Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
RIPOTI - SEMINA YA MOSHI JANUARI 2003


KAMA SI MUNGU      -         KILIMANJARO NA WASEME!

[Siku 16 za Miujiza na semina ya Neno la Mungu – Moshi Tarehe 12 – 27 Januari 2003]

       Katika Zaburi 124:1 tunasoma maneno haya, “Kama si Bwana aliyekuwa pamoja nasi, Israeli na aseme sasa.” Haya ni maneno ambayo mfalme Daudi aliyasema ili kuweka wazi jinsi mkono wa Mungu ulivyojidhihirisha katikati ya taifa la Israeli. Na sisi tunaona tuandike kichwa hiki kwa ajili ya ripoti hii kinachosema; “Kama si Mungu Kilimanjaro na waseme!” Tumeona na sisi tutumie maneno haya kama ya mfalme Daudi ili kueleza kile ambacho kimetokea katika siku zote 16 za semina ya Neno la Mungu tuliyoifanya Moshi mjini katika viwanja vya mashujaa tarehe 12-27 Januari 2003.

Mahudhurio

            Mahudhurio ya watu katika semina yalikuwa makubwa kuliko tulivyotarajia; kwa hiyo maandalizi yake hayakuweza kukidhi maelfu ya watu waliohudhuria. Tunasema hili kwa kuwa tulikuwa na hema lenye uwezo wa kukalisha watu 15,000 na tukaweka viti vilivyokuwa na uwezo wa kukalisha watu 12,000; bado kuna maelfu ya watu waliokuwa wanasimama ndani na nje ya hema – hasa siku za Jumamosi na Jumapili!

            Watu walitoka karibu katika wilaya zaote za mkoa wa Kilimanjaro,  na  wako waliokuwa wanahudhuria toka Arusha mjini kila siku – kwa siku zote 16! Tunamshukuru Mungu sana kwa wenye mabasi ambao walijikuta wakibadili utaratibu wao wa kila siku wa kusafirisha abiria, na badala yake kujikuta wanaleta watu kwenye viwanja tulipofanyia semina, na kuwasubiri watu kila siku jioni hapo hapo uwanjani.

Masomo

            Mungu alitupa utaratibu na mpangilio wa vipindi kwa namna ambavyo siku 16 zilionekana chache! Tunaamini kabisa yakuwa uwepo wa Roho Mtakatifu ndio uliofanya siku ambazo zilikuwa zinaonekana nyingi – zionekane chache! Wiki ya kwanza tulifundisha somo linalosema “USIMZUIE YESU KUKUSAIDIA”. Wiki ya pili tulifundisha juu ya majaribu, tukilenga juu ya . “LAKUFANYA UNAPOSONGWA NA MAJARIBU”. Masomo haya tulifundisha  vipindi vya jioni.

            Siku ya pili ya semina tuliwafundisha jinsi ambavyo mtu anaweza kumzuia Yesu asimsaidie kwa kuamua kumchanganya Mungu na miungu mingine katika maisha yake. Inajulikana wazi ya kuwa sehemu kubwa ya watu wa Kilimanjaro ni wakristo; lakini pia bado wana tabia ya kufanya matambiko kwa mizimu ya babu zao. Lakini, pia, kuna baadhi yao wamekuwa wakienda nje ya Kilimanjaro kununua uchawi hasa kwa ajili ya ‘kujilinda’ na kusaidiwa kupata ‘mali’. Tuliwaonyesha jinsi biblia inavyokataza mchanganyo huu na madhara yake kwao, kwa ardhi, na kwa watoto wao, ikiwa hawatatubia uovu huu.

            Tunamshukuru Mungu kwamba wengi walitubu kwa ajili yao na kwa ajili ya familia zao; huku wakileta ‘hirizi’ na ‘bangili’ za matambiko, ambavyo vyote vilichomwa moto katika Jina la Yesu!

            Wakati wa  asubuhi tulikuwa tunaombea nchi yetu hasa katika wiki ile ya kwanza. Katika wiki ya pili watu walifundishwa juu ya “ufuasi na ufuatiliaji” na walimu toka ofisi ya ‘Life Ministry’ ya Arusha.

Maelfu Waokoka!

            Inakisiwa na kamati ya maandalizi ya kuwa kiasi cha wastani wa watu 7000 walimpa Yesu maisha yao na kuokoka katika siku hizo 16 za semina. Makisio haya yalifikiwa baada ya kuona ya kuwa kadi zote 6000 zilizotengenezwa kwa ajili ya kuwaandikisha wanaookoka zilikwisha!

