Sura ya Nne
UTAJIRI
WAKE KRISTO USIOPIMIKA
" Mimi, niliye mdogo kuliko yeye aliye mdogo wa watakatifu
wote, nalipewa neema hii ya kuwahubiri Mataifa UTAJIRI WAKE KRISTO
USIOPIMIKA; na kuwaangaza watu wote wajue habari za madaraka ya siri
hiyo, ambayo tangu zamani zote ilisitirika katika Mungu aliyeviumba vitu
vyote, ili sasa, kwa njia ya Kanisa, hekima ya Mungu iliyo ya namna
nyingi ijulikane na falme na mamlaka katika ulimwengu wa roho"(Waefeso
3:8 - 10).
"
Na Mungu wangu atawajazeni KILA MNACHOHITAJI KWA KADIRI YA UTAJIRI WAKE
KATIKA UTUKUFU,NDANI YA KRISTO YESU" (Wafilipi 4:9)
Kristo ana utajiri usiopimika. Na wote walio ndani yake ni warithi
pamoja naye wa utajiri usiopimika. Kutokana na utajiri huo TUNAJAZWA
KILA TUNACHOKIHITAJI. Mahitaji haya ni ya kiroho, kiakili na kimwili.
Kwa hiyo hakuna sababu ya mkristo kuishi maisha ya kupungukiwa, ikiwa
Kristo yuko ndani ya moyo wake pamoja na utajiri wake usiopimika. Au
wewe una maoni tofauti juu ya hili?
Jambo
la kujiuliza ni hili; kwa nini utajiri huu wa Kristo usiopimika
hauonekani katika maisha ya wakristo wengi? Wakristo waishije katika
ushuhuda wa wokovu ndani ya Kristo, wakati wanaishi katika ulimwengu
wenye hali ngumu kiuchumi? Watumishi wa Mungu kwa mfano, wachungaji,
wainjilisti na kadhalika, waishije katika kumtumikia Mungu vizuri bila
kupoteza ushuhuda wao wakati wanaishi katika mazingira yenye maisha
magumu kiuchumi?
Haya
si maswali mepesi kuyajibu, lakini ni muhimu yatafutiwe ufumbuzi. Kabla
hatujaanza kuyajibu napenda tusome Waefeso 4:11;
" Naye (Yesu Kristo) alitoa wengine kuwa mitume; na wengine kuwa
manabii; na wengine kuwa wainjilisti; na wengine kuwa wachungaji na
Waalimu."
Ni
kwa kusudi gani Bwana Yesu Kristo aliamua kuwaweka hawa katika kazi yake
kanisani? Waefeso 4:12-16 inatupa maelezo:-
"Kwa
kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke, hata
mwili wa Kristo ujengwe; hata na sisi sote tutakapoufikia umoja wa imani
na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu mkamilifu, hata kufika
kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo, ili tusiwe tena watoto
wachanga, tukitupwa huku na huku, na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu,
kwa hila ya watu, kwa ujanja, tukizifuata njia za udanganyifu. Lakini
tuishike kweli katika upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote,
yeye aliye kichwa, Kristo. Katika yeye mwili wote ukiunganishwa na
kushikanishwa kwa msaada wa kila kiungo, kwa kadri ya utendaji wa kila
sehemu moja moja, huukuza mwili upate kujijenga wenyewe katika upendo"
Kwa kuisoma mistari hii tunapata kufahamu ya kuwa hawa waliotajwa ni
watumishi wa Mungu katika Kristo. Na wana wajibu maalum waliopewa na
Mungu. Pia ni muhimu kukumbuka kuwa si hao peke yao waliotumwa kazini na
Kristo, lakini kila mkristo ana wajibu wa kufanya (Yohana 17:18; Warumi
12:4-8).
Naamini kabisa ya kuwa tukifahamu Mungu aliwatunzaje watumishi wake
katika biblia, tutakuwa tumepata mwanga wa jinsi ambavyo anawatunza
watumishi na watu wake hivi leo. Ni budi tukumbuke ya kuwa Yeye ni yule
aliyekuwepo, aliyepo na atakayekuja (Ufunuo 4:8) na pia ni "Yeye
yule jana na leo na hata milele" (Waebrania 13:8)
Baada
ya kuisoma biblia kwa makini nimeona ya kuwa kuna njia nne ambazo Mungu
amekuwa akizitumia kuwahudumia na kuwatunza watumishi wake na watu wake.
Na naamini hata hivi leo anatumia njia hizi, kwa namna ambayo yeye
mwenyewe amechagua.
Njia ya kwanza; Mshahara:
Njia mojawapo anayotumia ni kuwapa watu wake mishahara au ujira -
kufuatana na kazi wanazozifanya.
