwa nini Mungu ayafute makosa yetu?
             Umewahi kujiuliza kwa nini Mungu aliamua kukusamehe mabaya yote uliyoyafanya maishani mwako?
             Watu wengine wanafikiri wokovu unakuja kwa kumpendeza Mungu kwa matendo yao. Na matokeo yake wanajihesabia haki wenyewe badala ya kuhesabiwa haki na Mungu.
             Utamsikia mtu anasema mimi sina dhambi, siibi, sizini, silewi, sijatengwa na kanisa, na naitunza Sabato kwa hiyo sina kosa kwa Mungu!
 Lakini neno la Mungu linatuambia mambo tofauti, kwa mfano neno linasema hivi:

" Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala SI KWA MATENDO, mtu awaye yote
 asije akajisifu
(Waefeso 2:8,9)

            Kwa hiyo, unaona kuwa matendo yako peke yake hayawezi kukupa wokovu, na ondoleo la dhambi, bila ya imani ndani ya Kristo. Imani lazima iambatane na matendo. Imani pasipo matendo imekufa (Yakobo 2:26).
            Kitu kinachomfanya Mungu akusamehe si uzuri wa matendo yako; bali anakusamehe KWA AJILI YAKE MWENYEWE.
              Mungu anasema; "Mimi, naam, Mimi, ndimi niyafutaye makosa yako KWA AJILI YANGU MWENYEWE"
            Huu ndiyo upendo wa ajabu!
            Kumbuka si kwa matendo yako bali kwa ajili yake mwenyewe Mungu, unapata kusamehewa makosa yako.

Mungu akisamehe anasahau:

            Hatua ya pili ambayo Mungu anaichukua mara tu anapofuta makosa yako ni kuyasahau aliyokwisha yafuta.
            Yeye mwenyewe ameahidi kwamba
".... Wala sitakumbuka dhambi zako". WALA SITAKUMBUKA DHAMBI ZAKO!
            Ina maana kuwa Mungu akiisha kukusamehe kwa ajili yake mwenyewe; anafuta na kusahau makosa uliyofanya, anakuhesabia haki bure mbele zake. Unasimama ndani yake kama mtu ambaye hajawahi kufanya kosa wala dhambi yo yote.
            Sasa kama Mungu amekwishafuta na kuyasahau mambo uliyofanya kabla hujaokoka na ukatubu, kwa nini wewe unayakumbuka? Jifunze kujisamehe mwenyewe! Mungu akikusamehe na wewe jisamehe. Mungu asipoyakumbuka makosa yako, na wewe usiyakumbuke!
            Huduma za watumishi wengi zinakwama mara tu anapokumbuka mambo aliyoyafanya zamani au maneno aliyoyasema - hata kama wamekwishayatubia!
            Kwa sababu hiyo, badala ya kusonga mbele katika Bwana, anajikuta kila wakati wanatubu juu ya dhambi hiyo hiyo. Na wanakosa ujasiri wa kusimama mbele za Mungu, mbele ya shetani na mbele za watu.
            Kila wanapotaka kufanya kitu, shetani anawaletea wazo kuwa, bado hawajasamehewa kosa alilolifanya jana au juzi. Na kwamba haitakuwa rahisi kwako kupokea baraka toka kwa Mungu. Kwa hiyo watu hawo anaanza kutubu tena upya!

            Watu wengi hata sasa hawana uhakika kama Mungu amewasamehe juu ya makosa waliyoyafanya.
            Uhakika utaupata katika Neno la Mungu.
Mungu ameahidi kuwa ukitubu katika Roho na Kweli, unasamehewa.
(1Yohana 1:9)
            Paulo alifahamu siri hiyo ya kuyasahau mambo ya nyuma aliyomkosea Kristo, kwa kuwatesa wafuasi wa Yesu, kabla ya kuokoka kwake. Hii ilimsaidia kulitangaza Jina la Yesu bila yeye kujisikia vibaya moyoni mwake.
Kwa hiyo Paulo aliweza kusema:
"...... ila natenda neno moja tu; nikiyasahau yaliyo nyuma, nikiyachuchumilia yaliyo mbele, nakaza mwendo niifikilie mede ya thawabu ya mwito mkuu wa Mungu katika Kristo Yesu" (Wafilipi 3:13,14)
            Ili uweze kusonga mbele katika wokovu, ni budi ujifunze kujisamehe na kuyasahau uliyoyafanya zamani.

Tabia hii unayo ndani yako:
            Kuyafuta makosa na kutoyakumbuka tena ni tabia ya Mungu ambayo imo ndani yako sasa.
            Ulipompokea Kristo moyoni mwako na kumkiri kuwa ni Bwana wa maisha yako, pia ulipokea ndani ya moyo wako tabia hii ya Mungu ya kufuta makosa na kutoyakumbuka.
            Hii ndiyo tabia inayotakiwa ionekane katika maisha yako unapokosewa na mtu.
            Tatizo la wengi ni kwamba wamekuwa viumbe vipya, lakini wanataka kutumia tabia yao ya zamani. Katika tabia ya zamani, walisamehe lakini hawakusahau walichokosewa. Tabia mpya ni kufuta makosa na kutoyakumbuka kabisa. Kwa hiyo na sisi tukikosewa tunatakiwa kusamehe na kusahau!

Hatua zifuatazo katika mfululuzo wa masomo yanayofuata wiki zijao zitakusaidia kuijenga na kuitumia tabia hiyo ya Mungu iliyo ndani yako. Tunaamini utakuwa pamoja nasi wiki ijayo ili kuendelea na somo hili - katika kipengele kinachosema: "Hasara za kulipiza kisasi"

Jifunze kusamehe na kusahau / Utang / 1 / 2 / 3 / 4 / 5 / 6 /

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.