            Lakini zaidi ya hayo siku ya 15 ya semina ambayo ilikuwa  na mahudhurio makubwa kuliko siku nyingine (kati ya watu 16,000 hada 20,000 inakisiwa walikuwepo uwanjani) – watu waliokoka awamu mbili. Roho Mtakatifu alituongoza kuita watu mbele waokoke kabla ya neno (awamu ya kwanza) na baada ya neno (awamu ya pili). Siku hiyo maelfu ya watu waliokoka kiasi ambacho wahudumu walizidiwa na wingi huo na hawakuweza kuwaandika wote waliookoka siku hiyo. Sifa zote ni kwa Yesu Kristo! Tunaamini utaungana nasi kumshukuru Mungu kwa hili, na kuwaombea wote waliookoka katika semina hii wasimame katika wokovu na kuendelea kwa ushindi ndani ya Yesu!

Miujiza!

            Katika semina hii wagonjwa wengi sana walipona kwa nguvu za Jina la Yesu! Kwa sababu ya muda tuliokuwa nao kutokutosha, si wote waliopona waliopata nafasi ya kushuhudia wakati semina ikiendelea. Lakini kwa wale walioshuhudia tuliona na kusikia mambo ya ajabu sana na yenye kumtukuza Mungu sana.

            Wakati huu baada ya kumaliza semina tunapokumbuka yaliyotokea tunaona ya kuwa kuna siku wagonjwa wa aina Fulani walikuwa wanapona wengi kuliko wengine! Kwa mfano, kuna siku walijitokeza watu watatu mfululizo wote wakishuhudia kupona na kufunguliwa sikio la kushoto na kuweza kusikia tena. Siku nyingine walijitokeza watu mfululizo waliokuwa na shida za macho na kutoona, na wengine kutosoma vizuri. Hao nao wakashuhudia jinsi Bwana Yesu alivyowaponya.

            Siku nyingine tena tukaona watoto na vijana kadhaa, walishuhudia wakiongozana na ndugu zao jinsi walivyopona magonjwa ya akili. Kijana mmoja alikuwa amechanganyikiwa akili toka mwaka 1997, na aliletwa kwenye semina na kijana mwenzake. Wote walikuwa hawajaokoka. Lakini wakati wa semina yule kijana aliyekuwa na tatizo la kuchanganyikiwa akili alipona, kisha wote wawili wakaokoka na kujazwa Roho Mtakatifu! Jina la Yesu libarikiwe sana!

            Tulishuhudia pia ‘wingu’ au ‘upako’ wa Roho Mtakatifu ukiwaponya watu kadhaa waliokuwa wamepata shida ya mifupa kuvunjika katika ajali mbalimbali. Kwa mfano mtu mmoja alisema alipopata ajali alipelekwa hospitali kwa matibabu lakini hata baada ya kupona mguu haukuunga vizuri, na ukawa mfupi kidogo. Kwa hiyo akawa hatembei vizuri kwa kunyooka. Wakati wa maombi katika semina, Bwana Yesu alimponya na kurefusha mguu wake uliokuwa mfupi – na akaweza kutembea vizuri kama vile mtu ambaye hakuwahi kupata ajali!

            Tunaweza kuendelea kuandika juu ya miujiza hii – lakini nafasi haitatosha. Lakini pia itakuwa siyo vizuri kutokukwambia jinsi Mungu alivyowatembelea watoto waliokuwa na shida mbalimbali. Kuna waliokuwa wamepagawa mapepo kishirikina waliyofunguliwa! Kuna mama aliyeshuhudia jinsi mtoto wake alivyoweza kuanza kutembea baada ya kutotembea tangu kuzaliwa! Mtoto mmoja wa miaka 10 alijitokeza kushuhudia jinsi ambavyo Mungu amemponya na tatizo la kukojoa kitandani lililokuwa limemsumbua miaka mingi.

            Tunaona tukushirikishe pia ya kuwa katika siku za wiki ya kwanza ya semina hii dada mmoja alishuhudia jinsi  Mungu alivyomponya ukimwi katika semina tuliyoifanya hapo hapo Moshi mjini mwezi wa nane mwaka 2002. Alisema baada ya semina alirudi hospitali kupima tena ambako walimkuta hana ukimwi tena!

Radio!