"Ni
askari gani aendaye vitani wakati wo wote kwa gharama zake mwenyewe? Ni
nani apandaye mizabibu asiyekula katika matunda yake? Au ni nani
achungaye kundi, asiyekunywa katika maziwa ya kundi? Je! Ninanena hayo
kwa kibinadamu? Au torati nayo haisemi yayo hayo? Kwa maana katika
torati ya Musa imeandikwa, usimfunge kinywa ng'ombe apurapo nafaka. Je!
hapo Mungu aangalia mambo ya ng'ombe? Au yamkini anena hayo kwa ajili
yetu? Naam, yaliandikwa kwa ajili yetu, kwa kuwa alimaye nafaka ni haki
yake kulima kwa matumaini; naye apuraye nafaka ni haki yake kutumaini
kupata sehemu yake."
Ikiwa
sisi tuliwapandia ninyi vitu vya rohoni je! Ni Neno kubwa tukivuna vitu
vyenu vya mwilini?
"..........
Hamjui ya kuwa wale wazifanyao kazi za hekaluni hula katika vitu vya
hekalu, na wale waihudumiao madhabahu huwa na fungu lao katika vitu vya
madhabahu? Na Bwana vivyo hivyo ameamuru kwamba wale waihubirio injili
wapate riziki kwa hiyo injili" (1 Wakorintho 9:7-14)
Kwa
sababu unafanya kazi ya injili, Bwana ameamuru kwamba upate riziki yako
katika injili. Watu wengine kwa kutokuelewa vizuri juu ya mistari hiyo
tuliyoisoma, wameigeuza kazi ya kumtumikia Mungu kama mradi wa kupatia
fedha za kumsaidia kuishi. Lakini kazi hiyo ni wito. Na kila wito una
kusudi lake. Na kwa kuwa Mungu anafahamu kuwa utahitaji kuwa na mahitaji
muhimu ya maisha, anakupa mshahara au ujira. Njia anazotumia kutoa
mishahara au ujira ni nyingi, na anazitumia kama apendavyo yeye.
Na
kwa wale walio na utaratibu wa kuwapa wachungaji kama mishahara, fedha
hizo mara nyingi zinakuwa hazitoshi kukidhi mahitaji yao ya kila siku na
familia zao. Na hii ndiyo hali halisi. Lakini jambo muhimu ni kwamba
wanapewa mshahara.
Ukisoma kitabu cha Hesabu 18:8-15, 18 - 20 na Kumbukumbu la Torati
18:1-5 utaona ya kuwa kwa kadri wana wa Israeli walivyomtolea Mungu wao
sadaka ndivyo na makuhani walivyoopokea ujira wao. Kwa maneno mengine
ina maana ya kuwa, kama wangetoa sadaka kidogo, basi na makuhani
wangepata ujira kidogo.
Na
pia watumishi wa Kristo wanatakiwa watunzwe kwa chakula katika nyumba
ambazo wanakwenda kuhudumu. " Akawaambia,
Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa
mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake. Enendeni, angalieni
nawatuma kama wana kondoo katika ya mbwa-mwitu ..... Na nyumba yoyote
mtakayoingia, semeni kwanza, Amani iwemo nyumbani humu ...... Basi,
kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda
kazi amestahili kupewa ujira wake ..... Na mji wowote mtakaouingia,
wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu"
(Luka 10:1-8).
Njia ya Pili: Utoaji:
Njia
nyingine ambayo watumishi wa Kristo na wakristo wanaweza kupokea vitu
vya kuwasaidia katika maisha yao ni kwa njia ya utoaji.
Biblia inasema katika Luka 6:38;" Wapenzi
watu vitu, nanyi mtapewa, kipimo cha kujaa na kushindiliwa, na
kusukwasukwa hata kumwagika, ndicho watu watakachowapa vifuani
mwenu. Kwa kuwa kipimo kile kile mpiamacho ndicho mtakachopimiwa".
Swali
muhimu la kujiuliza ni kama mtu anaweza kutoa kama hana kitu cha kutoa.
Ni wazi kwamba hataweza kutoa. Lakini mara nyingi hatakosa kitu cha
kumtolea Mungu.
Na
jambo hili Mungu anafahamu. Hata kule jangwani alipowaambia wana wa
Israeli watoe kwa ajili ya ujenzi wa Hema ya kukutanikia; alijua kabisa
kuwa alikuwa amewapa vitu hivyo kabla hawajatoka Misri. Kwa hiyo walitoa
walizokuwa wamepewa na Mungu tayari. Na walipotoa, Bwana aliwabariki
zaidi.
Kwa
mkristo je! Anapotakiwa atoe ili apokee, atoe kitu gani alichopewa na
Mungu? Wazo la kwanza linalonijia ni atoe fungu la kumi la mshahara wake
kila mwezi kama yanenavyo maandiko. Soma Malaki 3:10.
Mkristo asipokuwa mwaminifu kumtolea Mungu ahadi yake ya fungu la kumi,
anategemea kubarikiwa kwa njia gani? Na je! Ni vizuri kwa mchungaji
kutokuwa mtoaji, wakati anawafundisha wakristo wawe watoaji?
Bora
kutoa kuliko kupokea. Wengine wanasema bora kupokea kuliko kutoa. Lakini
neno la Mungu linasema bora kutoa kuliko kupokea.
