Yesu Akamwambia "Lisha Kondoo Zangu" (Yohana 21:17)
Home
Maombi
Ratiba
Shuhuda
Mafundisho
Maswali na Majibu
Barua za Mwezi
Kuchangia Huduma
MAFUNDISHO MAALUM KWA VIJANA


MAMBO YA KUTAFAKARI KABLA YA KUFANYA
UAMUZI WA KUOA AU KUOLEWA

Wiki ya Kumi na Moja

Jambo la Kumi na Moja
Uko tayari kuishi katika  hiyo ndoa kwa muda gani?

          Sasa ninakupa siri hapa ikusaidie, Kama umekaribia – karibia kuoa au kuolewa, na hujawahi kujiuliza maswali ya namna hii, basi Mungu anakuweka mahali pazuri kwa kukupa nafasi ya kusoma kitabu hiki. Labda nikuambie kitu cha namna hii kitakusaidia, kabla sijakupa mistari mingine kwenye biblia, ni hivi: Hakuna sababu ya kuolewa na kijana ambaye atakufa baada mwezi mmoja. Au hakuna sababu ya kuoa msichana atakayekufa muda si mrefu baada ya arusi yenu.

 Kwa nini uolewe leo uwe mjane baada ya miezi miwili? Na ukiishaolewa umekwisha badilisha kabisa hali yako na ya  mume wako; akiisha kufa wewe sio msichana tena, utaitwa mjane, hata kama umri wako ni mdogo. Tulienda mahali ulani tukasema tunaomba wajane tuwaombee, tulishangaa kuona ya kuwa robo tatu yao walikuwa ni wasichana. Ungeambiwa wameolewa ungekataa, lakini wamefiwa bado wana umri mdogo.

 Sasa mimi ninataka nikuulize swali, kwa nini unataka uolewe, halafu mume wako afe baada ya miezi miwili au unataka uoe mke wako afe baada ya mwezi mmoja, au baada ya mwaka? Hakuna kitu kinachosumbua kama hiki. Ngoja nikueleze hili tena ya kuwa ndoa ya pili sio ndoa ya kwanza. Ndoa ya kwanza ina utofauti wake, na ndoa ya pili ina utofauti wake.

Ikiwa unataka kuishi muda mrefu na mwenzi wako wa ndoa unahitaji;

1.     Kuwa mwangalifu kutii ile mistari ilioko kwenye biblia inayozungumzia juu ya muda wa mtu kuishi. Kwa mfano: Waefeso 6:1-3 inasema; “Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki. Waheshimu baba yako na mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, upate heri, ukae siku nyingi katika dunia”.

Kwa hiyo angalia uhusiano wako na wazazi wako kama bado wako hai. Lakini pia chunguza uhusiano wa huyo anayetaka kukuoa au anayetaka umuoe, na wazazi wake, kama bado wako hai.

2.      Omba Mungu akupe maisha marefu na huyo mwenzako hata kabla hamjaamua kuoana. Ili kama kuna mmoja wenu hataishi muda mrefu – basi Mungu awaarifu na kuwaongoza cha kufanya.

Mwingine anataka aingie kwenye ndoa kwa kubahatisha au kwa majaribio. Maana yake ndani ya nafsi yake anajiweka tayari kuachana na mwenzi wake kama anaona mambo ya ndoa yake hayaendi alivyotarajia. Mtu wa namna hii hataweza kuwa mvumilivu na mwepesi wa kutafuta suluhisho kukitokea tatizo katika ndoa yake.

Uamuzi wa kuoa au kuolewa unamtaka mtu aingie katika ndoa asilimia mia moja. Ikiwa hautakuwa tayari kuingia kwenye ndoa kwa asilimia mia moja – tafadhali usiamue kuoa au kuolewa. Utampotezea tu mwenzako – maana hakuna ndoa isio na matatizo. Lakini pia hakuna tatizo ambalo Mungu hawezi kulitatua. Lakini, je, uko tayari kushirikiana na Mungu katika ndoa kwa kiwango cha asilimia ngapi?.

Mambo ya Kutafakari Vijana / utang / 1 / 2 / 3 / 4 / 5 / 6 / 7 / 8 / 9 / 10 / 11 /

UNATAKA KUOKOKA?
Kama unataka kumpa YESU maisha yako sasa, bonyeza hapa
©2003 Tanzania Social and Economic Trust.  All Rights Reserved.