Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
MKRISTO NA UCHUMI


Sura ya Nane 

SADAKA NA WOKOVU

             “Palikuwa na mtu Kaisaria jina lake Kornelio, akida wa kikosi kilichoitwa Kiitalia, mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, naye alikuwa akiwapa watu SADAKA NYINGI, na kumwomba Mungu daima. Akaona katika maono waziwazi, kama saa tisa ya mchana, malaika wa Mungu, akimjia na kumwambia, Kornelio! Akamtazama sana, akaogopa akasema, kuna nini, Bwana? Akamwambia, Sala zako na SADAKA ZAKO zimefika juu na kuwa ukumbusho mbele za Mungu. Sasa basi, peleka watu Yafa, ukamwite Simoni, aitwaye Petro. Yeye ni mgeni wa mtu mmoja, jina lake Simoni, mtengenezaji wa ngozi, ambaye nyumba yake iko pwani; ATAKUAMBIA YAKUPASAYO KUTENDA” (Matendo ya Mitume 10:1 – 6).

            Tabia hii ya Kornelio ya kuwa mtu mtauwa, mchaji wa Mungu, yeye na nyumba yake yote, na pia tabia ya utoaji wa sadaka na kumwomba Mungu daima, inaonyesha wazi kuwa Kornelio alimpenda Mungu sana na alikuwa anatafuta namna yakukubalika mbele zake na namna ya kumpendeza Yeye.

            Tungezungumza kwa lugha nyepesi zaidi, ni kwamba alitaka kwa MATENDO YAKE aende mbinguni na kuurithi Uzima wa Milele baada ya kufa kwake . Kwa kifupi alimtafuta Mungu kwa njia ya Matendo.

            Hii ina maana ya kuwa Kornelio alitaka kuvuna  baraka za Agano Jipya katika damu Yesu, wa kutumia njia za kupendeza Mungu zilizomo katika Agano la Kale.

            Tena ingawa yeye hakuwa Myahudi kwa kuzaliwa, alitaka sana kuvuna baraka ambazo Mungu aliahidi juu ya Wayahudi.

            Mpaka hivi leo kuna watu wengi wanataka kuvuna baraka toka kwa Mungu bila kutumia utaratibu aliouweka Mungu wa kuzipokea. Ni vigumu sana kupokea ahadi za Mungu nje ya mpango wake.

            Huwezi kupokea ahadi za agano la kale kwa kutumia mbini za agano la kale na huku sasa hivi tumo katika kipindi cha agano jipya.

            Baraka zote zilizomo katika agano la kale aliahidiwa Ibrahimu na uzao wake MILELE. Soma mwenyewe Mwanzo sura ya 17 na 22. Kwa hiyo ukitaka kupokea baraka za agano la kale lililofungwa kati ya Mungu na Ibrahimu, inabidi uwe mzao au mtoto wa Ibrahim. - Kornelio hakufahamu hili; hata leo hii wengi hawafahamu.

            Baraka zote zilizomo katika agano jipya zimeahidiwa wale walio ndani ya Kristo – waliotoa maisha yao kwa Yesu kama vile Yesu Kristo alivyotoa maisha yake kwa ajili yao.

            Ni vigumu kupokea baraka za ahadi za agano la kale na zile za agano jipya NJE YA YESU KRISTO. Imeandikwa hivi katika Wagalatia 3:13,14,29;

“Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa, baraka ya Ibrahimu IWAFIKILIE MATAIFA KATIKA YESU KRISTO, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani…… Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi. "

  Ndiyo maana Mungu alimtuma Malaika wake ili amwambie Kornelio kuwa amwite Simon Petro ili awaeleze habari za Yesu Kristo – ili baraka ya Ibrahimu iwafikie na wapate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani –  SIYO KWA MATENDO PEKE YAKE.
            Jambo ambalo Mungu alitaka Kornelio ajue na sisi pia tujue ni kuwa matendo mema, maombi na SADAKA bila “kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya imani” yaani kuzaliwa mara ya pili kwa Roho au kuokoka – haitoshi  kumpendeza Mungu, wala kukubalika mbele zake au kuhesabiwa haki.


            Ndiyo maana Yesu Kristo alimwambia Nikodemo, yule Farisayo kuwa
“Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu ….. Usistaajabu kwa kuwa nilikuambia, HAMNA BUDI kuzaliwa mara ya   pili”(Yohana 3:3,7).