Tatizo la wakristo wengi katika utoaji huwa wanatoa bila ya kuwa na
lengo maalum. Wengine wanatoa kwa kuwa wameambiwa watoe, lakini wao
wenyewe hawana lengo maalum katika utoaji huo. Na kwa sababu hii hawaoni
baraka zilizopo katika maisha ya utoaji.
Ukiangalia katika Biblia utaona ya kuwa kuna sababu kubwa zifuatazo:
(a) Tunatoa ili Mungu ashukuriwe ndani ya Kristo Yesu kwa utoaji huo
(2Wakorintho 9:11 -12)
(b) Tunatoa ili injili ihubiriwe (1 Wakorintho 9:7-14)
(c) Tunatoa ili waliopungukiwa wapate riziki (2Wakorintho 9:12)
(d) Tunatoa ili Mungu amkemee shetani au yule anayeharibu matunda
yetu ndani ya Kristo (Malaki 3:10-12)
(e) Tunatoa ili tupate zaidi (Malaki 3:10 - 13; Luka 6:38; 2
Wakorintho 9:6-11)
Unapotoa kitu chochote kwa Mungu kama sadaka, au zaka au dhabihu, uwe na
malengo hayo ndani yako.
Wakristo wengi kwa mfano huwa wanatoa bila kutegemea kupokea. Mara
nyingi huwa nawauliza wasikilizaji ninapofundisha juu ya jambo hili hivi;
"Je! Ninyi huwa mnatoa fedha kama sadaka?"
Wanajibu; "Ndiyo'
Halafu nauliza tena; "Je!
huwa mnawapa watu fedha ili ziwasaidie katika shida zao?"
Pia wanajibu "Ndiyo"
Halafu nawaambia tusome Luka 6:38 inayosema hivi:"Wapeni
watu vitu, nanyi mtapewa; KIPIMO cha KUJAA na KUSHINDILIWA, na KUSUKWA -SUKWA
hata KUMWAGIKA, ndicho watu watakachowapa vifuani mwenu. Kwa kuwa kipimo
kile kile mpimacho ndicho mtakachopimiwa".
Ikiwa
umetoa fedha, Mungu kwa kutumia njia zake atakupa fedha nyingine kwa
kipimo cha KUJAA na KUSHINDILIWA, na KUSUKWA-SUKWA hata KUMWAGIKA! Kwa
nini Mungu akutajirishe? Ni ili malengo ya utoaji niliyoyasema yaendelee
kutekelezwa!
Kwa hiyo uwe mtoaji, kwa maana kuna vitu ambavyo Mungu amekwishakupa
tayari, hata kama ni vichache.
Njia ya tatu; Muujiza:
Muujiza ni tendo linalotokea tofauti na taratibu zinazofahamika na
mwanadamu.
Je!
unakumbuka jinsi Nabii Eliya alivyolishwa na Mungu kwa kumtumia kunguru?
Na unakumbuka jinsi ambavyo Mungu alivyomlisha Nabii Eliya kwa kumtumia
yule mama wa Serepta? Je! unakumbuka jinsi ambavyo Mungu alimlisha yule
mama wa Serepta pamoja na mtoto wake kwa miujiza.
Na
wana wa Israeli je! si nao walilishwa kwa mana jangwani?
Je!unadhani Mungu hawezi kuyafanya hayo tena? Au na wewe uko upande wa
wale wasemao miujiza ilikoma walipokufa mitume?
Mimi naamini Mungu wetu hajabadilika na anaweza kufanya tena miujiza
katika kuwalisha watumishi wake.
Lakini usije ukaacha kufanya kazi kwa kutaka kuusubiri muujiza wa Bwana.
Hiyo haitakuwa sawa. Kwa sababu Mungu anazo njia nyingi za kuwatunza
watu wake, muujiza ni njia mojawapo, na njia hii haitumii mara nyingi
sana; na kumbuka ataitumia katika muda anaotaka na kwa mtu anayemtaka;
kwa ajili ya utukufu wa jina lake.
Njia ya nne; Kazi za kuongeza kipato
Ni
kweli kwamba mishahara ya watu haitoshi kukidhi mahitaji yao ya kila
siku pamoja na familia zao.
Ukisoma katika 2Wathesalonike 3:6-12; Mtume Paulo anawaeleza
Wathesalonike juu ya umuhimu wa kila mtu kufanya kazi. Na hata
anaendelea kusema, "ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi , asile
chakula. Na katika 1Wathesalonike 4:11 - 15 anazidi kukaza juu ya mtu
kufanya kazi kwa mikono yake mwenyewe.
Naamini unafahamu ya kuwa ingawa watu walimhudumia Mtume Paulo kwa kumpa
vitu vya kumsaida kimaisha; lakini yeye mwenyewe hakuwalemea bali
alifanya kazi kwa mikono yake ili aongeze kipato chake.
Wachungaji na wakristo wengi wanajihusisha na miradi mbalimbali binafsi
kwa ajili ya kuongeza kipato. Hili ni jambo zuri; lakini ni muhimu kuwa
mwangalifu ili miradi hiyo au kazi unazofanya ili kuongeza kipato,
hazitaharibu uhusiano wako na Mungu na kuzorotesha wito wako.