            Ili kuwafikia watu wengi wakati wa semina, kila siku usiku tulikuwa tunarusha radioni mafundisho tuliyofundisha mchana uwanjani. Radio iliyotumika ni ya ‘Sauti ya Injili Moshi’. Tunaamini Mungu aliwafikia maelflu ya watu pia kwa njia hii. Maana radio hii inasikika mikoa ya Kilimanjaro, Arusha na Tanga.

            Kwa mfano kuna mama aliyejitokeza kushuhudia wakati wa wiki ya mwisho ya semina akisema Mungu amemponya ugonjwa wa ‘High blood pressure’ wakati akisikiliza kipindi chetu cha radio. Mwingine akaeleza jinsi alivyojikuta amejazwa Roho Mtakatifu na kunena kwa lugha mpya aliposhiriki maombi kupitia kipindi chetu cha radioni!

Hospitali Yatembelewa!

            Kwa sababu ya mambo ambayo watu walikuwa wakisimulia ya kuwa Yesu anayafanya uwanjani, habari hizi ziliwafikia wagonjwa waliokuwa wamelazwa katika hospitali ya rufaa ya KCMC iliyopo mjini Moshi. Kwa hiyo wengi wakataka kuja, wengine walituma nguo zao ili ziombewe halafu warudishiwe, na hata wengine waliwatuma ndugu zao waje wasimame katika maombi kwa niaba yao. Kuna mama mmoja ambaye alikuwa na mume wake amelazwa katika chumba cha wagonjwa mahututi kwa tatizo la kubanwa kifua, kiasi cha kushindwa kupumua vizuri na kushindwa kuongea vizuri. Huyu mama alisema alifika katika semina na kila siku wakati wa maombi ya wagonjwa alisimama kwa niaba ya mume wake aliyekuwa amelazwa KCMC. Baada ya kusimama kwa ajili ya maombi kwa siku tatu mfululizo mume wake ‘ghafla’ akafunguka ‘ICU’ na kupona – na kutolewa arudi nyumbani!

            Lakini pia kulikuwa na wagonjwa waliotaka kuja wenyewe kwenye semina ili waombewe. Kwa sababu ya hali walizokuwa nazo madaktari walishauri tuombwe tukawaombee huko huko hospitalini. Tulipoletewa habari hii tukaamua kwenda kuwaombea wagonjwa hao siku ya Jumapili asubuhi tarehe 26 Januari 2003. Viongozi wa hospitali walitupokea vizuri na kutuonyesha orodha ya wagonjwa waliohitaji maombi iliyokuwa na majina zaidi ya mia moja ishirini. Tulipokuwa tunaongozwa na viongozi hao kuwaombea wagonjwa hao; ghorofa kwa ghorofa; na chumba kwa chumba, tuliwaombea hata wale ambao walikuwa hawajaandikisha majina yao lakini walitaka maombi hayo pia. Siku hiyo hospitali ilikuwa na wagonjwa 560 waliokuwa wamelazwa – na tulitumia masaa matatu kuwaombea wote waliotaka maombi katika vyumba mbalimbali vya wagonjwa vilivyopo hapo hospitalini.

            Tulianza kuzungukia na kuwaombea wagonjwa saa 4 asubuhi na tukamaliza saa 7 mchana ambapo tulipelekwa ‘Chapel’ ya hospitali ili kuwaombea wagonjwa wengine waliokuwa wamekusanyika humo. Moja kwa moja tulianza ibada ya kuwaombea wagonjwa na kuimaliza saa 8.30 mchana. Wagonjwa wengi walipona na wengine walipata nafasi ya kushuhudia hapo hapo. Pia, waliookoka watu 62 hapo hospitalini wakiwemo wagonjwa na wauguzi wao vile vile.

Mwisho

            Kristo ni Yote katika Yote na sifa zote ni zake! Maana yote hayo na hata yale ambayo hatukuweza kuandika aliyoyafanya yamefanyika kwa neema na rehema zake. Tunaomba ushirikiane nasi kumshukuru Mungu kwa ajili ya hayo.

            Pia, tunapenda kumshukuru kila mtu aliyetuombea na kuomba kwa ajili ya semina hii. Na shukrani kwa kila aliyetoa fedha yake, mali yake na muda wake ili semina hii ifanikiwe. Mungu awabariki kila mmoja sawasawa na neno lake.

            Tunahitaji maombi kwa ajili ya semina zifuatazo: 16 – 23 Februari 2003 (Arusha mjini), 1 – 9 Machi 2003 (Dar es Salaam) na Tanga mjini tarehe 18 – 23 Machi 2003.

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.