            Haya maneno “Hamna Budi” maana yake ni “lazima” kwa hiyo Yesu Kristo alikuwa anasema “…… LAZIMA kuzaliwa mara ya pili”.

            Yesu Kristo alikuwa anasisitiza kwa Nikodemo, na hata kwetu sote tunaotaka kuurithi ufalme wa Mungu, kuwa hakuna njia nyingine isipokuwa LAZIMA kuzaliwa mara ya pili kwa Roho (au kwa maneno mengine) LAZIMA Kuokoka!

IMANI NA MATENDO

          Matendo peke yake hayatoshi kukupa ufalme wa Mungu. Kuna watu wengi sana ambao ni waaminifu sana katika kusali na kumtolea Mungu sadaka, lakini hawakubaliani na jambo kuokoka. Wanaona kuwa wao tayari wameokoka kwa sababu tu wanasali, wanatoa sadaka na kujitahidi kuishi katika matendo mema. Hebu soma   maneno ya mistari hii uone yanavyopingana na msimamo huu;

“Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; WALA SI KWA MATENDO, mtu awaye yote asije akajisifu” (Waefeso 2:8,9)

            Tunaokoka kwa njia ya imani itendayo kazi katika Yesu Kristo, “Wala si kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu”. Matendo yana faida zaidi kwa mtu baada ya kuokoka. Na pia imani bila matendo, imani hiyo imekufa nafsini mwake. Biblia inasema hivi:

           “Ndugu zangu, yafaa nini, mtu akisema ya kwamba anayo imani, lakini hana matendo? Je! ile imani yaweza kumwokoa?…. Vivyo hivyo na imani, isipokuwa ina matendo, imekufa nafsini mwake. Lakini mtu atasema, wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha IMANI YANGU KWA NJIA YA MATENDO YANGU …….. Maana kama vile mwili pasipo roho umekufa, vivyo hivyo na imani pasipo matendo imekufa” (Yakobo 2:14,17,18,26).

           Jambo ambalo Yakobo alikuwa anasisitiza hapa ni kutaka kuwaonya watu kuwa kusema wewe ni mkristo na huku matendo yako hayalingani na ushuhuda wa mdomo wako ni bure. Wokovu uonekane katika maisha yetu kila siku – la sivyo imani tuliyo nayo inakosa kuzaa matunda ya uzima wa milele. Ndiyo maana Yesu Kristo aliwahi kuzungumza juu ya kukatwa kwa tawi (Mkristo) lisilo zaa, soma Yohana 15:1-8 ili upate picha zaidi juu ya jambo hili.

CHUKUA HATUA LEO

          Malaika alimwambia Kornelio atume watu wakamwite Simoni aitwaye Petro ili AMWAMBIE YAMPASAYO KUTENDA. Mungu kwa uweza wa Roho wake Mtakatifu amekuletea maneno haya mkononi mwako ili UFAHAMU YAKUPASAYO KUTENDA.

          Kama hujaokoka na unadhani unaweza kuokoka kwa kutoa sadaka nyingi NAKUSHAURI KWA JINA LA YESU KRISTO WA NAZARETI uombe sala hii kwa sauti, ili utubu na kumpa Yesu Kristo maisha yako leo. HALAFU endelea kutoa sadaka nyingi ukiwa ndani ya Yesu Kristo.

           Omba sala hii kwa sauti; “Mungu Baba, unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu. Ninatubu kwako. Nitakase kwa damu ya Yesu Kristo. Bwana Yesu Kristo nimefungua moyo wangu nakukaribisha uingie ndani yangu, kwa uwezo wa Roho wako. Uwe Bwana na Mwokozi wa maisha yangu – sasa na hata milele. Asante kwa kunisamehe dhambi na kuniokoa. Amina”.

            Ikiwa umeisema sala hii kwa uaminifu, basi umefanyika kiumbe kipya – umezaliwa mara ya pili na Mungu hakumbuki dhambi zako tena. Soma 2Wakorintho 5:17, Waebrania 8:12. Karibu sana katika ufalme wa Mungu kwa jina la Yesu Kristo!

         Hili ndilo lililotokea kwa Kornelio na jamaa yake, Simoni Petro alipofika kwao aliwaambia habari za Yesu Kristo – walisikia maneno hayo wakamwamini Yesu na kujazwa na nguvu za Roho Mtakatifu wakati huo huo.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.